Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi nianze kwa kumpongeza kwanza Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na timu yake ya wataalam ikiongozwa na Katibu Mkuu, wamefanya kazi nzuri sana. Ukiangalia katika hii ripoti utaona ni kiasi gani wamefanya mageuzi katika hii Wizara. Mwaka uliopita utendaji ulikuwa ni asilimia 25 lakini kwa mwaka huu tulionao wa 2017/2018 Wizara hii imetekeleza kwa asilimia zaidi ya 56. Hiyo ni mara mbili ya ule utekelezaji wa mwaka jana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ninapenda kumpongeza Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa ziara walizozifanya kwenye Jimbo langu, zimeleta mageuzi makubwa. Naibu Waziri alikuja, alishuhudia mwenyewe miradi ya mabilioni ya pesa ambayo ripoti zake zinaonesha kuwa imetekelezwa na amekwenda site kwenye tenki akaambiwa hilo tenki lina maji, akapanda kwenye tenki kuangalia badala ya maji akakutana na mazalia ya popo. Kwa hiyo, inasaidia sana hizi ziara za Mawaziri wanapokwenda wenyewe site na kujionea ni nini kinachofanyika huko. Utekelezaji kwenye miradi mingi hasa ya vijijini ni kwa kiasi kidogo sana. Ni hela nyingi sana nchi hii zimeliwa, nakubaliana na wenzangu ambao wamependekeza kuundwe Tume ichunguze miradi ya maji ili tujue ni kiasi gani cha pesa zilizoliwa kwa vile tutaongeza tozo tutamlalamikia Waziri wa Fedha lakini kusipokuwa na usimamizi, hali huko vijijini ni mbaya sana, pesa zimeliwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni shahidi wa kilichotokea kwa Mheshimiwa Waziri kuchukua miradi ya Mbeya Vijijini, tulikuwa na asilimia mbili tu kwa mwaka uliopita lakini alipokuja Waziri akachukua miradi yote ya Mbeya Vijijini, leo tuko na asilimia zaidi ya 60 za utekelezaji. Miradi mingi inatekelezwa vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kuna mradi wa Iwindi, Izumbe, Mwashiwawala uko katika utekelezaji mzuri sana. Mradi wa Mbalizi tulikuwa tunalalamikia Mbalizi hakuna maji, lakini Waziri amechukua initiative zake za kuunganisha Mamlaka ya Maji Mbalizi na Mamlaka ya Maji Jiji. Miradi yote ya vijiji kumi ambayo ilikuwa imekwama kwa miaka zaidi ya saba leo hii iko kwenye utekelezaji mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata wewe mwenyewe ni shahidi, ninaomba kukushukuru kwa juhudi zako na jitihada zako umeweza kutusaidia mradi wa Irota ambao leo hii tuna imani tutaletewa zaidi ya shilingi milioni 250 kwa ajili ya kile kijiji ambacho kilikuwa hakina maji kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naisoma vizuri sana hii ripoti, tunaomba maji lakini ukiangalia ukurasa wa tano, hayo maji tunayoyaombea pesa hayapo! Mwaka 1962 uwezo wa maji tuliokuwa nao ilikuwa ni mita za ujazo 7,800, mwaka jana zimepungua mpaka mita za ujazo 1,800 kwa mtu kwa mwaka. Mwaka 2025 inaonesha tutakuwa na mita za ujazo 1,500; maana yake nchi hii itakuwa imeingia kwenye nchi ambazo hazina maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaongea sana hapa, tunataka bajeti za maji, maji yako wapi? Naliomba Bunge lako liunganishe nguvu za Wizara hizi mbili, Wizara ya Mazingira na Wizara ya Maji zifanye kazi kwa karibu. Wenzetu wameshachukua kwa makusudi kabisa kuvuna maji. Kuvuna maji ya mvua yamewasaidia vilevile hayo maji yanayozalishwa imekuwa ni zao ambalo linaloziletea hizo nchi pesa za kigeni kwa vile maji ukiangalia nchi zinayoizunguka Afrika Kusini wanayakusanya maji ya mvua na yale maji yanapelekwa Afrika Kusini na inazipatia pesa za kigeni hizo nchi, pesa nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoa mfano wa kule Jimboni kwangu, tuna mvua nyingi sana lakini mito mingi sasa hivi inakauka, mto Nzovwe unakauka, Mto Songwe unakauka na ukiangalia kuna mimomonyoko ya udongo, mvua zikishanyesha udongo wote unakwenda Ziwa Rukwa, na ziwa karibu linakauka. Nafikiri Wizara iangalie bajeti kubwa, ningeomba kwanza uanzie kwenye Jimbo langu kwenye Kata ya Mjele, jenga mabwawa ya kutosha ili tuweze kuvuna maji ya kutosha tuongeze huu ujazo wa maji badala ya kufanya projections za maji kukauka, tufanye projections za maji kuongezeka, hiyo trend ibadilike. Tusiongelee mita za ujazo 1,500, tuongelee ni namna gani turudishe mita za ujazo 7,800 na zaidi. Hilo ni jambo muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika bajeti ya Waziri wengi sana wamejadili kuhusu kuanzisha Mamlaka ya Maji Vijijini. Kama nilivyosema, Halmashauri yangu iwe ni pilot, imefanya kazi vizuri mno. Nakuomba Waziri, hili suala litakapoanza tumia modal uliyotumia Mbeya Vijijini iende kila Halmashauri, italeta mageuzi mno na hatutahitaji pesa nyingi kwa ajili ya maji. Tutahitaji bajeti ndogo, pesa ndogo sana kwa ajili ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naungana na wenzangu kuhusu kuongeza tozo kutoka shilingi 50 kwenda 100. Ni jambo muhimu, litatuletea neema sana, ukiangalia bajeti ya mwaka huu kwa kiasi kikubwa imetegemea tozo ya mafuta ya dizeli pamoja na petroli, bila hivyo tusingefikia hiyo asilimia 56. Kwa hiyo, tunaomba tuangalize zaidi namna ya kujitegemea badala ya kuangalia ni namna gani tutegemee misaada kutoka nje ambayo kutokana na hali ilivyo sasa siyo ajabu hatutaipata hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ningeomba Wizara ya Fedha ingeangalia. Kwa ile mitambo ya kuchimba mabwawa ya maji na ile mitambo na vifaa vyote vya maji vingeondolewa kodi ili viwezeshe kupunguza gharama za uchimbaji wa maji na miradi ya maji. (Makofi)

Baada ya kusema hayo, naomba na mimi niunge mkono hoja. Nashukuru sana.