Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie Wizara hii ya Ulinzi. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Katibu Mkuu, Mkuu wa Majeshi na Makamanda wote na Wanajeshi wote kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusicheze na amani jamani. Mimi nawasikitikia sana wanaotaka kuvuruga amani ya nchi hii. Tutakimbilia wapi sisi Watanzania, nchi zote ambazo zinaizunguka Tanzania, hakuna amani, tutakwenda wapi? Kwa hiyo, naomba sana Watanzania hii amani tuliyonayo ni tunu, kwa kweli tuilinde amani yetu ili Askari wetu hawa wasipate kazi kubwa ya kuhangaika kuzuia vurugu ndogondogo hizi. Mipaka yetu yote ni shwari, kwa hiyo naomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Mkuu wa Majeshi kwa kurejesha Kambi ya JKT Mpwapwa. Nimeiomba Kambi ile muda mrefu bado yuko Mkuu wa Majeshi Waitara, bado yuko Mkuu wa Majeshi hawa wastaafu Mboma, mpaka ndugu yangu Mwamunyange, hawa wote nimewaomba turejeshe Kambi ya JKT Mpwapwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kambi ile imerejeshwa, lakini bado ina matatizo makubwa, hasa miundombinu majengo ya kuishi Askari. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri atenge bajeti kwa ajili ya kujenga majengo pale. Eneo lile linafaa sana kwa kilimo awapelekee matrekta, itawasaidia sana wale vijana kulima mashamba na waweze kujilisha wao wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu makazi ya Wanajeshi. Naomba sana Mheshimiwa Waziri Wanajeshi wasipange uraiani. Wanajeshi wakae pamoja lakini kukaa uraiani wakati fulani zinatokea vurugu na wananchi. Kwa hiyo nashauri wajengewe nyumba katika kila kambi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usafiri wa Wanajeshi kwenye makambi, haipendezi kukuta Askari wananing’inia kwenye malori. Wakati fulani huwa napita pale Ihumwa yaani nakuta Askari wako barabarani, wakati fulani napata huruma tunasimama na gari yangu napakia watatu, wanne lakini wengine wanaomba lift mpaka kwenye malori. Kwa hiyo naomba tuongeze usafiri kwenye Kambi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu posho au lishe ya Askari wetu. Posho ingeongezwa kwa sababu posho wanayopata sasa haitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, yule Mkuu wa Jeshi aliyestaafu juzi anaitwa Mwakinyange ‘Jenerali Davis Mwamunyange’ samahani sana Mkuu wangu nakosea jina lako, lakini naye alifanya kazi nzuri sana pamoja na wote hao. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nichangie hoja hii na naunga mkono kwa asilimia mia moja.