Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. ABDALLAH HAJI ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa mambo yote. Aidha, nampongeza Mheshimiwa Spika kwa uongozi wake hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Mikopo inafanya jambo zuri kwa kutenga fedha kwa ajili ya kuwawezesha wanafunzi wa nchi hii wa elimu ya juu kuweza kulipia masomo yao ya vyuo vikuu. Pamoja na hayo, kuna changamoto nyingi juu ya upatikanaji wa mikopo ya elimu ya juu. Kwanza idadi ya wanafunzi wapatao mkopo wa elimu ya juu ni kidogo sana, idadi kubwa ya wanafunzi wanaohitaji mkopo wa kuendelea na elimu ya juu wanakosa fursa hiyo. Naishauri Serikali kuongeza bajeti ya Wizara ili na Bodi ya Mikopo ipate fungu kubwa la kuweza kuwakopesha wanafunzi wengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha hayo, hao ambao wanapata mkopo kuna changamoto ya vigezo. Ili upatiwe mkopo wa elimu ya juu unahitajika kukidhi vigezo mbalimbali jambo ambalo ukiacha vigezo hivyo baadhi ya wanafunzi huwa wanapatiwa mikopo hiyo bila ya vigezo. Hivyo, naishauri Wizara husika kuzingatia vigezo na kutoa mikopo kwa wale wanaostahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ya Bodi ya Mikopo ni ukusanyaji wa mikopo hiyo. Mategemeo ni kurejeshwa kwa mikopo hii ili na wengine waweze kukopeshwa na wao wajiendeleze ila hili linategemea kupata ajira kwa wahitimu waliokopa ili Serikali iweze kuwabana na kukatwa kwenye mishahara yao kwa kiasi kilichokubaliwa na kurejeshwa Wizarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha ni pale wahitimu wengi wanapokosa ajira na kubaki mitaani bila kazi na hatua za kuwafanya walipe wakati hawana ajira ni ngumu. Hivyo, naishauri Serikali mara tu wahitimu wetu wa elimu ya juu wanapohitimu Serikali isiwe na kigugumizi cha kuwaajiri kwani ajira zao ndiyo njia ya kurejesha mikopo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu inahitaji kuwekewa miundombinu mikubwa. Wakati umefika wa kwenda na wakati na moja ya miundombinu ni lugha ya kufundishia. Kwa sasa naiomba Serikali kutilia maanani na mkazo juu ya lugha ya kiingereza. Sisemi kwamba lugha ya kiswahili iachwe lakini mkazo mkubwa uwekwe kwenye lugha ya kiingereza kwani ndiyo lugha inayotumika katika mambo yote ya kimaendeleo ya duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu inaingia katika uchumi wa viwanda, viwanda vinategemea wafanyakazi wenye taaluma na wataalam wetu tunategemea kuwapata katika vyuo vyetu vya ufundi. Nashauri Serikali kwa makusudi ilibebe suala hili na iziwezeshe shule na vyuo vya amali viweze kutoa mafundi wazuri ambao tutawatumia katika kukuza uchumi wetu wa viwanda. Walimu wa vyuo hivyo wapewe motisha na wawezeshwe ili na wao wawawezeshe wanafunzi wao kitaaluma kwa mafanikio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu motisha kwa walimu. Naiomba Serikali isiwasahau walimu kwani ndiyo mambo yote. Ikiwa walimu wanabaki na malalamiko kila kukicha basi na ufanisi kwa wanafunzi wetu utakuwa mgumu. Naishauri Serikali kukisikiliza kilio cha walimu kwa kuboresha maslahi yao. Ahsante.