Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Joseph Leonard Haule

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mikumi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JOSEPH L. HAULE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii nyeti ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha Sukari cha Illovo – Kilombero; kumekuwa na malalamiko makubwa sana ya wafanyakazi waliokuwa wanafanya kazi kwenye Kiwanda cha Sukari cha Kilombero kilichobinafsishwa na Serikali mwaka 1999-2000 ambapo wafanyakazi zaidi ya 3000 mpaka leo hawajalipwa fidia zao na wanapigwa danadana na hawapewi majibu ya kueleweka ya fidia zao, wengi ni watu wazima wengine wanakufa bila kulipwa haki zao na wengine wanategemea fidia hiyo ili waweze kusomesha watoto wao na pia kujiendeshea maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Waziri atakapokuja atupe majibu ni lini wananchi hawa waliokuwa wanafanya kazi Kiwanda cha Sukari Kilombero watalipwa fidia zao ambazo ni haki yao ya msingi? Pia kwenye Kiwanda cha Sukari cha Illovo kumekuwa na malalamiko ya muda mrefu sana ya wakulima wa miwa kuhusu upimaji wa sucrose, upimaji wa mzani na bei ya miwa yao wanayokipeleka kiwandani kutokuwa ya uwazi kabisa, maana vitu vyote muhimu vinafanywa na kiwanda yaani upimaji uzito, utamu na upangaji wa bei wote unafanywa na kiwanda na kuwabana sana wakulima wa nje (out growers). Je, ni lini Serikali itawaamuru wawekezaji hawa kuwapa wakulima mzani huru wa tani za miwa, utamu na ni lini wakulima hawa wataanza kulipwa kutokana na buggers na sprit ambapo sasa hivi wanalipwa utamu wa muwa peke yake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda kidogo cha sukari cha Mufilisi – Mikumi; Serikali kwenye bajeti ya 2015/2016 ilikuja na bajeti na kusema wametenga pesa za kuanzisha Kiwanda cha Sukari cha Mufilisi. Je, zoezi hili limeishia wapi? Maana sasa kwenye bajeti hatuoni tena likizungumzwa na halipo kabisa. Je, Serikali inaweza kutuambia tumekwama wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vya kusindika nyama, nyanya, ngozi, maziwa, viazi na matunda na mboga mboga, mbaazi; Mheshimiwa Waziri Wilaya ya Kilosa tumebarikiwa mifugo mingi sana na wingi huo wa mifugo unasababisha changamoto kubwa sana ya mapigano ya wakulima na wafugaji, kwa sababu wafugaji wamezidiwa sana na mifugo mingi na hawana pa kuwapeleka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali iangalie umuhimu wa kuanzisha viwanda vya kusindika nyama, ngozi, maziwa ili wafugaji hawa wapate uhakika wa soko la kuuza mifugo yao na kupunguza mifugo yao tofauti na sasa ambapo tunawaambia wafugaji wapunguze mifugo yao. Je, waipeleke wapi wakati hawana masoko ya uhakika ya kuuza mifugo yao, naomba Waziri uliangalie sana hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vya kusindika nyanya, viazi, mbogamboga, mbaazi na matunda; wakulima wengi wa Wilayani Kilosa wanalima sana mazao haya na mengine mengi, kitendo cha kukosa soko la uhakika kinawapa umaskini mkubwa sana na kuwakatisha tamaa ya kuendelea kulima wakati wote, tunajua kilimo ndio uti wa mgongo wa Taifa letu. Tunaomba sana Serikali itusaidie jimboni Mikumi tupate viwanda vya kusindika mazao haya ili tuweze kumkomboa mkulima wa Mikumi na Wilaya ya Kilosa kwa ujumla hasa kwenye kata zinazoongoza kwa kilimo kama Kata za Kisanga, Tindiga, Mabwerebwere, Vidunda, Malolo, Kilangali, Mhenda, Zombo, Ulaya, Masanze, Ruaha, Mikumi, Kidodi, Ruhembe na Uleling’ombe. Hili naomba majibu ya Waziri ni lini watatujengea viwanda vya kusindika mazao jimboni Mikumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, COSOTA; bajeti inayopelekwa na kutengwa kwenye taasisi hii muhimu ni ndogo sana na inapelekea COSOTA kushindwa kutimiza wajibu wake sawasawa. COSOTA ni chombo muhimu sana kinapaswa kiangaliwe kwa jicho la kipekee sana maana ndicho chombo kinachoweza kuwasaidia wanamuziki wetu wa Tanzania kwenye wizi wa kazi zao ambacho kimsingi wizi wa kazi za wasanii ndicho kilio kikubwa sana cha wasanii wetu Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Sheria ya Hakimiliki na Hakishirika Namba 7 ya mwaka 1999 imepitwa sana na wakati na imekosa meno kabisa, niiombe sana Serikali kama kweli ina nia thabiti na dhamira ya kweli ya kuwasaidia wasanii wa nchi hii basi ilete muswada wa sheria hii Bungeni ili tuweze kuirekebisha na kuipa nguvu ili tuweze kuwakomboa wasanii wetu wengi waliojiajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwekezaji, Jimbo la Mikumi lina ardhi nzuri na bora tena kubwa sana na tumebarikiwa sana kuwa na vyanzo mbalimbali na vingi vya maji kwenye mito mbalimbali na ardhi yetu maji yapo juu kabisa kwa maana ya water table. Tunaomba sana Serikali iweze kutupatia ardhi kubwa sana ambayo imetekelezwa na wawekezaji ambao wanahodhi mashamba hayo makubwa bila kuyaendeleza. Kurudishwa kwa mashamba hayo kutawezesha sana wawekezaji wengi kuweza kuja jimboni kwetu Mikumi na Wilayani kwetu Kilosa ili tuweze kutoa ajira zaidi kwa Wanamikumi na pia kuweza kuleta maendeleo kwa wanakilosa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho tunaomba sana Serikali itupie macho kwenye Jimbo la Mikumi ili waweze kutuletea wawekezaji maana Mikumi inajitosheleza katika kila sifa inayotakiwa na wawekezaji ili waje na kufanya uwekelezaji hasa kwenye masuala ya kilimo, utalii na viwanda. Ahsanteni sana na karibuni sana.