Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Kilimo

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kupata nafasi ya kwanza kuwa mchangiaji wa Wizara hii muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri kwa wasilisho la Wizara hii ya Kilimo lakini nimpongeze kwa jitihada ambazo alizifanya kwenye Mkoa wa Katavi, kuwaruhusu wananchi wa Mkoa ule waweze kulima zao la pamba. Tunakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwenye zao la tumbaku. Zao la tumbaku lilikuwa linachangia pato kubwa sana la Taifa na wakulima wa zao hilo kupata fedha nyingi ambazo zilisaidia jamii kwenye maeneo yanayozalisha zao la tumbaku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo matatizo ambayo yamelikumba zao hili la tumbaku. Tatizo la kwanza ni mabadiliko yaliyosimamiwa na Serikali ya kubadilisha mfumo wa kuuza tumbaku badala ya kuuza kwa dola sasa inauzwa kwa shilingi ya Kitanzania. Maamuzi hayo tuliyoyatoa yamewapa umaskini wakulima wa zao la tumbaku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mjadala wa bei ulipokuwa unajadiliwa kilo moja ya tumbaku wastani wa dola ulikuwa Sh.2,246 leo hii dola moja ni sawa na Sh.2,289. Mkulima huyo atapoteza kwa kila kilo Sh.43 ukizidisha kwa kilo ambazo zitazalishwa kilo milioni 63, mkulima wa zao la tumbaku atapoteza karibu shilingi bilioni 4.77. Naamini ukifika mwisho wa msimu mkulima huyu anaweza akawa amepoteza shilingi bilioni 5. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, maamuzi mengine ambayo tunayafanya na Serikali tunayabariki, yanaleta umaskini kwa wakulima wa nchi hii. Ifike mahali Waziri ashuke chini akasikilize kilio cha wakulima wa zao la tumbaku, akaangalie mapato ambayo yanapotezwa kwa sababu ya maamuzi mabovu. Naomba hili mlifanyie kazi. Kima nilichowatajia cha shilingi bilioni 4 mpaka shilingi bilioni 5, tunakipoteza kwa sababu ya kushindwa kuwa na usimamizi mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine kwenye zao la tumbaku ni juu ya mfumo wa uagizaji wa pembejeo. Zao la tumbaku lina kalenda yake. Haiwezekani unaagiza pembejeo kwa kuchelewa ukitegemea kwamba utawasaidia wakulima hawa. Nia nzuri ya Serikali ya kuagiza kwa pamoja, mfumo huo kwa wakulima wa zao la tumbaku haukuwasaidia wakulima, ndiyo maana kila eneo wana bei yake tofauti na ilivyokuwa zamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda Kahama mfuko mmoja unauzwa kwa Sh.74,00, Chunya Sh.96,000, Mpanda Sh.96,000, Tabora na maeneo mengine mpaka Sh.98,000 lakini walipokuwa na chombo kimoja, wakulima wa zao la tumbaku walikuwa wana uwezo wa kutumia bei moja kwa nchi nzima. Naomba Mheshimiwa Waziri, atakapokuwa ana-wind up hotuba ya Wizara hii, watafute majibu ya suluhu ya kuwatafutia chombo ambacho kitawasimamia wakulima wa zao la tumbaku ili waweze kusimamia zao lao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni zao la pamba. Serikali imefanya kazi nzuri ya kuhamasisha wakulima wa zao la pamba katika nchi yetu. Karibu maeneo yote wamelima na wameitikia wito wa Serikali. Niwaombe sana Serikali iangalie ni jinsi gani wakulima hawa wa zao la pamba watapata soko lao vizuri. Niwaombe sana mliangalie hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yangu ya Tanganyika ambayo ndiyo imeanza kulima zao la pamba hawajajipanga vizuri juu ya kuweka msimamo wa kununua zao la pamba kupitia kwenye ushirika, watanunua vipi ile pamba? Naomba Waziri atupe majibu. Mfumo uliopo wamelima bila kupitia kwenye ushirika na ushirika haukuandaliwa, naomba na hili mlifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni zao la mahindi. Wakulima wa mahindi, mpunga, mbaazi na mazao mengine wamekuwa watumwa katika nchi yao. Mkulima wa mahindi ndiye pekee katika nchi hii anayeonewa, anapangiwa bei ya kuuza mazao yake hapewi nafasi ya kuyauza mazao mahali ambapo anahitaji kuyauza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba muwaonee huruma wakulima wa mazao ya tumbaku na mpunga. Hawa wakulima ndiyo wamekuwa watu ambao wanalinda mfumuko wa bei, kitu ambacho siyo sahihi. Mkulima wa zao la mahindi ama mpunga asipewe mzigo wa kulinda mfumuko wa bei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii sukari inauzwa Sh.3,000 mpaka Sh.2,800, kwa hiyo mkulima wa kijijini akitaka kununua sukari ya kilo 10 lazima abebe gunia mbili ndiyo anunue kilo 10. Haiwezekani! Fikeni mahali mbadili mfumo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Waziri waimarishe Kitengo cha Ununuzi wa Mazao. Kwenye bajeti nimeangalia, mmetenga shilingi bilioni 15 kwa ajili ya kununua mazao, ambapo uhalisia mnahitaji shilingi bilioni 86 kwa mujibu wa Kamati ya Kilimo. Niombe mfuate maelekezo ambayo Waheshimiwa Wabunge wanayatoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani, mwananchi tajiri awe anapata unafuu kwa mwananchi kutoka kijijini. Mwananchi wa kati analishwa na mwananchi wa kijijini, mwananchi mzururaji wa nchi hii analishwa na mwanakijiji ambaye yuko kule kijijini, haiwezekani! Naomba Waziri aje na majibu ya msingi, wawaruhusu wakulima wauze mazao yao mahali popote wanapotaka. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mfumo wa pembejeo, Serikali ilikuja na nia njema lakini haijawasaidia wananchi. Pembejeo hazikufika kwa wakati na kulikuwa na urasimu mkubwa. Naomba Waziri aje na majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kwenye ushirika. Serikali mmesema kwamba mtaanzisha Tume ya Ushirika, kwenye Tume ya Ushirika hamna kitu chochote kilichofanyika. Vyama vya Ushirika vinasimamiwa na Tume hii ya Ushirika, hampeleki fedha watajiendesha vipi? Katika wafanyakazi ambao wanashida nchi hii ni wanaushirika. Maafisa Ushirika wamebaki na jina tu kuitwa Maafisa Ushirika lakini uhalisia hakuna kitu chochote kinachofanyika. (Makofi)