Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia hotuba ya Waziri wa Maji na Umwagiliaji kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na tatizo la tabianchi, maeneo mengi ya Jimbo la Tunduru Kusini yameathirika kwa kiasi kikubwa kwa kukauka kwa mito mingi, hivyo kufanya kuongezeka kwa kukosekana kwa maji katika vijiji vingi sana. Kuna uhitaji mkubwa wa visima vya maji vifupi na virefu ili kupunguza kero ya maji hasa katika vijiji vyenye mkusanyiko mkubwa wa watu. Vijiji hivyo ni Azimio, Seveni, Mgalia, Mwaji, Jiungeni, Mrusha, Lukala, Mahande, Mitwana, Kazamoyo, Imani, Nasya, Tuwemecho, Namesaku, Mdingula, Chemchemi, Namasakata, Ligoma, Makate, Chiwana, Mkadu, Mbesa, Chikomo, Chinunje, Umoja, Misyaje, Mchuba, Meladi, Wenji, Njenga, Likwaso, Mcheteko na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji wa Kijiji cha Mtina ni wa muda mrefu sana, tangu mwaka 2012 katika Miradi ya World Bank. Halmashauri imesitisha mkataba na mkandarasi tangu Desemba, 2017 na mradi umesimama. Tunaomba mradi ule ukamilishwe haraka iwezekanavyo ili kuondoa kero za wananchi wa eneo la Mtina.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa maji katika Kijiji cha Mbesa bado unasuasua. Tunaomba Serikali kuweka mkazo mradi huo ukamilike kwa wakati ili kuondoa kero za maji katika Kijiji cha Mbesa ambacho kina idadi kubwa ya wakazi kutokana na uwepo wa Hospitali ya Mbesa ya Mission. Mradi wa Umwagiliaji wa Misyaje ni wa muda mrefu sana. Umetumia zaidi ya shilingi milioni 800, lakini mpaka leo mradi huo haufanyi kazi kabisa. Hivyo fedha zinakwenda bure na upo kwenye kiwango cha chini sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa umwagiliaji Madaba nao umegharimu zaidi ya shilingi bilioni moja, lakini haupo katika kiwango kizuri kwa maana na hufanyi kazi ipasavyo. Hivyo unahitaji marekebisho makubwa sana ili uweze kufanya kazi vizuri. Vilevile kuna miradi mipya miwili katika vijiji vya Wenje na Mkapunda. Tunaomba miradi hiyo ifanyiwe kazi ili kuongeza uzalishaji wa mpunga ambao unaonekana kuwa na tija kwa wakulima wa Tunduru Kusini.

Mhesjhimiwa Naibu Spika, miradi ya maji Lukumbule na Nalasi wananchi wanashindwa kuiendesha kwa kwa kuwa na gharama kubwa sana kutokana na kutumia dizeli. Tunaomba miradi hii ya wananchi itumie umeme wa solar ili kupunguza gharama za dizeli ambapo zaidi ya lita 60 kwa siku zinatumika kuendesha mitambo ya kusukuma maji. Kuna miradi mitatu iliandika andiko la miradi, tulileta Ofisi ya Wizara ya Maji ili kututafutia pesa kwa ajili ya kuchimba visima na kusambaza maji katika vijiji vya Namasakata, Tuwemacho na Malumba/Molandi pamoja na Kijiji cha Mchoteka.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba miradi hiyo ipewe umuhimu wa kuifanyia kazi ili wananchi wa maeneo hayo wapate maji kuondoa adha inayowakumba.