Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

MHE. DKT. DAMAS D. NDUMBARO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nichangie kwenye suala hili la kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Songea wamenituma nifikishe ujumbe kwa Wizara ya Kilimo na kwa Serikali. Wananchi wa Songea wanasema kwao zao la mahindi ni chakula, kwao zao la mahindi ni biashara, kwao zao la mahindi ni siasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Songea wanasema hawana viwanda wanategemea mahindi. Wananchi wa Songea wanasema mahindi ndiyo uhai wao lakini sasa hivi wana kilio kikubwa sana. Katika msimu uliopita mbolea haikupatikana kwa wakati. Katika msimu uliopita bei ya mbolea ilikuwa inabadilika kama homa za vipindi. Katika msimu uliopita upatikanaji wenyewe wa mbolea ulikuwa ni shida na ukiwanyima mbolea maana yake umewaua kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Songea wanajitahidi sana kuzalisha mahindi. Takwimu za mwaka 2015/2016 wananchi wa Songea na Mkoa wote wa Ruvuma walizalisha mahindi tani milioni 1.9. Mahitaji na matumizi kwa mkoa mzima ni tani 400,000, hivyo kulikuwa na ziada ya tani milioni 1.5. Uwezo wa NFRA kununua ilikuwa ni tani 10,000 tu ambayo ni sawasawa na asilimia 0.7 ya ziada yote. Hii inamaanisha kwamba kulikuwa na asilimia 99.3 ya uzalishaji ambao haukuweza kununuliwa, ni ziada hii. Sasa NFRA hawawezi kununua, soko la nje mipaka imefungwa, huku ni kuwaumiza na kuwaua wakulima wa mahindi wa Songea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu tunategemea tuzalishe mahindi kwa wingi zaidi kuliko mwaka jana na yale ya mwaka jana bado hatujauza. Tunaiomba Wizara, kuna option mbili tu hapa; tuongeze fedha NFRA za kununua mahindi na kama hilo haliwezekani tufungue mipaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kule Songea tuna bahati tuna mipaka miwili, Malawi na Msumbiji, turuhusuni tuuze mahindi. Hakuna sababu ya kumtaka mkulima ambaye amelima kwa juhudi zake, amevuna kwa juhudi zake na hii ni ziada, Serikali inathibitisha kwamba ni ziada, auze kwa kibali, kwa nini? Tunaomba suala la mahindi Songea lipewe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kutokana na ugumu wa suala la mahindi, wananchi wa Songea pamoja na wananchi wa Jimbo la Peramiho wameanza kulima strawberry na wanategemea ndege ambayo Mheshimiwa Rais aliipeleka Songea (Bombardier), ibebe zile strawberry kwenda Dar es Salaam kwenye soko lakini sasa hivi ile ndege haipo, haiendi tena Songea mnazidi kutuua. Tunaomba mturudishie ile ndege iendelee kubeba zile strawberry. Mheshimiwa Jenista wananchi wetu wanataka ile ndege itubebee strawberry zetu na kuzipeleka kwenye soko Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu alipotembelea Songea aliagiza Kiwanda cha Tumbaku kifufuliwe. Katika speech ya Mheshimiwa Waziri ameahidi kiwanda kitafufuliwa lakini hajasema ni lini kitafufuliwa. Naomba Mheshimiwa Waziri aje na kauli thabiti ni lini Kiwanda cha Tumbaku Songea kitaanza kufanya kazi angalau atufute machungu sisi wananchi wa Songea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kunipa tani nyingi sana katika ujenzi wa vihenge. Songea ametoa tani 81,000 lakini capacity hiyo haina maana kama ununuzi wake ni mdogo. Kwa nchi nzima ununuzi ni tani 30,000 maana ile shilingi bilioni 15 inaweza kununua tani 30,000 tu, sasa hizi tani 81,000 alizonipa zitakuwa hazina faida kama NFRA hawawezi kununua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niongelee suala la mbolea hasa hii mbolea ya Minjingu. Kinachofanya mahindi yaweze kuzaa vizuri ni nitrogen katika mbolea ile. Minjingu ni mbolea ambayo ina nitrogen kidogo zaidi kuliko mbolea nyingine, percent ya nitrogen ni 9, sasa mkiandelea kutulazimisha kutumia mbolea ya Minjingu wakati kuna tatizo hili la kitaalam hamtatusaidia. Ni wazo zuri la kufufua viwanda vya ndani lakini nalo liangaliwe. Tunachotaka sisi mbolea ambayo inatumika iweze kutumika vizuri, iweze kusaidia uzalishaji siyo tu kukuza mahindi. Kwa hiyo, hili suala la kulazimisha kutumia Minjingu nalo tuliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ameongelea mambo mtambuka katika bajeti yake na mimi naomba niongee mambo mtambuka katika hoja yangu. Moja, nimelisema hatuna viwanda sisi, kiwanda chetu ni mahindi lakini pili kama tukiruhusiwa kuuza soko letu ni Msumbiji, barabara ya kwenda Msumbiji ni ya vumbi, inapitika kwa shida. Kwa hiyo, huku NFRA hawanunui mahindi, soko la nje limefungwa, hata likifunguliwa barabara ni mbovu. Kwa hiyo, tunaomba hilo nalo liangaliwe ili na sisi tuweze kuuza mazao yetu nchi nyingine za jirani ikiwemo Msumbiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ametembelea Songea na anajua kwamba Songea mbolea ndiyo kila kitu. Nitaomba atakapokuja kuhitimisha aje na kauli thabiti kuwahakikishia wananchi wa Songea kwamba msimu huu unaokuja watapata mbolea kwa wakati, kwa bei nafuu na kwa bei ambayo itakuwa ni moja kwa msimu mzima. Mpango ambao umewekwa wa kununua mbolea kwa pamoja ni mzuri sana, lakini ni sawa na mtu kununua gari zuri, kuwa na hilo gari zuri ni kitu kimoja lakini kuliendesha ni kitu kingine. Tunataka usimamizi na utekelezaji wa mpango huu wa kununua mbolea kwa pamoja (bulk procurement) ufanyike kwa ufanisi wa hali ya juu ili kuondoa hii kero ambayo imewakuta wananchi wa Songea katika msimu huu.