Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Joram Ismael Hongoli

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lupembe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. JORAM I. HONGOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa nafasi na mimi niweze kupata kuchangia kwenye Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuanzisha utaratibu wa elimu bila malipo, nimpongeze sana kwa Wizara ya Elimu pia kwa kazi ambazo wanazifanya kwa maana ya Waziri, Naibu Waziri na Katibu wa Wizara hii na Makamishna wote na watengaji wote wa Wizara kwa kazi kubwa ambazo wanazifanya ili kuhakikisha kwamba Watanzania wanaweza kupata elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu wameeleza sana Waheshimiwa Wabunge na wameeleza vizuri sana kuhusu elimu kushuka. Mimi niseme kwamba hili suala halihitaji kuangalia upande mmoja, ni lazima Serikali, wazazi na wadau wote tuweze kushirikiana kuhakikisha kwamba ni namna gani tutaboresha elimu yetu. Mheshimiwa Rais ameweka elimu bure ili kutoa fursa kuhakikihs kwamba watanzania wote wanapata fursa ya kupata elimu ya msingi na sekondari. Kwa hiyo sasa kwa kuwa tayari Rais ameshafungua fursa sasa ni jukumu letu sisi wadau, wana taaluma, pia ni jukumu letu sisi Wabunge kuwaelimisha wazazi namna gani ya kuweza kushirikiana na walimu kwenye mashule ili elimu yetu iweze kuboreshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tukibaki tunalaumiana hivi hatutaweza kufanikiwa, lazima sisi sote tushiriki katika kuhakikisha kwamba elimu yetu kwenye majimbo yetu na kwenye maeneo yetu inaboreshwa. Kwa hiyo, jitihada za kuboresha elimu zinaanza na wewe Mbunge zinaanza na wazazi waliopo katika maneo husika lakini pia kwa kushirikiana na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme juu ya elimu hii ya ufundi. Tunaenda kwenye Tanzania ya viwanda ni lazima kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge wengine, ni lazima tuwaandae vijana wetu. Mimi nafikiri kama alivyoeleza Mheshimiwa Mwalongo alieleza vizuri sana katika mchango wake aliutoa juzi kwamba ni muhimu tuwe na masomo ya ufundi kwenye shule zetu za sekondari, lakini mimi niseme kwamba ni vizuri tuanze mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba kwenye kila shule ya msingi ikiwezekana tuwe na darasa la ufundi, wanafunzi wanapokuwa kwenye shule ya msingi wapate stadi za ufundi pale pale shuleni, kama ilivyokuwa zamani. Tulivyokuwa tunasoma shule ya msingi tulikuwa tunajifunza mambo mbalimbali. Kuna shule nyingine tulikuwa tunajifunza useremala, kuna shule nyingine wanajifunza utengenezaji wa vitu mbalimbali na hatimaye tukapata mafundi wengi, mafundi wengi wanaojenga nyumba sasa hivi huko vijijini na maeneo mengine, mafundi wengi wanaofanya kazi za welding yaani uungaji wa vyuma, mafundi wengi wanaofanya kazi za umeme wamejifunza wengine toka shule za msingi na wengine wamejifunza sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tukiamua kwamba shule zetu za msingi ziwe na angalau wanafunzi wawe wanapata kipind kimoja cha ufundi, nina hakika kabisa tutapata vijana wengie, tutapata mafundi michundo wengi. Kwa hiyo, mimi nitoe rai kwa Serikali, niiombe tubadilishe sera kidogo tuanzishe shule za misingi kule kule angalau kuwe na kipindi cha ufundi toka shule ya msingi, akienda sekondari akutane na darasa la ufundi na hatimaye wengine pengine waweze kwenda kwenye vyuo vingine huko juu. Kwa hiyo, watoto tukiwaanzisha mapema watapenda ufundi na watapenda kusoma masomo hata ya sayansi ili waje kuwa mafundi mazuri baadae. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haiwezekani kuanzisha kwenye shule zote basi angalau kwenye kata tuchague shule moja ambayo itakuwa ni shule ya msingi ya ufundi ili watoto waweze kujifunza pale, na ikiwezekana hata wale wengine wanaokaa maeneo yanayozunguka ile shule wanaweza wakaenda kujifunza elimu ya ufundi pale kwenye ile shule ya ufundi katika kata zetu. Kwa hiyo, tukianzisha utaratibu huu tutawezesha vijana wetu wengi kwanza kuwa na uwezo wa kujiajiri kwa sababu amejifunza ufundi fulani. Kwa hiyo, niombe sana Wizara tujaribu kuchukua mawazo haya ili tuweze kusaidia ili vijana wetu wengi waweze kuenenda na uchumi wa kati, uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeongea sana juu ya suala la lugha ya kufundishia. Imekuwa ni mjadala wa muda mrefu sana. Tumekuwa tukijadili kwamba either tuamue twende kwenye kiingereza au twende kwene kiswahili, na muda mwingi tumekuwa tukifundisha shule za msingi kwa kiswahili lakini wanafunzi hawa wakienda sekondari wanakutana na lugha ya kiingereza. Hii imekuwa ikileta confusion kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia watoto wa sekondari walio wengi hawaielewi lugha ya kiingereza na wengine wakiwa wanajibu mitihani wanaandika kwa kiswahili; na kwa kuwa wameandika jibu ambalo sio lugha rasmi, wametumia lugha isiyo rasmi wamekuwa wakikatwa kwa maana wakipata kosa kwenye yale majibu yao. Kwa hiyo kumbe Watanzania wengi wanaelewa kiswahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ni kwanini tusiamue sasa tukaanza darasa la kwanza mpaka Chuo Kikuu tukafundisha kwa kiswahili?

Mheshimiwa Mwneyekiti, wengine wamesema kwamba tutakuwa tumejifungia, hapana! Mbona nchi hizi zilizoendelea, tumeona China, tumeona Korea wanafundisha kwa lugha yao ya Kikorea lakini ndiyo nchi ambazo tunasema leo kwmaba zinakuwa uchumi kwa kasi kubwa sana. Na sisi tuamue, tusibakie tu kwenye kiingereza, tusibakie tu kwenye hii lugha ya wakoloni, turudi kwenye kiswahili. Tuanze kufundisha kiswahili toka darasa la kwanza, sekondari na hatimaye Chuo Kikuu, naamini Watanzania kwa sababu ni lugha mama wataelewa vizuri na wataweza kujibu majibu kwenye mithani vizuri na ufaulu utapanda kwa kuwa wanatumia lugha ambayo wao wenyewe wanaielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia juu ya Kitengo cha Udhibiti Ubora. Kitengo hiki cha Udhibiti Ubora kipo hoi, hawana magari, hawana fedha za kujaza mafuta kwenda kukagua shule na tumesema kwamba Udhibiti wa Ubora ndilo jicho la Serikali, ndilo jicho tunalolitumia kuangalia nini kinachoendelea kwenye shule zetu. Niiombe sana Serikali iwezeshe kitengo cha udhibiti ubora waweze kupata magari lakini pia waweze kupata fedha za kuweza kujaza mafuta na kwenda kukagua kwenye sule zetu hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ilivyo, kama Halmashauri haina fedha, wadhibiti ubora hawawezi kwenda kwenye shule, hawana uwezo wa kwenda kwenye shule kufanya ukaguziā€¦(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)