Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi nichangie Wizara hii. Kwanza nimpongeze Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na miradi ya maji; kama walivyozungumza Wabunge wenzangu, kwa nini miradi haikamiliki Mheshimiwa Waziri? Kwangu kuna visima vinne vimechimbwa katika vijiji vya Mima, Iyoma, Bumila pamoja na Mzase. Tangu mwaka juzi, mwaka 2016 umeleta wakandarasi, sawa, sasa wako pale karibu mwaka mzima hawafanyi kazi yoyote, hakuna fedha na inatakiwa upeleke shilingi milioni 426. Sasa Mheshimiwa Waziri hivi tutakuwa tunawachimbia watu visima halafu inakuwa kama white elephant, watu wanaangalia tu kwamba tuna kisima hapa, miaka mitatu, miaka minne, kisima hakikamiliki, kwa nini sisi Wabunge tusilalamike?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba sana Mheshimiwa Waziri Miradi ya World Bank imechukua miaka kumi, mingine imekamilika juzi, mingine haijakamilika. Kwa mfano, Kijiji cha Kimagai ndiyo mradi umekamilika juzi, miaka kumi Miradi ya Benki ya Dunia. Sasa tatizo ni fedha au tatizo la wakandarasi? Naona tatizo ni wajkandarasi hamuwalipi. Bunge sisi kama Bunge tunatenga fedha, tunakaa hapa miezi mitatu, tukishapitisha bajeti haiendi kwenye miradi, inakuja nusu tu, hizi fedha zinakwenda wapi huko Hazina? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Mheshimiwa Musukuma, nadhani ipo haja ya kuunda Tume ichunguze Wizara hii fedha zinakwenda wapi? Miradi haikamiliki, miaka kumi, miaka nane? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shida kubwa katika nchi hii ni maji, ni shida kubwa sana, kila kijiji ukienda tatizo ni maji. Sasa ahadi tulishaahidi, Ilani ya Uchaguzi kwamba mkinichagua nitahakikisha mnapata maji, sasa Mheshimiwa Waziri unatutakia mema kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana peleka Jimbo la Mpwapwa shilingi milioni 426 ili wakandarasi waweze kukamilisha miradi hii ya maji. Mpwapwa Mjini tunatumia maji ya chumvi, ni kweli wanasema siyo kila aina ya maji ya chumvi yana madhara tumboni kwa sababu yale maji yanapimwa, unachukua sample inapelekwa kwa Mkemia Mkuu wanaangalia mambo mawili, wanafanya chemical analysis pamoja na bacteriological examination. Kama yana madini yanayoweza kudhuru afya ya binadamu ama kama kuna bacteria, maana maji mengine yanaleta homa ya matumbo lakini wamepima yanafaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mheshimiwa Waziri ukienda Wilaya ya Mpwapwa, hasa Mpwapwa Mjini, ujaribu kuonja yale maji ndiyo binadamu wanakunywa. Kwa hiyo, nakuomba na nilikwishaiomba Serikali ifanye utafiti kuna sehemu ambazo ukichimba kisima cha maji kuna maji baridi, tuwaonee huruma wananchi wa Mji wa Mpwapwa jamani wanateseka. Kweli maji yapo lakini ni ya chumvi mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.