Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii kukushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia kwenye sekta hii ambayo ni kipaumbele cha Taifa na vilevile ni Dira ya Taifa kupitia Mpango wa II wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda vilevile niipongeze sana Wizara kupita kwa Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu na Watendaji wote kwa sababu kwa kweli utaona wanafanya kazi na kama walivyoeleza kwamba viwanda vinaongezeka, niwapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli kwa kuonyesha dhamira yake ya dhati ya kujenga Sekta ya Viwanda katika Taifa letu. Ukikuta Rais ameonyesha dhamira yake nina hakika Watanzania wote watajielekeza huko na naomba tufanye hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais katika hotuba yake ndani ya Bunge hili, alisisitiza kuwa sekta ya viwanda ina jukumu kubwa la kuipeleka Tanzania kwenye uchumi wa kati ifikapo 2025. Toka alipozindua Bunge hili, dhamira ya Rais inatupa uhakika wa kufikia azma hiyo.

Mheshimiwa Spika, vilevile nilimuona Mhesimiwa Waziri wa Fedha, akizindua kitabu kilichoandikwa na Watendaji Wakuu wa Serikali kilichoelezea changamoto ambazo zinaikabili azma yetu hii, kama ifuatavyo:-

(i) Ukosefu wa vipaumbele madhubuti;

(ii) Sera thabiti;

(iii) Ukosefu wa umeme wa uhakika;

(iv) Ukosefu wa mitaji;

(v) Ukosefu wa uzalendo wa kiuchumi; na

(vi) Ukosefu wa mfumo mzuri wa elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuwe na viwanda hayo yote ni muhimu. Nimefurahi sana katika ukurasa wa 140, Waziri wa Viwanda mwenyewe amesema kwamba watajaribu kuangalia Sera ya Viwanda endelevu na ndiyo ilikuwa changamoto ya pili kwamba sera zikipitwa na wakati azma yetu inaweza isifikiwe. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri fanyeni haraka ili tusishindwe kufika kwenye azma yetu ifikapo 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda nizungumzie mradi wa Liganga na Mchuchuma wa chuma na mkaa. Kama Waheshimiwa Wabunge wengine walivyosema, kwanza niipongeze sanasana Serikali kwa kuuweka mradi huu kuwa mradi wa kielelezo. Wamefanya hivyo, umeanzia Awamu ya Nne na awamu hii imeweka umuhimu mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwa uhakika uchimbaji wa chuma ni nguzo muhimu na ni sekta mama kwa kweli, ni viwanda mama au ni viwanda vya msingi. Liangalieni jengo hili thamani yake robo tatu ni chuma uone chuma inavyohitajika nchi hii. Kwa hiyo, tutakavyoharakisha utekelezaji wa mradi huu utasaidia sana nchi hii. Angalieni hata maendeleo ya nchi za Ulaya yametokana na chuma wakati wa Oliver Twist. Angalieni maendeleo ya India, Mahalanaumis alifungwa lakini chimbuko la uchumi wa India leo ni mradi wa chuma kule India. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba tuone hilo, fikirieni kama reli hii ya kati inayojengwa sasa hivi chuma chake kingekuwa kinatoka Liganga ni kiasi gani cha ajira kingebaki Tanzania? Ni kiasi gani cha manufaa makubwa ya uchumi yangebaki Tanzania? Kwa hiyo, naomba sana tuangalie mradi huu ambao unaelezwa toka nikiwa shuleni hata kabla, naomba utekelezaji wake uende kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana miradi kama hiyo incentive zinazoombwa mziangalie, tunaweza tusipate faida lakini baadaye maendeleo ya kiuchumi na ya viwanda yatakuwa ni ya upesi zaidi, iron and steel industry ni chimbuko la maendeleo yote duniani. Angalieni chuma tutakachoagiza nje na kitakavyojenga ajira na uchumi wa nchi ambazo zinatuletea, hayo tunawanyima Watanzania. Nikimwangalia Waziri na azma ya Serikali ya Awamu ya Tano, sina wasiwasi na nina hakika tunataka bati na misumari itoke hapa, kila kitu ambacho kinataka chuma kitoke hapa, tuna uwezo. Chuma kina multiplier effect, sina neno la Kiswahili, kinanufaisha sana sekta zingine kwa haraka. Naomba Serikali iharakishe utekelezaji wa mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda vilevile kuongelea masuala ya biashara, naomba Serikali ijitahidi sana kuweka mazingira bora ya kufanya biashara nchini. Tumejitahidi toka miaka iliyopita lakini sasa tuendelee na jitihada hizo. Jambo kubwa ambalo linafanya sasa biashara iwe ya shida, Waziri wa Fedha yupo hapa ni mzunguko mdogo wa fedha. Mzunguko wa fedha uongezeke lakini ziwe fedha ambazo zinakubalika zisiwe ni fedha chafu. Kama cash haipo biashara haitakuwepo. Kwa hiyo, Serikali iangalie ni namna gani mzunguko wa fedha utaongezeka ili biashara iende na nchi yetu iendelee kupata faida kutokana na biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni mazingira ya uwekezaji, nami ni-declare interest hapa nilikuwa Waziri wa Uwekezaji. Mazingira ya uwekezaji yakiwekwa sawa ujenzi wa viwanda hivi utaenda kwa kasi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo nitalishauri hapa na ambalo limeanza na najua Wizara nayo na Serikali kwa ujumla inafanyia kazi, ni kuwa na One Stop Center. Hatuwezi kuwa na taasisi mbalimbali zinazohusika na ambazo zimetawanyika tukafikiri kwamba mwekezaji atakuwa na uvumilivu awaze kuona kwamba atabaki hapo na hela zake zinabaki benki halafu hazimletei faida hatakubali . Kwa hivyo, naomba tuharakishe hii One Stop Center ianze kufanya kazi. Ukimkamua ngā€˜ombe kama humlishi hutapata maziwa. Kwa hiyo, wawekezaji tuwawezeshe ili waweze kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niongelee juu ya viwanda Hanang. Hanang ni eneo la kilimo, kwa hiyo, viwanda ambavyo vinatakiwa pale ni vya kilimo. Sisi tuna limestone nyingi sana kwenye ukuta wa bonde la ufa na hakuna mahali patakuwa na bei na gharama nafuu kutengeneza cement kama Hanang. Kuna mwekezaji amekuwa anaomba kuwekeza pale mpaka anakata tamaa kwenda Singida lakini hatapata mazingira mazuri kama ya Hanang, ukuta ule wote una limestone. Itigi kuna gypsum ambayo inatakiwa umbali wake ni chini ya kilomita 100. Fikiria Dar es Salaam na Mtwara wanapata gypsum wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana kiwanda hiki kiweze kuanzishwa na tumfanye yule mwekezaji awe na matumaini na kwa hivyo tusimzungushe. Napenda kusema kwamba bureaucracy au urasimu unapaswa utumike kuwezesha viwanda vianzishwe na kurahisha uwekezaji. Naomba tusitumie urasimu kuzuia wawekezaji kuwekeza vinginevyo nchi yetu haitapiga hatua. Nataka niseme kwamba Tanzania ni ya pili Afrika katika ukuaji wa uchumi na naipongeza Serikali kwa hili. Ili maendeleo ya nchi yawe sustainable lazima yapitie kwenye uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Wizara, naunga mkono hotuba ya Waziri na tukizingatia ushauri huu, kazi yangu ni ushauri siyo kupinga. Ahsanteni sana.