Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ABDALLAH HAJI ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa mambo yote. Aidha, nakupongeza wewe binafsi kwa uongozi wako mzuri Bungeni na unaotumia busara.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni maisha ya kila kilicho hai duniani. Kutokana na umuhimu wa maji, takribani Wabunge wote wametoa malalamiko yao kuhusu matatizo ya maji katika majimbo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kushangaza ni kwamba miradi mingi ya maji inalalamikiwa kwamba wakandarasi hawafanyi vizuri kwenye miradi hii ambayo huwa inaigharimu sana Serikali. Miradi mingi kwa mujibu wa maelezo ya Wabunge hukabidhiwa kwa wananchi kwamba imekamilika lakini kwa masikitiko ni kwamba miradi hiyo haitoi maji. Hii ni hasara kubwa kwa Taifa hakuna Mbunge yeyote ambaye alipopata nafasi ya kuchangia asitoe malalamiko ya shida ya maji kwa wapiga kura wake hususani majimbo ya vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hapa ndipo Serikali inapaswa kujitathmini yenyewe kwamba fedha inatoka kwa utekelezaji wa miradi ya maji, lakini upatikanaji wa maji hayo ni wa kusuasua na thamani ya fedha itumikayo ya walipa kodi na zile za wahisani ukweli haionekani. Hivyo wananchi wanolipa kodi wana haki ya kuilalamikia Serikali yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa maelezo ya Wabunge walio wengi kwamba sababu kubwa ya ukosefu wa maji ni wakandarasi wasio waaminifu au wasio na weledi wa masuala ya upatikanaji wa maji. Naishauri Serikali kwamba suala la maji ni mtambuka na ndio kipaumbele cha maisha ya kila kiumbe kilicho hai, sasa ikiwa Serikali imekusudia kumtua mama ndoo kichwani yenyewe ijiongeze na iweze kusimamia utekelezaji wa wakandarasi na ihakikishe unatoa tija ili kuondokana na shida hii. Aidha, kufanya upembuzi yakinifu kwa wakandarasi wenye uwezo wa weledi wa miradi ya maji ili kuepuka kupewa dhamana kwa wasio na uwezo. Hili likiwezekana angalau kwa asilimia 50 litaepusha malalamiko ya wananchi na kutoa thamani ya fedha ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo hii sio mara ya kwanza kulizungumzia ni upotevu wa maji ya mvua ambayo ni neema kubwa kutoka kwa Mungu. Kwa eneo hili bado naishauri Serikali kutenga bajeti maalum ya kutengeneza mabwawa maalum ya kuvuna maji ya mvua ambayo yakifanyika hayo tunaweza kupunguza kwa kiasi kikubwa shida ya maji. Mabwawa yataweza kusaidia kilimo cha umwagiliaji, kunyweshea mifugo, kufugia samaki na matumizi ya nyumbani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tumekuwa wamwagaji wakubwa wa maji baharini kwa maana kwamba maji ya mvua yote kwa muda mfupi yanakimbilia baharini na kuiacha nchi ikiwa kame. Jambo la uvunaji na uhifadhi wa maji ya mvua pamoja na kwamba una hasara yake lakini una faida kubwa. Mfano hapa Dodoma mvua yote iliyonyesha lakini ni muda mfupi tu sasa maji yote hayaonekani. Ahsante.