Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Nuru Awadh Bafadhili

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. NURU A. BAFADHILI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mimi napenda niende haraka haraka, nianze na suala zima la walimu waliostaafu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna walimu ambao wamestaafu hadi leo hawajapewa posho zao za usafiri kurudi makwao. Mpaka leo wamebaki katika vituo vya kazi. Sasa tunaomba Serikali ituambie lini itawalipa mafao yao hayo?
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kuzungumzia kuhusu walimu. Kuna walimu ambao wanadai baadhi ya malimbikizo yao, lakini baya zaidi kuna baadhi ya walimu walisimamia mitihani ya darasa la nne na darasa la saba toka mwaka 2015 hadi leo hawajalipwa pesa zao hizo za kusimamia mitihani. Nadhani kosa sio la Wizara lakini naiomba Wizara ihakikishe, iulizie hizi Halmashauri. Nadhani kuna ubadhirifu fulani katika hizi Halmashauri, kwa sabbau pesa zinatolewa, lakini walimu husika hawapewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu suala la UMITASHUMTA. Wanafunzi wa shule za msingi kuanzia sasa hivi nadhani wako katika michezo hii ya UMITASHUMTA, nadhani Serikali inatoa pesa, lakini bila shaka zile pesa ni kidogo. Kwa sababu kuna baadhi ya shule wako mbali na vituo vinavyofanyika hiyo michezo, hivyo inabidi wapate usafiri wa kwenda kule, kwa hiyo, inawagharimu walimu wao wenyewe wajitolee pesa zao kutokana na uhaba wa ile pesa inayopelekwa katika shule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walimu hao hao maskini ya Mungu hawana fedha za kutosha kujikimu wao wenyewe lakini pia wanaona kheri wawasaidie wale wanafunzi, kwa sababu utakuta mwanafunzi wakati mwingine anatoka nyumbani kwao hajala inabidi mwalimu ajitolee awaununulie angalau hata karanga watafune, pesa ile inatoka mfukoni kwa mwalimu. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali inapoandaa hii michezo ya UMITASHUMTA ihakikishe kuwa wanaweka fungu kubwa ambalo litawasaidia walimu kuwawezesha watoto waweze kwenda kucheza ile michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kuna hiki kitega uchumi cha CWT. Enzi hizo tuliambiwa kuwa ni kitega uchumi ambacho kitawasaidia walimu na jengo hili limejengwa Dar es Salaam, Ilala Boma pale Mwalimu Nyerere House. Lakini cha kushangaza sijui kitega uchumi hiki kinawasaidiaje walimu kwa sababu kuna walimu wengine kama sisi tumestaafu, kuna walimu wengine wamekufa na kitega uchumi bado kiko pale pale. Je, hawa waliostaafu na hawa waliokufa watasaidiwaje na kitega uchumi hiki? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la mimba za utotoni. Kweli watoto wetu wa kike wanapata mimba, miaka tuliyosoma sisi ilikuwa mtu akipata mimba ilikuwa ni mambo ya ajabu sana, lakini sishangai sana kwa sasa hivi kutokana na utandawazi uliopo. Mambo ni mengi, watoto wanaangalia luninga na wanakuta mambo mengi ambayo na wao wanafanya majaribio.

Ombi langu kwa Serikali, naomba ikiwezekana wafanye mobile clinics wawapitie kila wakati watoto wetu wa kike. Kwa sababu mwanafunzi atakapoona, eeh, nitakuwa kila wakati nafuatiliwa fuatiliwa afya yangu, kwa hiyo ataliogopa lile tendo kulifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwennyekiti, vile vile wanafunzi wetu wanapokuwa shuleni wanakuwa ni wengi mno madarasani kiasi ambacho mwalimu anashindwa kusahihisha, anashindwa kuwapa kazi za kutosha na hiyo haitoshi, utakuta mwalimu kutokana na wingi wa wanafunzi, darasa moja ni wanafunzi 80 anachagua baadhi ya wanafunzi wa madarasa ya juu wamsaidie kusahihisha. (Makofi)

Hata mitihani inasahihishwa na baadhi ya wanafunzi wa madarasa ya juu. Utakuta mwanafunzi karudi shuleni swali amelipata lakini amewekewa kosa na marks zake nimekatwa na akienda kwa mwalimu akimwambia, mwalimu, hili swali nimelikosa, anamwambia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)