Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Kunti Yusuph Majala

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuchangia Wizara hii ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niseme kwamba hakuna Mbunge hata mmoja ambaye anaamini kwamba maji siyo muhimu. Nisikitike tu watu wanaopinga suala zima la kuundwa kwa tume ya kwenda kuchunguza hali halisi ya miradi ya maji kwenye maeneo yetu. Leo kama Wabunge tungekosa maji hakuna Mbunge hata mmoja angekuja humu ndani, hayupo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la uundwaji wa tume, Wabunge tunahitaji tume iundwe kwa sababu tumekuwa tukizungumza suala zima la ufisadi kwenye miradi ya maji, Serikali kwa maana ya Wizara mmekuwa hamtuelewi. Mwaka jana nilizungumza suala la Mradi wa Ntomoko, mwaka juzi hali kadhalika, mradi huu sikuwahi kupata majibu, uliendelea kupigwa danadana kwenye vitabu vya Waziri, safari hii hata kwenye kitabu cha Waziri Mradi wa Ntomoko haupo na matokeo ni mpaka Rais ndiyo amekwenda kutoa kauli ya kwamba waliotumia fedha za Mradi wa Maji Ntomoko wachukuliwe hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tuna kosa gani Wabunge tukisema Mawaziri hawako tayari kwenda kufanya kazi na kusimamia miradi hii ya maji kwa ukamilifu wake? Kwa nini tukisema kwamba Mawaziri mmeshindwa, amebaki mtu mmoja peke yake ndiye anayetoa kauli za miradi na shughuli mbalimbali za Serikali kutendeka.

Suala la Ntomoko tumelisema hapa miaka nenda, miaka rudi, hamkuwahi kusema chochote na hamjawahi kuchukua hata hatua yoyote mpaka Rais amekwenda kuchukua hatua. Sasa ninyi Mawaziri kazi yenu ni nini, si bora mtoke wote abaki Rais Magufuli peke yake afanye kila kitu, ninyi mnafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la upatikanaji wa maji nchini ni changamoto kubwa sana. Vijijini kuna shida ya maji wote humu ndani sisi ni mashahidi. Taabu hii wanaoipata ni wanawake wanaoishi vijijini. Mwanamke wa kijijini kulala kwake analala saa mbili, anaamka saa saba za usiku, saa tisa za usiku anatembea zaidi ya kilometa 20, 40 anakwenda kutafuta maji, anarudi mwanamke huyu amechoka bado anatakiwa kwenda kuihudumia familia yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini watoto wetu wa kike wanapata taabu kubwa sana. Leo watoto wa kike wanapata mimba za utotoni kwa sababu ya kutembea umbali mrefu kwa ajili ya kwenda kutafuta maji na Serikali mnawakatalia watoto wetu wa kike kurudi shule wanapopata mimba za utotoni eti kwa sababu amepata mimba, akienda shuleni atakuwa ni mzazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Chama cha Mapinduzi haina dhamira ya dhati ya kwenda kumtua mwanamke na mtoto wa kike ndoo kichwani. Serikali ya Chama cha Mapinduzi inaendelea kumdidimiza Mtanzania wa chini aendelee kudidimia kwenye shughuli za kiuchumi, elimu na hatimaye sisi Wabunge tulio wengi wa Chama cha Mapinduzi tunaopata maji safi na salama, elimu bora na familia zetu zinasoma vizuri ili watu hawa wanyonge wa huko chini watoto wao wasisome, wasipate maji safi na salama, wafe kwa maradhi, ili familia zenu viongozi wa Chama cha Mapinduzi waje waendelee kuliongoza Taifa hili. Dhambi hii Mwenyezi Mungu anawaona na hakuna malipo yanayokwenda kulipwa akhera, tutalipana hapahapa duniani na kila mmoja ataonja jasho lake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee suala zima la madeni ya taasisi za maji. Mwaka jana nilisema taasisi za Serikali zinadaiwa na Mamlaka za Maji zikiwemo Ofisi ya Rais, Ofisi ya Makamu wa Rais, JKT, Polisi na Magereza. Taasisi zote hizi za Serikali zinadaiwa na Mamlaka za Maji. Kibaya zaidi unakuta taasisi hizi zinadaiwa hazikatiwi maji, Mtanzania/ mwananchi wa kawaida anadaiwa mwezi mmoja tu hajalipa anakwenda kukatiwa maji, huu ni uonevu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mbaya zaidi Jeshi la Polisi kwa hapa Dodoma ilifanyika operesheni, walivyokwenda kukatiwa maji Jeshi la Polisi likaamua kukamata magari yote ya DUWASA pamoja na pikipiki, vifaa vyote vikakamatwa vikaenda kujazwa pale kwenye kituo cha polisi.