Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kunipa fursa hii ya kuchangia hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara. Nitangulize kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri na kwa utekelezaji mzuri wa ilani, nampongeza yeye, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu na watendaji kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa utekelezaji wa mkakati huu wa ujenzi wa viwanda. Hili jambo ni jambo adhimu, ni jambo zuri ambalo litaweza kutupelekea sisi mwaka 2025 kufikia hadhi ya nchi ya uchumi wa kati na hili ni jambo la ukombozi pia kwa vijana wetu wa kike na kiume wa Tanzania kwa sababu katika matatizo makubwa ambayo vijana wanayapata ni tatizo la ajira, hili ni tatizo namba moja. Kila kijana awe wa chuo, awe wa shule ya msingi, awe wa sekondari na kadhalika shida yake kubwa ni ajira na viwanda ni ajira kwa hivyo tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa mkakati huu wa ujenzi wa viwanda katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imepanga vizuri na kutenga maeneo ya EPZ na SEZ na maeneo haya ni maeneo muhimu sana yanatoa fursa moja nzuri sana, yanatoa fursa ya kujenga viwanda katika mpangilio mzuri na katika hali ambayo mazingira yanalindwa vizuri kwa maana unaweza mkaamua kwamba hapa ni viwanda vya madawa, hapa vya nguo, kule vya chuma na kule vya chaki bila muingiliano usiokuwa na mpangilio kwamba mtu anaamua huyu anaweka hapa cha tofauli na mwingine anakuja hapo hapo anaweka cha battery, mwingine anakuja hapo hapo anaweka kiwanda cha alizeti, kwa hiyo inakuwa shaghala baghala hakuna mpangilio mzuri. Naiomba Serikali yetu iweke mkazi mkubwa iweze kuhakikisha kwamba maeneo maeneo haya ya EPZ na SEZ yanafanyiwa kazi kwa umuhimu na kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1979 China iliamua kwamba itenge eneo la mfano la viwanda ikachangua SEZ ilikuwa na watu 30,000 tu pale sasa hivi ina watu zaidi ya milioni 11 na viwanda ambavyo vina mpangilio mzuri na vinatoa tija kubwa sana na huo ndiyo mfano ambao inabidi twende nao na kwa haraka. Tumechukua muda mrefu sana, tumezungumza sana lakini vitendo vimekuwa nyuma, kwa hivyo sasa ni wakati ambao Mheshimiwa Rais ameshaweka nia yake lazima tufanye sasa huu ndiyo wakati sasa wa kuweza kutekeleza jambo hili kimakini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Bagamoyo Serikali imetenga eneo la EPZ, imetenga kwa awamu mbili, awamu ya kwanza jumla ya hekta 5,742 kwa ajili ya ujenzi wa viwanda na mpaka hivi sasa tayari imeshalipia hekta 2,399 isipokuwa kuna wananchi 1,025 ambao mpaka hivi sasa hawajalipwa fidia zao katika maeneo hayo, kwa maana ni miaka 10 sasa tangu eneo hili limetengwa na wananchi wakatathminiwa lakini hawajalipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale ninaposema kwamba tufanye uharaka, basi uharaka unaanzia kupata ardhi ambayo iko free, haina tatizo na mwananchi yoyote kwamba walipwe hawa mapema iwezekanavyo ili eneo hili sasa wawekezaji waanze kulitumia kwa ajili ya kujenga viwanda ambavyo viko katika mpangilio mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba sana Mheshimiwa Waziri, juhudi kubwa najua anaifanya lakini kwa sisi kule Bagamoyo nguvu zake tutaziona tu kwamba zimekuwa za kutosha kama pale ambapo tutakuta kwamba fidia hizi zimelipwa kwa haraka ili eneo hili liweze kuwa free na viwanda vianze kujengwa bila hivyo ujenzi wa viwanda unakuwa mgumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na stahiki ya fidia hii na hasa kwa sababu najua kwamba sasa hivi mwekezaji ana jukumu la kulipa fidia na kwa hiyo wawekezaji hawa wapo tayari kulipa fidia, basi niiombe Serikali ifanye haraka sana kuweza kuwapa ruhusa au kuwasukuma ili waweze kulipa fidia zao mapema iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili la EPZ, eneo la Awamu ya Pili la EPZ jumla yake ni hekta 3,338 hili eneo hili linajumuisha maeneo yenye makazi makubwa ya wananchi na limeingia kwenye EPZ bila ya wananchi kuridhia kwamba liingie kwenye EPZ. Linajumuisha Kijiji cha Zinga, Kijiji cha Mlingotini, Kijiji cha Pande na Kijiji cha Kiromo na Kijiji cha Kondo. Vijiji hivi ni vya zamanai na vimejengwa, vina wananchi wengi sana wamejenga kwa miaka mingi wako mle tayari wameshatoa eneo la zaidi ya hekta 5,000 kwa ajili ya EPZ. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaomba chonde chonde tafadhali Mheshimiwa Waziri wananchi hawa waruhusiwe kuishi katika maeneo yao haya kwa amani na usalama na hasa kwa kuzingatia kwamba wameshatoa maeneo ya kutosha kwa ajili ya EPZ eneo ambalo ni mji mzima kabisa tunaweza tukapata SEZ nyingine katika Jimbo la Bagamoyo kwa kuchukua tu eneo lile ambalo tayari limeshakubaliwa katika awamu ya kwanza. Naomba kwa heshima na taadhima Serikali ikubali kuwaaachia wananchi hawa jumla ya kaya 3,381 kwa sensa ya mwaka 2012 ama wananchi 12,797 hawa wataathirika maeneo yao ambayo tayari yameshajengwa, ni vijiji vinavyojulikana kuingizwa kwenye EPZ na kuambiwa kwamba waweze kuondoka kwa ajili ya kujenga viwanda.

Mheshimiwa Waziri utakuwa umefanya jambo zuri sana na la muhimu sana kwa wananchi hawa kama utaweza kusimamia kuhakikisha kwamba wananchi hawa wanaweza kuendelea na maisha yao kwa amani na usalama katika maeneo haya bila kubughudhiwa tena kuweza kuhama kupelekwa maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili la SEZ Bagamoyo kuna eneo la ujenzi wa bandari ambalo waziri anahusika moja kwa moja na analisimamia kwa uzuri na alifuatilia, ameshafanya safari mpaka China kwa ajili ya kufuatilia ujenzi wa bandari hii, lakini wananchi hawa wanaopisha ujenzi wa bandari, jumla ya kaya 460 wao wananchi hawa mpaka hivi sasa hawana eneo mbadala la kwenda kuishi na kwa bahati Serikali iliwahi kuahidi kwa maandishi kwamba watapewa eneo mbadala la kwenda kuishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu tukufu, namuomba Mheshimiwa Waziri chonde chonde ahakikishe wananchi hawa wa Kijiji cha Pande na sehemu ya Kijiji cha Mlingotini ambao wanapisha ujenzi wa bandari wapatiwe eneo lile la makazi mbadala ili waende wakaanze maisha mapya katika eneo hilo ama sivyo watakuwa ni watu ombaomba tu ambao tutakutana nao miaka inayofuata hawana mahali pa kuishi, wako hovyo, wanamuangalia Mbunge wanamuona hafai, hana maana kwa maana kwamba wao walikuwa wamekaa mahali pazuri, wanapopapenda lakini sasa leo imekuja bandari imewafanya wawe watu ombaomba, watu masikini wa kutupa. Naiomba Serikali chonde chonde ihakikishe kwamba suala la resettlement kwa wananchi hawa wa Pande na Mlingotini ambao tayari walikuwa wameshaahidiwa na Serikali basi waweze kupatiwa maeneo yao waweze kuanza maisha mapya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo ninashukuru sana, ninaunga mkono hoja, ahsante sana.