Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuipongeza Serikali na Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa juhudi kubwa ya kuwaletea wananchi miradi ya maji katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri bado tunalo jukumu kubwa mbele yetu katika kufikia malengo ya mwaka 2020 ya kutoa huduma ya maji vijijini kwa asilimia 85. Katika Jimbo langu la Singida Kaskazini tunalo tatizo kubwa la maji katika vijiji vyetu na kuwafanya wananchi kuhangaika kutafuta huduma ya maji. Hata katika baadhi ya maeneo yaliyo na vyanzo vya maji, maji hayo siyo safi na salama kwa matumizi ya binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishukuru sana Serikali kwa kuliweka Jimbo la Singida Kaskazini katika mradi wa matumizi ya teknolojia ya nishati jadidifu ambao tayari umeshaanza katika vijiji vya Ghalunyangu na Mughunga. Pia kwa kutengea fedha shilingi 1,644,481,000 kwa ajili ya miradi ya maji vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, vipo vijiji na vitongoji katika Kata ya Mughunga ambavyo ni kijiji cha Nduamughanga na vitongoji vya Mukulu ambavyo vipo umbali wa kilometa 25 kutoka makao makuu ya kijiji. Maeneo haya hayana huduma ya maji safi na salama. Pia vipo vijiji vya Lamba, Sughana, Misuna, Gairo na vingine vingi katika Jimbo la Singida Kaskazini.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali kuongeza fedha za miradi ya maji ili kupunguza tatizo hili na kufikia malengo tuliyonadi kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kilimo cha umwagiliaji, ipo miradi mingi ambayo inafaa kwa umwagiliaji ambayo tayari Wizara imeainisha na niombe kupatikana fedha za kutekeleza miradi hii sasa ili iweze kuongeza tija. Miradi ipo maeneo ya Ikhanuda, Itanika, Ngimu, Songambele, Songa, Ndang’onyo na Sagara. Lipo pia Bwawa la Msange ambalo utafiti ambao umeshafanyika na miradi bado haijaanza. Nimuombe Mheshimiwa Waziri aweze kutembelea jimbo langu na kujionea miradi ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 144 kwenye ukarabati wa mabwawa, inaonesha kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Singida inatengewa fedha, lakini bwawa hili na vijiji vilivyoainishwa vipo katika Wilaya ya Ikungi, Jimbo la Singida Mashariki. Nimuombe Mheshimiwa Waziri wafanye marekebisho ili yaingizwe mabwawa na vijiji vya Jimbo la Singida Kaskazini.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja.