Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami pia nampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Naibu Waziri na Maafisa wote kwenye Wizara yake kwa hotuba nzuri. Naomba nianze kwanza kwa maombi maalum kwa Wilaya yangu ya Ileje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya yangu ya Ileje kwa ufadhili wa Balozi wa Japan tulijengewa Chuo cha Ufundi VETA tukaweza kupata majengo mawili na karakana na condition moja wapo ilikuwa Halmashauri imalizie jengo la utawala, vyoo na sehemu ya kulia chakula. Niliwaomba Wizara watusaidie wakatupa conditions kuwa tupanue eneo la hiki chuo, tusajili ile ardhi, kwa mfano tuwe na title deed, halafu ndiyo tutaikabidhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuliwaandikia barua mwezi tarehe 8 Novemba, 2017 kuwa tumekamilisha na tunaomba sasa waichukue ili waiendeshe na kumalizia miundombinu iliyobakia kama ambavyo wenyewe walikuwa wameahidi wangefanya. Sasa naangalia katika kitabu hiki cha hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 26 - 27 ambako ndiyo amezungumzia masuala ya VETA, sioni sehemu yoyote ambapo imetajwa Ileje na sielewi sasa hiki chuo kimeshasimama zaidi ya miaka mitatu hakifanyi kazi na ndicho chuo pekee cha ufundi Mkoa mzima wa Songwe. Pengine sasa wangetufikiria jinsi gani watatusaidia, japo kianze kufanyakazi. Kwa sababu hata mfadhili wa kwanza ameahidi kurudi tena kutusaidia lakini mradi kianze kwanza, hilo ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Ileje ni Wilaya ya pembezoni na ni Wilaya kongwe na kwa miaka mingi hatuna shule ya wasichana ya boarding wala ya day. Watoto wetu wa kike inabidi wakae ama kwenye mabweni machache ambayo hayatoshi au wapange kwenye nyumba za watu au wanakwenda Wilaya nyingine kabisa kwenda kusoma shule za sekondari. Tuna tatizo kubwa la mimba za utotoni kwa sababu ya matatizo yanayowapata wasichana katika hekaheka hizi za kutafuta elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wazazi wanakuwa na gharama kubwa sana inapobidi wasafirishe watoto wao kwenda kuwapeleka kusoma Wilaya nyingine. Je, kwa nini Serikali haina utaratibu wa kuwa na shule ya wasichana ya sekondari kila Wilaya kama ambavyo ni utaratibu wa mambo mengine katika Wizara zingine? Tunaomba sana tusaidiwe tayari wenyewe tuna mikakati ya kuanza ujenzi wa shule ya sekondari ya wasichana, lakini tutahitaji Serikali na yenyewe kutia mkono wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maoni mengi yametolewa na Waheshimiwa Wabunge pande zote, ningependa hayo pia yazingatiwe. Kamati imetoa maoni mazuri sana, naomba yote kama ikiwekeza yazingatiwe kwa sababu ninaamini kabisa yakifanyiwa kazi hayo hii Wizara itafanya kazi nzuri zaidi na watoto wetu watafaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije sasa kwenye suala zima la VETA na Vyuo vya Ufundi Stadi au Vyuo vya Kati. Imetokea tabia au mtindo kuwa vyuo vya kati vikifanya vizuri vinapandishwa na kufanywa kuwa vyuo vikuu, nafikiri tunafanya makosa makubwa sana kwa kufanya hivyo. Vyuo vya Kati ni vyuo vinavyofundisha masuala ambayo ni ya moja kwa moja yanaweza kuingia katika ajira, kwenye viwanda na hali kadhalika, kwa sasa hivi tunazungumzia uchumi wa viwanda, huu ndiyo ulikuwa wakati sasa wa kuboresha vyuo vya kati, kuviongezea mitaala ambayo inalingana na mahitaji ya viwanda tunavyotaka kwenda kuvijenga na kuvifanya viwe vinatoa ufundi mzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuhamasisha kama itawezekana, vyuo vya ufundi vyote vifundishe kwa mitaala yao kwa kiswahili, itawasaidia hawa mafundi wadogowadogo ambao wanatusaidia mitaani magari, redio, television, karakana mbalimbali hizi wale vijana wangefundishwa kwa Kiswahili kwa sababu wengi ni darasa la saba na form four tungejikuta tuna mafundi ambao wana weledi mzuri badala ya ule wa kubahatisha, vilevile tukajikuta kuwa tumeanzisha ajira nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado niko katika masuala ya vyuo vya ufundi, hasa VETA. VETA tumekuwa tukiichangia fungu la skills development levy ya asilimia 4.5; theluthi moja ndiyo imekuwa ikienda VETA moja kwa moja, theluthi mbili ya tatu imekuwa ikienda Serikali Kuu. Sasa hii inachangiwa na waajiri. Waajiri hawa hawajui ile theluthi mbili inakwenda kufanya kazi gani, kwa sababu lengo ilikuwa ni kupeleka VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu tayari waajiri wanakuwa na wasiwasi kwa nini hela haiendi yote VETA? Nashauri kwamba sasa hivi tunataka kwenda kwenye uchumi wa viwanda, VETA zetu lazima ziimarishwe, basi lile fungu lote la asilimia 4.5 liende VETA moja kwa moja kama ambavyo hiyo theluthi moja inakwenda. Hii kwanza itawafanya waajiri wenyewe wanaochangia kuwa na imani, lakini vilevile wanaweza hata kuweza kuchangia zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kuhusu VETA na vyuo vya ufundi stadi viko chini ya Wizara ya Elimu lakini vinalenga waajiri ambao wako chini ya Wizara ya Kazi na Ajira.

Ninapenda kuihamasisha Serikali kama itawezekana na kama ambavyo inafanyika kwenye nchi nyingine nyingi, VETA na vyuo vya ufundi stadi viende chini ya Wizara ya Kazi na Ajira kwa sababu kwanza itakuwa ina uhusiano wa moja kwa moja na itajibu moja kwa moja hoja za waajiri juu ya mahitaji yao ya ajira. Jinsi ilivyo sasa hivi waajiri hawana namna ya kuongea na Wizara ya Elimu kuhusiana na masuala haya kwa sababu hakuna ule uhusiano wa moja kwa moja, lakini wakiwa kwenye kazi na ajira moja kwa moja kutakuwa kuna mahusiano ya waajiri ambao ndiyo wanawahitaji hao wafanyakazi wenye weledi na Wizara, lakini vilevile itapunguzia Wizara hii kazi nyingi. Hii Wizara inashughulikia mambo mengi mno, matokeo yake hata ufuatiliaji wa ufanisi unapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara moja inashughulikia elimu ya msingi, sekondari, vyuo vikuu, ufundi stadi, maktaba, taasisi mbalimbali, sasa vitu vyote hivi viko chini ya Wizara moja halafu haohao wasimamie ubora, wasimamie utoaji huduma, wasimamie miradi, kwa kweli naona kama tumerudhika vitu vingi sana kwa Wizara moja. Serikali... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)