Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji na Umwagiliaji kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja iliyopo mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwa kuwapongeza viongozi na watendaji wa Wizara hii, tukianza na Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mheshimiwa Engineer Kamwelwe kwa kazi yake nzuri anayoifanya, vilevile Naibu Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Mheshimiwa Aweso, Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Profesa Kitila Mkumbo na Naibu Katibu Mkuu, Engineer Kalobelo, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi mnazozifanya tunaziona na jinsi mnavyohangaika kurekebisha sekta ya maji na mna nia njema ya kumtua mama ndoo lakini changamoto kubwa ambayo mnakabiliwa nayo ni ukosefu wa fedha, lakini kwa fedha chache zilizopo matokeo tunayaona, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tukabiliane na tatizo hili la fedha ambazo Wizara hii muhimu na nyeti na ambayo inamgusa kila mwanafamilia asubuhi anapoamka basi niungane na wazo ambalo limetolewa na Kamati na wazo ambalo limetolewa na baadhi ya Wabunge, kwamba sasa ni muda muafaka wa kuhakikisha kwamba ile tozo ambayo mwaka jana tuliahirisha kwamba tusiongeze shilingi 50, mwaka huu tuongeze ili tupate fedha za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ni ushahidi ulio wazi, kama Kamati ilivyosema vizuri kwamba fedha ambayo ina uhakika ni fedha ya Mfuko wa Maji, kwa hiyo tuongeze tozo kwenye Mfuko wa Maji ili tupate fedha za kuwezesha kutekeleza miradi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna maendeleo bila maumivu. Kwa hiyo tuongeze shilingi 50 kwenye maji, tutaumia kwenye mafuta lakini kwenye utekelezaji wa miradi ya maji matokeo yataonekana, hivyo na mimi naunga mkono kwamba tuongeze hiyo tozo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili utajikita kwenye miradi ambayo inafadhiliwa na fedha kutoka nje. Inawezekana Wizara inatoa taarifa hizi mapema sana kwa sababu miradi inachukua muda mrefu. Katika Mkoa wetu tuna mradi wa maji wa Makonde na tulishaambiwa kwamba kuna fedha, dola milioni 87 kutoka mkopo wa India na ni zile fedha za miradi 17.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi hata viongozi wetu wa kitaifa nakumbuka mwaka juzi, Mheshimiwa Makamu wa Rais alifanya mkutano mkubwa pale Tandahimba na akawaambia wananchi wa Tandahimba kwamba tatizo la Mradi wa Makonde sasa limefika mwisho tumepata fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu wa Makonde unahusisha Halmashauri nne ambazo ni Halmashauri ya Newala, Halmashauri ya Mji Newala, Halmashauri ya Tandahimba na Halmashauri ya Mji wa Nanyamba. Kwamasikitiko makubwa Kaka yangu Mheshimiwa Mkuchika amekuwa akielezea mara kwa mara kwamba mradi huu ulijengwa wakati wa mkoloni, unahitaji ukarabati mkubwa, lakini kwa masikitiko makubwa fedha hizi hadi leo hazijapatikana na ukiangalia ule ukurasa wa 72 utakuta bado majadiliano yanaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe Serikali yangu sikivu kwamba sasa mharakishe haya majadiliano. Hiyo finanicial agreement isainiwe ili hii miradi 17 sasa ianze kutekelezwa. Kwa sababu ukiangalia kitabu cha mwaka 2016/2017 maelezo yapo, 2017/018 maelezo yapo na sasa hivi 2018/2019 maelezo ni hayohayo. Kwa hiyo, naiomba Wizara ya Fedha iharakishe hayo mazungumzo sasa..

T A A R I F A . . .

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake, lakini Serikali ipo hata kama Waziri wa Fedha hayupo, Serikali ipo kwa hiyo message itafika kwa Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Mtwara tuna mradi mwingine ambao mzungumzaji aliyetoa taarifa naye unamgusa vilevile, mradi wa kutoa maji Mto Ruvuma na kupeleka Manispaa ya Mtwara. Mradi hii vilevile ni wa mkopo kutoka Exim Bank ya China, lakini huu mwaka wa tatu sasa fedha hizo hazijapatikana na mradi haujatekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba hii miradi ambayo inachangiwa na wahisani tuweke kwenye taarifa zetu pale tunapokuwa na uhakika kwamba fedha sasa ziko tayari, la sivyo mnatupa kazi wanasiasa, tunapokwenda kule tunaulizwa na wananchi. Kwa sababu taarifa hizi sasa wananchi wanazo, kwamba kuna fedha za utekelezaji wa mradi kutoka Mto Ruvuma kupeleka Manispaa ya Mtwara. Mheshimiwa Waziri wa Maji wewe unaufahamu mradi huu vizuri, ulishatembelea kule na umezunguka maeneo yote na unaona shida ya maji ya Vijiji vya Chawi, Maembechini na maeneo mengine ya Kitae, kwa hiyo nafikiri hili litafanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utekelezaji wa miradi ya maji; kama nilivyosema, Wizara inafanya kazi vizuri sana, mmerekebisha upelekaji wa fedha, mmerekebisha hata mgao wa fedha. Ukiangalia hiki kitabu ukurasa wa 114 kila Halmashauri imeweka kiasi ambacho watapata ila changamoto iliyopo hamuweki fedha za usanifu wa miradi. Mradi hauwezi ukafikia hatua ya kutangazwa bila kusanifiwa, fedha hizo hamuweki. Hivyo, inailazimu Halmashauri ikope kwenye vyanzo vingine mradi usanifiwe, utangazwe hiyo tender document itoke ndiyo baadae mkandarasi akipatikana a-raise certificate Wizara ndiyo mnaanza kulipa. Kwa hiyo, naomba hapo Wizara hebu mrekebishe, muweke fedha kidogo kwa council ili waweze kufanya hizo kazi za awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango Mradi wa Maji wa Mitema – Lienje – Nanyamba. Kwanza nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali yangu ya Awamu ya Tano na kipekee nimshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji kwa sababu ulifika Mitema, naona umetenga shilingi milioni 600, nakushukuru na kukupongeza sana, lakini andiko la awali la mradi huu gharama ya mradi huu ni shilingi bilioni kumi na moja (11)).

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipokea hii shilingi milioni 600 kwamba tutaanza na utekelezaji wa mradi lakini Mheshimiwa Waziri hebu katika bajeti ijayo basi muweke fedha za kutosha ili mradi uweze kutekelezwa kwa wakati lakini pia kwa eneo kubwa la mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu ni mkubwa sana utahusisha takribani kata tisa, vijiji 35 na wewe eneo hili umelitembelea na ni muhimu kwa Mkoa wa Mtwara, kwa hiyo nakuomba kwenye bajeti ijayo basi tutenge fedha za kutosha ili mradi huu wa Mitema – Lienje – Nanyamba uweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie vilevile kuhusu wazo la kuanzisha Wakala wa Maji Vijijini. Hili ni suala zuri na ni suala ambalo kila mtu anaunga mkono, lakini tuwe na tahadhari wakati wa kuanzisha, kwamba tujiandae. Wakati wa Wizara ya TAMISEMI tulikuwa tukiilaumu TARURA hapa kwa sababu tumeanzisha TARURA bila kuwa na maandalizi ya kutosha kwa hiyo Wakala wa Maji Vijijini hebu tuwe na fedha ya kutosha ili watekeleze miradi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja.