Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia hotuba hii muhimu iliyopo hapa mbele yetu. Nianze kwa kutoa pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri, Profesa kwa kazi nzuri ambayo anaifanya kusimamia sekta ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo masuala machache ambayo ningependa kuchangia na nitajaribu kwenda kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kwanza ambayo ningependa kuchangia ni kwamba sote tunaelewa Wizara ya Elimu ndiyo inayotoa sera na miongozo ya kusimamia elimu, lakini pia Serikali inazo shule ambazo nyingi zinasimamiwa na TAMISEMI, kwa hiyo Serikali inatoa sera lakini vilevile inamiliki shule. Huwezi ukawa wewe ndiyo unamiliki shule na wewe mwenyewe ndiyo unatoa sera na unajisimamia. Nadhani wakati umefika wa kuwa na chombo ambacho ni independent cha kusimamia elimu na chombo hicho sasa tukiunde, kitaundwa kwa sheria (Tanzania Education Regulatory Authority) kisimamie shule za Serikali lakini pia kisimamie shule za binafsi na kifanye hivyo kwa usawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili linawezekana na tukifanya hivyo tutaweza kupiga hatua kwa sababu haiingii akilini unakuta Afisa Elimu anasimamia shule binafsi ina upungufu wa choo kimoja au vyoo viwili inafungwa halafu unakuta shule ya Serikali haina choo lakini inaendelea, hii inakuwa siyo sawa. Jambo hili inabidi tuliangalie, labda niseme tu mimi similiki shule lakini siku zijazo ninaweza nikamiliki shule pia, kwa hiyo sina maslahi yoyote katika hili bali nazungumza kwa maslahi mapana ya maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ningependa kuzungumzia changamoto. Ziko changamoto nyingi zinazoikabili sekta ya shule binafsi na nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Hussein Bashe kwa taarifa nzuri aliyowasilisha kwa niaba ya Kamati yake. Mheshimiwa Hussein Bashe kati ya jambo ambalo na mimi najivunia kwa sababu nilikufundisha siasa na naona unajifunza vizuri uendelee hivyo na kwa taarifa uliyowasilisha hapa imebainisha mambo mazito ambayo yatasaidia sekta ya elimu, kwa hiyo unapofundisha wanafunzi wako na wakafanyakazi nzuri wapongeze. Mheshimiwa Bashe nakupongeza kwa kuwasilisha vizuri mawazo ya wenzako kwenye Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ziko nyingi, changamoto hizi lazima tuziangalie na tuzifanyie kazi. Moja, ukiangalia shule binafsi tuna zaidi ya shule 4,000 sasa na shule za Serikali zipo lakini ukiangalia matokeo ya mwaka jana 2017 shule 100 zilizofanya vizuri kulingana na matokeo yaliyotolewa na Wizara ya Elimu, Serikali ilikuwa na shule nne na shule binafsi ni 96 ukiona hivyo maana yake lazima tuangalie Serikali tuna kazi ya kufanya lakini pia lazima tuendelee kuziunga mkono shule hizi binafsi kwa sababu zinapofanya vizuri ndipo tunajivunia kwamba sasa shule 100 bora, kwamba shule 100 bora hizi, 96 ni binafsi na nne tu ndiyo za Serikali sasa ikishakuwa hivyo ni vizuri kuziwezesha hizi shule na kushughulikia changamoto zinazowakabili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya changamoto zinawakabili ni utitiri wa fedha ambazo wanalipishwa. Kwa mfano, ukihitaji walimu kutoka ndani ya Afrika Mashariki kama ni shule binafsi unaambiwa lazima uende Idara ya Labour kule ulipe dola 500 kwa kila mwalimu pia ulipe dola 550 Idara ya Uhamiaji kwa kila mwalimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kati ya jambo ambalo nikiri nadhani na wewe baadae utakiri kati ya jambo ulipokuwa Waziri na mimi nilikuwa Naibu wako tulipokuwa tuna-negotiate common market kati ya jambo ambalo nadhani tulikosea ni pale tuliporuhusu kwamba sasa hizi ada zitaendelea kuwepo na tulisema kwamba ziwe kidogo a token, isiwe chanzo cha mapato, lakini kama unavyofahamu siku hizi mawazo yetu tulifikiri hii haitakuwa chanzo cha mapato watu wamegeuza imekuwa chanzo cha mapato sasa matokeo yake tunaziadhibu shule binafsi bila sababu ni jambo ambalo nadhani liangaliwe kwa sababu linaongeza gharama nyingi bila sababu za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nadhani tuliteleza ukikosea lazima ukubali makosa tulizungumza wakati ule kwamba tunahitaji tu walimu wa degree peke yao kutoka nje ya Tanzania, tulifikiri tunao walimu wa kutosha ndani ya nchi, lakini ukweli umeonesha kwamba hata ndani ya nchi hatuna walimu wa kutosha ndiyo maana tuna upungufu wa walimu, pia ukianagalia kwa umakini ni kwamba kwa upande wa walimu wa kufundisha hizi za english medium tuna upungufu wa walimu wa sayansi 26,000 na kila mwaka tuna uwezo wa kutoa walimu 2000 sasa tunapozuia kwamba walimu wasitoke nje ya Afrika Mashariki tunajiadhibu wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni changamoto ambayo ziko na kodi nyingi zimeorodheshwa hili ni jambo la kuangalia kinachotakiwa ni dhamira ya kujua kwamba shule binafsi hizi siyo binafsi, kwangu mimi naweza nikasema hakuna shule binafsi ni kwamba unakuwa na shule mbalimbali nyingine kwa sababu una uwezo unaziendesha mwenyewe ambazo hauna uwezo unakariobisha private sector inafanya kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Waziri kule kwetu Misenyi tuna Minziro High School tunajenga kule, Bwabuki tunajenga high school pale na Bunazi tumeanzisha high school inafanya vizuri, nichukue nafasi hii kumuomba Mheshimiwa Waziri tunapoendelea kujenga shule hizi high school ambazo ni muhimu sana basi niombe Wizara yako itusaidie wananchi wa Misenye ili tuweze kuenda kwa kasi ambayo inatarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi pia kuzipongeza shule binafsi zilizo katika Wilaya ya Misenyi, niipongeze Kadea Sekondari ambayo ina headmaster huyu anatoka Uganda, lakini shule hii inafanya vizuri sana karibu kuliko shule zote na kitu kikubwa alichonacho huyu headmaster anasisitiza discipline. Nadhani discipline ni jambo muhimu sana ukiangalia Kadea Sekondari kitu peke inachozishinda shule zote zilizotuzunguka pale ni discipline, wakifanya mitihani wanafanya vizuri kuliko shule zote, lakini kuna shule nyingine pale Kanyigo inaitwa Kanyigo Islamic Seminary na hii inafanya vizuri sana ukiangalia sifa yao kubwa waliyonayo ni discipline, ukienda kule Tweyambe wanafanya vizuri sana ni private hizi sifa kubwa waliyonayo ni discipline. Kwa hiyo, Profesa nadhani eneo hili la kusisitiza umuhimu wa discipline mliangalie jinsi gani na shule zetu za Serikali zinaweza zikatoa kipaumbele kwanye masuala ya discipline ili tuweze kuendelea kufanya vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.