Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake yote kwa kazi kubwa wanayoifanya kwa kuhakikisha wananchi wanapata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Lushoto hasa katika Kata za Kwai – Makanya, Kilole, Malibwi Kwekanga, Mbwei, Ngulwi, Ubiri Gare pamoja na Kwemashai. Maeneo yote haya yana shida kubwa mno ya maji. Hivyo basi, naomba Serikali yangu iangalie kwa jicho la huruma kabisa kutupatia fedha kwa ajili ya kunusuru wananchi hawa hasa akina ama.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali yangu tukufu kwa kunipatia pesa shilingi milioni 770 kwa ajili ya maji katika Mamlaka ya Maji Lushoto, lakini pesa hizi hazitoshi kwani zinajenga banio moja na kisima kimoja chenye ujazo wa lita 600,000. Kwa hiyo, naiomba Serikali iongeze pesa ili kazi hii inayoendelea kufanyika iende sambamba na usambazaji wa maji yaani tupatiwe fedha kwa ajili ya kununua bomba na kutoa mabomba ya zamani ambayo ni ya tangu mkoloni.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, kuna Kata mbili za Ngulwi na Ubiri; kata hizi huwezi kuzitenganisha na Mradi wa Mamlaka ya Maji Lushoto, kwani kata hizi zipo chini ya mji wa Mamlaka ya Mji Lushoto na mradi huo unaelekea maeneo hayo ya kata hizo mbili. Hivyo basi, naiomba Serikali ituongezee fedha ili mradi huu uunganishwe na kata hizo mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wangu hasa waishio katika Mamlaka ya Mji hubambikiwa bili. Hivyo basi, naiomba Serikali ilichukue suala hili na kutoa hatua kali za kisheria maana watu hawa wa Idara ya Maji wananyanyasa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Ngulu umefanyiwa hujuma na Mkurugenzi wa Halmashauri baada ya kumsimamisha mkandarasi wa kwanza bila kufuata utaratibu na akampa mkandarasi mwingine bila kutumia utaratibu kwa minajili ya kupewa asilimia 10. Hii imepelekea mpaka sasa hivi mradi ule kusimama na wananchi wamekosa huduma mpaka leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri ni shahidi, alikuja na kutoa maelekezo na baadhi ya Madiwani na Mwenyekiti wa Kijiji walimpongeza Mkurugenzi yule lakini akawaambia msimpongeze bado ni muda mfupi aliokaa. Hili limekuwa kweli. Hivyo basi, naomba Mheshimiwa Waziri atume timu yake ikatoe mwelekeo au yeye mwenyewe akamalize suala hili ili wananchi waweze kupata huduma hii muhimu ambayo wanaisubiri kwa hamu kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi naunga mkono kuanzishwa kwa Mamlaka ya Maji Vijijini kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi wa Mtumbi, huu mradi ni wa muda mrefu lakini mpaka sasa mradi ule bado hauna hata dalili ya kuanza na sasa ni takribani miaka sita imeisha. Naiomba Serikali ipeleke pesa ili mradi huu uweze kuanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yangu tukufu itujengee mabwawa hasa katika maeneo ya Mazashai, Mbwei, Makanya Kwai, Kwemakame, Boheloi, Mshangai, Ubiri na Mazumba kwani katika Wilaya ya Lushoto kuna mito mingi sana inayopeleka maji sehemu za mabondeni na maji haya kuharibika tu wakati wananchi wana shida kubwa ya maji. Hivyo basi, kwa kujenga mabwawa, itasaidia wananchi kupata maji ya kunywa pamoja na kulima kilimo cha umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Lushoto wana hali mbaya sana hasa wananchi waishio Kwemakame, yaani mpaka sasa wananunua ndoo ya maji shilingi 1,000. Nakuomba eneo hili uliangalie kwa jicho la huruma kwani imekuwa ni kilio changu kila tunapokutana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.