Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Eng. Edwin Amandus Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Namtumbo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ENG. EDWIN A. NGONYANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii, ingawa nikiangalia saa pale inanipa shida kidogo, lakini nitajitahidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza moja kwa moja na suala la Jimbo langu la Namtumbo. Miradi iliyokuwa inaitwa ya World Bank ambayo ilianza mwaka 2005/2006 na kwa maana hiyo ni wakati ambapo Serikali ya Awamu ya Nne ilipokuwa inaingia madarakani, kwangu kwa kweli imepata msukumo mkubwa sana na Mheshimiwa Engineer Kamwelwe kama Waziri wa Wizara hii ya Maji na Umwagiliaji. Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri, umelipa certificates mbili za Mradi wa Mkongo - Gulioni na Nahimba na nimeambiwa kwamba kutokana na ile certificate uliyoilipa katika wiki zijazo maji yatakuwa yametolewa kutoka kwenye chanzo na kuingizwa kwenye matenki na baada ya hapo, hatua ya pili ya kuyatoa kwenye matenki na kusambaza kwa wananchi itafuatia, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nikuombe mradi mwingine katika hii miradi ya World Bank wa Likuyu - Sekamaganga ambayo advanced payment au certificate ya awali inahitaji nayo ilipwe ili na huo mradi nao upate msukumo mkubwa kama ambavyo umeipa msukumo mkubwa huu Mradi wa Mkongo - Gulioni na Nahimba. Naomba na huu Mradi wa Likuyu - Sekamaganga nao upate msukumo mkubwa kama huu mwingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile Mradi wa Luhimbalilo na Naikesi ni kati ya miradi hiyohiyo ya World Bank. Nikuombe nayo uipe msukumo mkubwa, kulikuwa na tatizo la ubadilishaji wa chanjo kwa sababu chanjo cha mwanzo ilionekana maji sasa yalikuwa hayatoshi kutokana na miaka hii kumi yote iliyopita na sasa chanzo kipya kimepatikana, kina maji mengi sana. Nikuombe na huo mradi tupate fursa ya kuutangaza ili nao utekelezwe. Pamoja na kwamba ulitakiwa utekelezwe miaka kumi iliyopita lakini kwa namna wewe Mhandisi ninavyokuona utanisaidia na huo mradi uanze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mradi mwingine mkubwa unao-cover vijiji karibu vitano, unajulikana kama Mradi wa Hanga – Mawa – Msindo. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, kwa kasi kubwa uliyoianza ya kutusaidia miradi hiyo miwili ya mwanzo na huu nao uupe msukumo mkubwa ili hatimaye Wananamtumbo, ambao zaidi ya asilimia 95 ni watu wa vijijini waweze nao kunufaika na sera au na kaulimbiu ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya kuwafikia wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuhakikishie katika miradi hii ambayo umeanza kuipa msukumo, hakika unatekeleza kauli mbiu hii ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano ya kuwafikia wanyonge, watu wa chini na kwa kweli kwa upande wa Wilaya nzima ya Namtumbo tunaongelea zaidi ya asilimia 95. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna certificate ya pili kwa Mradi wa Kumbara – Litola ambao naamini Mheshimiwa Rais atakapofika kutembelea Wilaya ya Namtumbo pengine tutapata fursa ya ama kuwekea jiwe la msingi au pengine ukiwahisha kulipa fedha hizo atafika tayari maji nayo yatakuwa yametoka kwenye chanzo na kufika kwenye matenki kwa sababu ujenzi wa matenki tayari umeshakamilika. Nikuombe sana hii certificate ya pili ya kazi nayo ilipwe ili miradi hii ipate msukumo, imechelewa kwa muda wa miaka kumi lakini tunataka kuitekeleza katika miaka miwili, mitatu ya Serikali ya Awamu hii ya Tano. Nikuombe kwenye hilo unisaidie sana iweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna miradi hii iliyokuwa imetwa ya quick win, ni kwa ajili ya vijiji vya Namabengo na Mchomoro. Tuliiweka katika Programu ya Miradi ya Quick Win, ilitengewa shilingi milioni 300 kwa mwaka huu unaokaribia kuisha, nadhani unafahamu kwamba tumeomba toka mwezi wa saba na baadae kukawa na mawasiliano ya kubadilisha makadirio na namna ya ku-design tukabadilisha, mwezi wa tisa tukawaletea. Tunaomba tupate kibali cha kutangaza kwa sababu huo ndiyo utaratibu, pamoja na kwamba fedha zimetengwa hizo milioni shilingi 300 katika hiyo miradi miwili na lengo lilikuwa ni quick win lakini mpaka sasa hatujapata kibali cha kutangaza. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, hebu ongeza msukumo kwa watendaji wako, miradi hii miwili ya quick win ipate ruhusa ya kutangazwa ili hatimaye tuitangaze na tuwahi kabla ya tarehe 30 Juni tuweze kutumia hizo shilingi milioni 300 tulizotengewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu fedha hizi za shilingi milioni 300 kwa miradi hii miwili ya quick win kama hatutaweza kutangaza ina maana tutashindwa kuzitumia. Sasa mmetutengea shilingi milioni 80 kwa kila mradi, toka shilingi milioni 300 tunashuka kwenye shilingi milioni 80, tusipoitumia ile shilingi milioni 300 hiyo shilingi milioni 80 haitafanya kazi kubwa na kwa kweli maana halisi ile ya quick win haitakamilika. Nikuombe sana utusaidie, tupe ruhusa ya kutangaza ili tuweze kutangaza na tuweze kuzitumia hizi shilingi milioni 300 ili hizi shilingi milioni 80 zinazofuata kwa mwaka 2018/2019 tuweze sasa kukamilisha kabisa na wananchi wale wa Mchomoro pamoja na Namabengo waweze kupata maji kama ambavyo Serikali ya Awamu ya Tano ilikusudia kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana liangalie hilo. Kibali cha kutangaza ni barua tu na kwa maana ya kuutathmini huo mradi mlishafanya hiyo kazi kuanzia mwezi Julai mwaka jana. Nikuombe sana, hebu tupe hicho kibali ili hii miradi iweze kuanza kutekelezwa na maana ya quick win ikamilike.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana unisaidie katika maeneo mengine sugu sana ya Mgombasi, Matepwende ya Msisima, Matempwende ya Ligera au Matepwende ya Milonji, Lometa pamoja na Mtakanini, ni vijiji ambavyo vina matatizo makubwa sana ya maji. Labda tu nikwambie pale Mtakanini hilo ombi lilitolewa na Marehemu Mzee Kawawa na likakubalika na wakati huo Rais wa Awamu ya Tatu, Mheshimiwa Mkapa lakini mpaka sasa hatujapaangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe sana na hapo napo tupaweke vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.