Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara yetu hii ya Mambo ya Ndani. Nianze kwa kuipongeza Serikali kupitia Wizara yetu ya Mambo ya Ndani kutokana na hali ya usalama wa nchi na wananchi pamoja na mali zao. Jeshi la Polisi pamoja na majeshi mengine ambayo yako chini ya Wizara hii yamefanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako maeneo machache ambayo napenda kushauri. Wenzangu waliotangulia wameshaanza kusema, nianzie na Jeshi la Polisi. Jeshi la Polisi pamoja na kwamba wanafanya kazi nzuri, lakini kwa kweli askari wetu hawa wanafanya kazi katika mazingira magumu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazingira ya watumishi wa Jeshi la Polisi ni magumu sana kwa sababu hawana vitendea kazi, usafiri, majengo yao wanayofanyia kazi katika ofisi ni mabovu sana lakini na makazi yao ni duni kabisa na kuwafanya wale watumishi kuwa kama wamekata tamaa. Wakati mwingi inakuwa kama vile wamesahaulika labda kutokana na wingi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda sana nishauri katika bajeti hii ambayo tunaendelea wajaribu kuliangalia. Sasa hivi kama Mheshimiwa Waziri alivyosema tayari kuna ujenzi umeshaanza kwa mfano kule Arusha tukishirikisha wadau. Yako maeneo ambapo wadau wa maendeleo hawa hawana michango mikubwa sana hasa katika sekta hizi za ulinzi na usalama kutokana na mapato yao au jiografia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukitegemea sana wadau wa maendeleo na Serikali tukakaa pembeni tu kwa kweli yako maeneo ambayo wanajeshi wataendelea wetu kupata matatizo makubwa ya vitendea kazi lakini kuendelea kuishi katika maisha duni na hivyo kutoa huduma zilizo duni kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule jimboni kwangu kwa kweli, nilishamwomba hata Mheshimiwa Waziri aweze kufika, vituo vyetu vya polisi vinatia kinyaa. Yako maeneo kwa mfano ukienda katika Kata moja ya Ngimu, kituo cha polisi wamekwenda kukodisha eneo la Serikali ya Kijiji, wamekwenda kukodisha kwenye majengo ya zamani ya Chama cha Mapinduzi na wanashindwa hata kuyakarabati majengo hayo kwa sababu kwa upande mmoja wanaona majengo sio yao na kwa upande mwingine Jeshi letu la Polisi halina fedha za kutosha kuweza kufanya ukarabati wa majengo haya. Matokeo yake ni nini sasa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia wale watumishi wanakaa kwenye nyumba za kupanga. Wakati mwingine ni mbali kabisa na maeneo wanakotakiwa kufanya kazi. Jambo hili linarudisha nyuma sana utendaji wa Jeshi letu la Polisi kwa sababu pale ambapo wananchi wanawahitaji kwenye vituo hawawezi kupatikana kwa urahisi. Ukizingatia bado tunalo tatizo la miundombinu ya mawasiliano hata kuwapata askari imekuwa ni shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Wizara ifanye mkakati wa makusudi wa kuhakikisha kwamba tunaboresha sana mazingira ya kufanyia kazi kwa askari wetu ili hizi huduma ambazo tunaziomba za kutoka Jeshi la Polisi za ulinzi na usalama ziweze kupatikana kwa urahisi, lakini tuweze kuwatia moyo askari wetu kufanya kazi ya kuilinda vizuri nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo hili ni kubwa. Wamezungumza waliotangulia, hatuna fedha za kupeleka hata mahabusu wetu kwenye mahakama zetu, kwenye Mahakama za Kata wakati mwingine hata kwenye Mahakama za Wilaya na hivyo tunajikuta kwamba haki za wananchi zinacheleweshwa ama hata wakati mwingine zinapotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vingine havina hata sehemu ya kutunzia mahabusu, tunao ushahidi kabisa kuna maeneo wananchi wamelazimika kwenda kuvamia sehemu hizo na kuwatorosha wahalifu wale ambao walikuwa wanakusudiwa kupelekwa katika vyombo vya kutolea haki. Sasa ni vizuri sana Serikali ikaangalia suala hili na kuona kwamba tunahitaji kwa kweli kuwa na mazingira mazuri ya kufanyia kazi katika vituo vyetu vya polisi kuanzia kwenye kata hata ngazi ya wilaya ili kusudi wananchi waweze kupata haki zao kwa wakati wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze sana Wizara kuna zoezi la vitambulisho linaendelea na hata kule jimboni kwangu naona sasa wanakwenda na wananchi wanaendelea kupata vitambulisho hivyo. Niombe kasi hii iongezeke na wananchi wapewe taarifa ili katika zile siku ambazo zimepangwa, tuweze kuhakikisha kwamba tunatoa huduma hii kwa haraka na kuhakikisha kwamba wananchi walio wengi wanaostahili kupata vitambulisho wanaweza wakapata vitambulisho kabla wale watendaji wetu hawajahama katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lipo pia suala la namna ya kuwahudumia mahabusu wetu hasa kwenye masuala ya chakula. Tunawategemea sana wananchi wale ambao wapendwa wao wanakuwa wamechukuliwa na bado wako chini ya polisi hawajafikishwa mahakamani kutoa support ya chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengine kwenye jimbo kama la kwangu vituo vya polisi hivi viko vichache mno na unakuta wananchi wale ambao wanatakiwa kuwahudumia ndugu zao wako mbali. Wananchi wanapata tatizo kubwa la kuweza kuwahudumia wale ndugu na wakati mwingine wasipopata nafasi ya kufika pale, askari wetu wanapata shida kubwa sana ya kuhakikisha kwamba mahabusu hawa wanaweza wakapata angalau huduma zile za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Jeshi letu la Polisi na Wizara tuangalie namna ya kuweza kusaidia katika maeneo haya. Kwa sababu hawa wananchi hawajahukumiwa kwamba wametenda makosa, wana haki ya kuendelea kupata chakula, wana haki ya kusikilizwa, zipo haki za kimsingi ambazo wanastahili kuzipata ili kusudi tusianze kuwahukumu kabla hata hawajafika mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni la muhimu sana kwa sababu kesho na keshokutwa na sisi pia, tutakuwa huko, vituo vyetu hali zake ndiyo hizi hakuna hata mahali pazuri pa kuwaweka wananchi. Kwa hiyo, niombe sana Wizara waangalie namna ya kuweza kuboresha miundombinu hii lakini huduma za chakula, mafuta kwa ajili ya askari wetu na vitendea kazi. Hata wale ambao tumewapa pikipiki, tusiwape tu pikipiki tukashindwa kuwapa mafuta na fedha za matengenezo ili waweze kuendelea kufanya patrol maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la usalama barabarani. Nilipongeze sana Jeshi la Polisi, sasa hivi utii wa sheria bila shuruti umeongezeka kwa kiasi kikubwa. Hili ni jambo jema na la kujivunia sana. Pamoja na kwamba yako maeneo mengine bado askari wanafanya kazi za kuvizia ni kutokana na tabia ya sisi madereva ambao wakati mwingine tunalazimika kuanza kuviziwa katika maeneo hayo. Niombe sana Wizara tufanye kazi kubwa na hasa Jeshi la Polisi ya kuendelea kuwaelimisha wenzetu hawa madereva.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi hii ya kutoa elimu kwa madereva ni muhimu sana kuliko kutoza fine. Pamoja na kwamba nimesikia katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri inawezekana kwamba tukakimbilia sana kwenye fine ili kuongeza mapato, njia hii haiwezi ikatufanya tukawa na utii wa sheria bila shuruti. Wako wengine wenye fedha wanavunja sheria kwa makusudi ili kusudi waweze kupigwa fine na wanalipa lakini wanaendelea na uvunjaji wa sheria na maisha ya wananchi wetu yanaendelea kupotea kwa sababu ya madereva wa aina hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Jeshi la Polisi litoe sana elimu kwa madereva hawa kila siku maana ni lazima kukazia maarifa. Madereva hao wanafanya makosa wakati mwingine sio tu kwa sababu wana fedha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kuunga mkono hoja.