Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza viongozi wa Wizara kwa kazi nzuri wanayoifanya; Mheshimiwa Profesa Joyce Ndalichako (Mb) Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia na Naibu Waziri Mheshimiwa William T. Ole Nasha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita katika maeneo manne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kuhusu ubora wa walimu na mabadiliko ya mitaala; ubora wa walimu umeelezwa na wachangiaji wengi kuwa umeshuka; maelezo haya si sahihi, wengi wanazungumzia matokeo ya shule ya private kama kigezo cha kushuka kwa elimu kwa shule za umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri changamoto zilizopo ambazo wengi wanahusisha na kushuka kwa elimu zifanyiwe kazi. Changamoto hizo ni upungufu wa miundombinu ya shule za vijijini, mafunzo kazini kwa walimu na kuboresha mazingira ya kujifunzia na kufundishia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna madai ya kubadilika mara kwa mara kwa mtaala jambo ambalo si sahihi, wakati wa majumuisho Mheshimiwa Waziri atoe ufafanuzi tangu tupate Uhuru mtaala umebadilishwa mara ngapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu wa sekondari kuhamia msingi, naipongeza Wizara kwa uamuzi huu kwani walimu wamepelekwa shule za msingi ambako kulikuwa na uhaba mkubwa wa walimu. Walimu hawa wamepata mafunzo ya kuweza kuwapa ujuzi na maarifa hata watoto na si kama wanavyodai wajumbe wengine kuwa walimu wa sekondari hawawezi kufundisha; si ya kweli. Vyuo vingi siku hizi wanawapeleka walimu tarajiwa wa diploma na degree kwenye mazoezi ya kufundisha (BTP) kutumia shule za msingi za jirani na chuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Wasimamizi Ubora wa Elimu; Idara hii inakabiliwa na changamto ya rasilimali fedha na vitendea kazi, ili kuweza kukagua shule zote na kutoa ushauri uliotarajiwa katika kuboresha elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ofisi hii haina fedha za kutosha kwa ajili ya matengenezo ya magari yao. Nashauri Wizara kutenga fedha nyingi na kuwezesha Wizara hii kutekeleza majukumu yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri nyingi zinapoanzishwa basi na Wadhibiti Ubora wa Elimu wapelekwe. Halmashauri ya Mji wa Nanyamba haina Wadhibiti Ubora wa Elimu hivyo ukaguzi wa shule inategemea wale wa Mtwara DC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vyuo vikuu vya binafsi, vyuo hivi vina changamoto nyingi ikiwemo uhaba wa wahadhiri, majengo na mazingira yasiyo rafiki ya kufundishia na kujifunzia. Serikali iongeze ufuatiliaji katika vyuo hivi ili vile visivyokuwa na sifa au vinavyoshindwa kutimiza vigezo vifungwe.