Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue fursa hii ya awali kabisa kukushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ambayo naitafuta kwa udi na uvumba ahsante sana. Vilevile nimshukuru Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais pamoja na Waziri Mkuu na Waziri mwenyewe kwa dhamira yao ya dhati ya kumtua mama ndoo kichwani na kama itatokea hivyo kwa kweli Mungu awabariki sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mnyimi wa fadhili kama sitampongeza na kumshukuru Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Watendaji wote chini ya Wizara hii kwa sababu kwa kweli kama siyo ufinyu wa fedha utaona kwamba wanajihadi kubwa sana. Kwa hivyo, naomba muendelee kukazana ili nchi ipate maji kwa malengo ambayo mmeyaweka na kwamba watu wasiende zaidi ya mita 400 kutafuta maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji ni uhai, maji ni usafi wa mazingira, maji ni afya na kwa ujumla maji ni maendeleo lakini ilivyo maji ni siasa vilevile. Kwa hivyo, ninaomba tutekeleze haya maji kwa kuondoa kiu ya maji, vilevile kusambaza miradi hii nchi nzima ili kusudi kila mwananchi wa Tanzania aweze kunufaika na miradi mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imepanga mambo mengi na imetekeleza mengi, Serikali ilipitisha sera hii nzuri kwamba maji yasiwe mbali zaidi ya mita 400 kutoka kaya mbalimbali na Serikali imetaka by 2020 wananchi asilimia 85 wamefikiwa na maji, lakini hadi sasa utaona na kama Waziri alivyoeleza ni asilimia 58.7 ambao wamepata maji na hasa vijijini. Ninaomba tufanye yafuatayo ili hayo mambo yatekelezeke kwa kasi kubwa zaidi. Niko kwenye Kamati hii na ni lazima ni-declare interest, nimeona changamoto nyingi ambazo zipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kwamba Serikali kama imetenga shilingi fulani itoe zote basi kwa sababu bajeti ndiyo instrument kuu ya kutekeleza mambo ya maendeleo bila bajeti hatuwezi kufika mbali. Pili kwa sababu bajeti inaonekana kwamba haifikii malengo basi tuendelee na kuhakikisha kwamba katika bajeti hii shilingi 50 zimeongezeka kwenye mfuko wa maji kutokana na mafuta, dizeli na petroli na mafuta ya taa. Kwa sababu mimi ninavyoona ndivyo namna pekee na kila moja ni shahidi kwamba miradi ya mwaka huu au mambo yaliyopangwa mwaka huu yametekelezwa kwa asilimia 66 na mfuko wa maji na bajeti iliyopangwa imetekeleza kwa asilimia 22 tu. Kwa hivyo, Wabunge wanapokazania hii tozo ya shilingi ya 50 ni kuitaka Serikali iweze kufikia azma yake na wanachi waweze kupata maji kama tunavyotegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna vifaa au ya kujenga miundombinu ya maji mingi inatozwa kodi, maana yake ni kwamba mnapunguza bajeti ya kutumia vifaa kwenye miundombinu, naomba tuangalie na hilo. Jambo la nne ni uundaji wa wakala wa maji, hakuna labour force ya kutosha au wataalam wa kutosha kwenye Halmashauri zetu ambao watatekeleza miradi ya maji na ndiyo maana contractors wengi kwanza hawana uwezo kwa hivyo tukiwa na wakala miradi mingi itatekelezeka upesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nijielekeze kwenye Wilaya yangu ya Hanang ambako Mbunge ni mimi. Niliomba kwa miaka minane lambo ya Gidahababieg na Waziri anaijua, ninaomba wakati akitujibu aweze kuniridhisha na awaridhishe watu wa Hanang kwamba miaka hii minne hatudanganywi bali lambo litapatikana. Ninajua anataka sana kufanya hivyo lakini aendelee kutupa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni maji katika Mji wetu Mkuu wa Katesh, ninaishukuru sana Serikali imeipa kazi hii Mamlaka ya Maji Babati lakini kwa muda mrefu Katesh haina maji, shilingi milioni 100 haitatosha, naomba Waziri uangalie na hata kwenye mfuko huo mdogo ambao tunao ili Katesh ipate maji. Huwezi kuwa na Makao Makuu ya Wilaya ambayo hayana maji, kwa kweli siyo jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna miradi mingi kwa mfano, tulitengewa shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya mradi wa Endasaki, Endagau, Endasiwold, lakini mpaka sasa tumepokea shilingi milioni 700 naomba hizi shilingi milioni 600 zitoke kusudi maeneo yaliyobaki kama Endasiwold Endagau waweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna mradi mwingine wa Malama, Maskararoda, Masakta na Lambo ambao tulitengewa shilingi bilioni 1.2 hatukupata hata senti moja na kule kuna matatizo makubwa sana ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Hanang ipo kwenye Rift Valley ukichimba kisima unaenda zaidi ya mita mia moja huoni maji, kwa hiyo gharama ni kubwa. Ninaomba sana watu wetu wasibaki bila maji wakati malengo ya Serikali ni mazuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba fedha hizi za Malama, Endagau, Endasaki na Endasiwold zimepangwa kwa miaka mitatu mpaka leo maji hayajapatikana. Naishukuru sana Serikali kutokana na mradi huu Endasaki imepata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna visima zaidi ya tisa ambavyo vimeshachimbwa watu wanaona na wanataka kututoa macho kwa sababu miundombinu haipo, hakuna pump hakuna nini, watu hawachoti maji wanaangalia maji yako pale, ninaomba sana ninaomba sana miradi hii ikamilike na ninaomba Waziri kama walivyosema wengine kwa kweli tuunde Tume wakaangalie miradi ya maji nchi nzima ikiwepo Hanang yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie kwamba Endamdaiga haina maji, Gawidu haina maji, Gisambalang haina maji na vijiji vingi ambavyo havina maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwamba kwa vile Hanang haina maji ya chini ya kutosha bonde la ufa ninaombeeni mtupangie fedha za kuweza kuchimba mabwawa au malambo. Sisi tuna wafugaji, wanaotumia maji watu wengi takribani laki nne, tunao wakulima vilevile.

Jambo lingine ambalo nilitaka niongelee ni kuhusu umwagiliaji. Tuna mradi wa Endagau ambao ulipokea shilingi milioni 900, kama utatekelezwa vizuri Hanang watakuwa na manufaa makubwa kwa sababu hatuna uhakika wa mvua. Naomba sana kama Serikali ilivyoanza iendelee kuufuatilia mradi ule ili uende vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo linalosikitisha ni kwamba design zinakuwa si sawa na hasa ukienda kwenye miradi yote ya umwagiliaji ndani ya nchi utakuta kwamba zina faults au zina matatizo. Endagau ni moja ya maeneo yenye matatizo lakini naomba sana Serikali nayo iweze kuuangalia mradi huu ili Hanang nayo iweze kunufaika na miradi ya umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba, kama tunavyojua maji yalivyo na umuhimu barabara hazijengeki bila ya maji, hakuna mradi wowote utakuwepo bila ya maji, hata viwanda havitajengeka bila ya maji. Ndiyo maana Waheshimiwa Wabunge wote hapa wanataka hiyo tozo ya shilingi 50 iongezwe kusudi maji yatakapokuwa na uhakika ndani ya nchi hii, mengine yote yatawezekana na watoto watakuwa na malezi mazuri kwa sababu mama zao hawatachukua muda mwingi na hawataenda masafa marefu ya kutafuta maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na kwangu mimi kipaumbele cha kwanza ni maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri, naomba Waheshimiwa Wabunge tuipitishe ili Watanzania wapate maji.