Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

Hon. Anthony Calist Komu

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji

MHE. ANTONY C. KOMU: Mheshimiwa Spika, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia bajeti hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Wizara ambayo kimsingi ndiyo inayobeba kaulimbiu ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, Dkt. Joseph Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hiyo kaulimbiu ya Mheshimiwa Rais lakini uhalisia kwa maana ya bajeti haupo. Kwa sababu 2015/2016 bajeti ya kwanza ya Mheshimiwa Rais, utekelezaji kwenye bajeti ya maendeleo kwenye Wizara hii ilikuwa ni asilimia 5 tu, 2017/2018 ikawa asilimia 9.47. Katika hali ya namna hii ukiunganisha hiyo kaulimbiu na majigambo yote yaliyokuwepo na dhamira ya kutaka kuona kwamba tunakwenda kwenye uchumi wa viwanda haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye ripoti ya CAG ambayo inaangalia ufanisi kwenye viwanda vidogo vidogo na vya kati ambavyo mahali popote duniani ndiyo moyo wa mapinduzi ya uchumi wa viwanda, anasema hali si nzuri, bajeti kwenye sekta hiyo imeendelea kushuka katika ngazi zote maana yake mpaka kule kwenye halmashauri zetu, si zaidi ya asilimia 16, kwa hiyo, bado uhalisia unaendelea kuonekana kwamba haupo. Mafunzo kwenye viwanda hivi vidogo vidogo kwenye sekta hii bado yameendelea kushuka, CAG anasema yako kwenye wastani wa asilimia 7 tu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Vituo vya Maendeleo ya Teknolojia ambavyo vilianzishwa na Mwalimu Nyerere mashine ambazo zinatumika mpaka leo zina umri wa miaka 40, amesema Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, siyo sisi tunaosema. Sasa seriousness iko wapi? Ukiangalia CAG anasema, sekta ya viwanda vidogo vidogo na kati inaporomoka kwa asilimia 30 ikilinganishwa na kukua kwake kwa asilimia 5.6. Kwa hiyo, kauli mbiu ya Mheshimiwa Rais ya kujenga Tanzania ya Magufuli ya Viwanda haina uhalisia wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mwenyekiti wa Kamati alivyokuwa anazunguza hapa amezungumzia mazingira ya kufanya biashara Tanzania. Mpaka tunavyoongea hapa sasa hivi sisi ni wa 137 duniani kati ya mataifa 190 kwa mazingira rahisi ya kufanya biashara. Kinachokwenda kupeleka huo ugumu ni nini? Ni matamko ya viongozi wetu wa siasa wa upande huu wa CCM ambayo yanafanya mazingira yetu yawe si ya kutabirika na kwa sababu hiyo uwekezaji unakuwa ni mgumu katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukitaka kupata kupata kibali cha kuanzisha kiwanda hapa pamoja na mbwembwe zote anazosema Mheshimiwa Waziri hapa unaweza ukatumia miezi kadhaa. Kuna marufuku zinatolewa tu kila siku na hata wafanyabiashara waliomo humu ndani wamekuwa wakilalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni-declare interest nilikuwa kwenye Kamati ya Viwanda na Biashara, tulikutana na tatizo hili ambalo Mwenyekiti amelizungumza hapa vilevile la vibali vya sukari ya viwandani. Vipo viwanda ambavyo tunapozungumza sasa hivi vimefungwa kama Kiwanda cha SAYONA kule Dar es Salaam kutokana na sukari yao kuzuiliwa bandarini tangu mwezi wa nane eti uhakiki unafanyika na ukimuuliza Mheshimiwa Waziri anasema hili liko kwa tajiri mwenyewe. Kwa hiyo, masuala kama haya yanaleta shida. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kuna masuala ya hizi mamlaka zetu za udhibiti, TRA, ubabe mtupu na urasimu ambao hausaidiaa nchi hii. Nimeona kwenye magazeti ya leo TRA sasa wanawaomba wafanyabiashara walifunga biashara zao warudi. Hizi kauli za kukinzanakinzana zinatupa shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jana Waziri wa Fedha alikiri kwamba hali ni mbaya na ndiyo maana bajeti hazitekelezeki. Hawawezi kukusanya mapato kwa sababu ya hii mikanganyiko ambayo ipo kwenye uendeshaji wa Serikali yetu. Kwa hiyo, tunawataka waache hayo mambo ambayo wanafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni kushikashika vitu vingi bila ya kuwa na jambo moja ambalo tumeamua kulifanya kwa sababu ya tafiti ambazo tumefanya na tukalikamilisha. Mheshimiwa Zitto hapa amezungumzia Mchuchuma na Liganga. Hivi kweli kama tuna akili sawasawa, tumefanya tafiti zetu na tumedhamiria kweli kuleta mapinduzi na kukomboa watu wetu ni kwa nini hatuutekelezi mradi huu? Tuna mradi wa Bwawa la Kidunda pale Morogoro ambalo linahitaji Dola za Marekani milioni 251 ili tupate umeme, ajira, kusaidia kilimo chetu, ku-stabilize Mto Ruvu na maji kwa ajili ya viwanda lakini jambo hili linaendelea kuwa ni hadithi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati huo huo nilisema hapa juzi, nchi hii inaagiza chakula kwa mwaka kulingana na takwimu za Benki Kuu ya kwetu sisi bilioni 888.5. Hivi jamani hii Serikali haina uchungu na nchi hii? Hivi hawaoni kwamba tungechukua hizo Dola bilioni 251 tukawekeza pale Kidunda tungeweza tukaokoa hizo bilioni 888.5 na baada ya hapo tukaenda sasa kuwekeza katika mambo mengine ambayo kwa kweli mimi naita ni mambo ya kishamba tu, ya kujionyesha. Eti na sisi tuwe na ndege kwa kuwekeza trilioni moja tena sisi kwa sera ya nchi yetu tumeshakubaliana kwamba twende kwenye Private Public Partnership (PPP) hatufanyi. Tungeweza tukaweka hayo masuala ya ndege kwenye hiyo PPP, sasa hivi tunajenga reli ya standard gauge ambayo ni kitu cha maana na muhimu sana lakini tukaenda kwenye utaratibu huo. Tunachukua pesa za Watanzania, badala ya kuwekeza kwenye mambo ya msingi ambayo yatawapa matokeo ya haraka na yatakayosaidia kupiga hatua kwa haraka.