Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hotuba ya Wizara ya Viwanda na Biashara ambayo ni Wizara muhimu sana hasa kwa Serikali ya Awamu ya Tano kwa sababu ni Serikali ya viwanda na kwa ajili ya kukuza uchumi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri, Naibu Waziri na timu yake yote ya wataalam pamoja na watu wote wanaomsaidia, wanafanya kazi vizuri sana. Ni kweli pamoja na kwamba watu wanasema labda Mheshimiwa Mwijage anaongea kwa utani lakini kwa jinsi navyomwangalia nafikiri yupo serious ndiyo sababu hata Mheshimiwa Rais amemwamini kwa kipindi chote hicho amebaki kuwa Waziri wa Viwanda na Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa ambacho nataka nichangie kwenye Wizara hii, naona tumejikita mno kwenye viwanda, hatujaangalia biashara. Leo hii ukiniuliza hata mimi, masoko yako kwa nani? Yako kwa Wizara ya Viwanda au yako Kilimo au Mifugo au yako kwa nani, sijui. Wakulima wanahangaika na sehemu ya kuuza mazao yao. Ni nani mwenye jukumu hilo, hatuelewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwenye kilimo, tumehangaika kuhusu mahindi hapa, aliyesulubiwa ni Waziri wa Kilimo. Nimezungumza kwa muda mrefu kuhusu pareto hapa. Nilikuwa naongelea kupitia kwa Waziri wa Kilimo lakini leo hii nilipoangalia hotuba hii, nikakuta kuna chombo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara kinaitwa TANTRADE, kazi yake ni kutafuta masoko ya viwandani na mazao. Jiulize humu ndani kama kweli hawa watu hizo kazi wanazifanya zaidi ya Maonyesho ya Sabasaba. Inabidi tusifumbiane macho, tunapata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwangu nalima pareto. Nimeongelea kuhusu pareto mpaka Wizara imeamua iifute pareto kwenye mazao manne ya kimkakati Tanzania wakati pareto tunayolima Tanzania tunaongoza Afrika na ni ya pili duniani. Sasa uangalie ni kwa kiasi gani wakati mwingine tunafanya vitu vya ajabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pareto tunayozalisha leo hii haizidi tani 1,000 ndiyo tumejitahidi sana, lakini potential ni karibu tani zaidi ya 10,000, ndiyo inatakiwa duniani. Kwa nini hatufiki huko? Kwa sababu mnunuzi ni mmoja. Ni nani alitakiwa atutafutie wanunuzi? Ni huyu mtu anaitwa TANTRADE au Wizara ya Viwanda ba Biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachomwomba Mheshimiwa Waziri aje na mkakati ni namna gani atusaidie Tanzania kwa sababu potential tuliyonayo Tanzania ni kuwa wazalishaji wakubwa wa pareto duniani. Leo hii pareto tunaiuza mkulima anapata kwa bei kati ya Sh.2,300 mpaka Sh.2,700 lakini ukipeleka sokoni moja kwa moja, wale wanaonunua wanapata kati ya Sh.8,000 mpaka Sh.10,000 na hiyo ni kwa vile ni biashara wanaotuchezea. Anayenunua na anayezalisha Tanzania ndiyo huyo huyo anayenunua Marekani. Anapeleka Marekani kama crude, anakwenda kuichakata kule na sisi Tanzania hatuonyeshwi kama ndiyo tumeizalisha hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kiwanda kilianzishwa Inyala kikajaribu kupeleka pareto nje, wale waliponunua na kuingia mkataba, wakatishiwa kwamba kwa sababu mnanunua pareto kwa huyu mzalishaji mwingine kutoka Tanzania, nasi ndiyo tumekamata zao la pareto duniani, basi hatutawaletea tena pareto, kwa hiyo, wale watu wakaogopa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona kuna chombo chini ya Wizara hapa kinaitwa FCC kama sikosei na kazi zake, sijui kama haya wanayaona ya kwamba zao ambalo tunaongoza Afrika, hata FCC sijui kama wanajua ni kiasi gani wakulima wananyonywa? Mnunuzi ni mmoja, ame-dominate soko la pareto ndiyo giant duniani. Tukiendelea namna hii tutakuwa tunamsaidia vipi mkulima wa Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho nilitaka nichangie kidogo ni kuhusu kufufua viwanda. Watu wameongelea kuhusu kufufua viwanda na Mheshimiwa Waziri ametamka kuwa ana nia ya kufufua Kiwanda cha Nyama kwa kutafuta mnunuzi wa Kiwanda cha Nyama cha Tanganyika Packers kule Mbeya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nimfahamishe Mheshimiwa Waziri, tuna kiwanda ambacho kimejengwa na Halmashauri. Ni kiwanda cha thamani ya shilingi bilioni 2, kimejengwa kwa asilimia 90. Vifaa ya UNIDO vimeshawekwa mle ndani na sasa hivi Halmashauri inaomba pesa kidogo tu kama shilingi milioni 900 ili waweze kumalizia. Kiwanda hiki ni cha kisasa na ni kizuri kuliko hicho ambacho wanataka kufufua sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanganyika Packers ilijengwa kabla ya mwaka 1970, yale mashamba sasa hivi yamezungukwa na jiji, yako mjini. Kuna ekari pale karibu 5,000 ziko mjini na mjini huruhusiwi kufuga wala kulima zaidi ya ekari tatu. Sasa unakuta Mheshimiwa Waziri naye anasimama anasema tunatafuta mwekezaji kwa ajili ya Tanganyika Packers. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba muwe mna- coordinate. Halmashauri imeomba lile eneo wapewe na wao wametoa ekari 7,000 kwenye sehemu ambayo ndiyo kuna ng’ombe wengi iwe kama holding ground, lakini tubakize kiwanda, kutoka pale ni kilomita 30. Wizara ya Ardhi walishauja, Naibu Waziri wa Ardhi alikuja, Katibu Mkuu wa Ardhi alikuja, wote waka-recommend nami mwenyewe nimeongea na Treasury Registrar akaona hilo ni wazo zuri ili lile eneo sasa ambalo lilikuwa ni la Tanganyika Packers libadilishane na hili eneo, Halmashauri iliendeleze hili eneo kwa ajili ya kuupanga mji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hilo ni karibu kabisa na Songwe International Airport. Sasa badala ya kutenga maeneo kwa ajili ya EPZ unataka wewe ukachungie ng’ombe, nafikiri hivyo ni vitu ambavyo katika dunia ya leo havikubaliki. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hilo kwa makusudi kwa vile hiki kiwanda ni kwa ajili ya soko la ndani na nje. Kiwanja cha ndege sasa hivi kimetengenezwa ili kiwezeshe ndege kubwa kutua Mbeya ziende moja kwa moja Ulaya, tuweze kupeleka nyama kutoka Mbeya kwenda Ulaya na tupeleke maparachichi na kadhalika. Kwa hiyo, hatukatai Kiwanda cha Nyama ila tunachosema ni mfumo gani tuuchukue ambao unaendana na leo? Ile spirit ya 1970 huwezi ukaitumia hiyo hiyo mpaka leo ukawa unaimba humo Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho napenda kuchangia kidogo ni hii taasisi mpya ya inaitwa Tanzania Commodity Exchange Market, ni nzuri mno na inaweza kuwa mkombozi. Sasa ndiyo hivyo ambavyo nachanganyikiwa kwamba, je, itakuwa chini ya nani; Wizara ya Viwanda, Wizara ya Fedha au labda Wizara ya Kilimo? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hilo kwa makusudi. Kilimo sasa hivi walikuwa wanahangaika jinsi ya kuuza kahawa. Unajaribu kuangalia, je, kuuza kahawa ni Wizara ya Kilimo, au ni Wizara ya Viwanda au ni TANTRADE? Sasa Wizara ya Kilimo badala ya kuboresha kilimo wanaanza kuhangaika na kutafuta masoko. Nafikiri tutapoteza mwelekeo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hivi vitu tuvifanye kwa makini. Imarisha Tanzania Commodity Exchange, tuige Ethiopia, Nairobi wana soko la kuuza kahawa. Tanzania tunauza kahawa kwa kilo 50 dola 150 wakati Nairobi ni kati ya dola 350 mpaka 400 na Ethiopia ni zaidi hapo. Sasa angalia ni kiasi gani uchumi wa nchi hii tunavyoupoteza kwa kutokuwa na mipango mizuri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba hili wenzetu nao wakajipange vizuri. Zao la kahawa liingie moja kwa moja kwenye Tanzania Commodity Market Exchange. Kwa sababu gani TCB wao ni regulator, huwezi ukamfanya regulator vilevile akawa ni muuzaji. Sisi wengine ni wakulima wa kahawa, unaona kabisa kuna watu pale wanajifanya wana mnada lakini wanaangalia kahawa ya leo ya Tanzania tununue kwa shilingi ngapi? Tumenyonywa kiasi cha kutosha, naomba tubadilike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa Wakala wa Vipimo. Amezungumza Mheshimiwa Lwenge akafikiria labda viazi vya kutoka Mporoto ambako ndiyo Jimboni kwangu labda kuna nafuu, sisi ndiyo kuna usumbufu mkubwa, hatulali. Magari yanakuwa yamebeba viazi, wakulima maskini amekodi gari tani saba siyo ya mtu mmoja, hana hela, akiuza Dar es Salaam ndiyo apate nauli ya kumrudishia mwenye gari lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naunga mkono hoja.