Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

Hon. Mattar Ali Salum

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shaurimoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi

MHE. MATTAR ALI SALUM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia leo. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwa mzima wa afya na kuweza kusimama katika hili Bunge kuweza kuchangia siku ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayoifanya ya kutoa passport mpya. Vilevile nichukue nafasi hii kumshukuru Rais kwa kuhakikisha Watanzania waliotimia umri wanapata vitambulisho vya Utanzania ili viweze kuwasaidia katika mahitaji yao ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Kamishna wa Jeshi la Polisi wa Zanzibar kwa kuteuliwa kuwa Kamishna wa Jeshi la Polisi wa Zanzibar. Nimpongeze sana na nimtakie kazi njema kwa upande wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niipongeze Wizara inafanya kazi nzuri ya kuhakikisha wanasimamia utoaji wa passport mpya. Vilevile niwapongeze sana Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya ya kuhakikisha Watanzania waliotimia miaka ya kupata vitambulisho vya Utanzania wanapata vitambulisho vya Mtanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar tuna vitambulisho vya Mzanzibar Mkaazi. Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilifanya kazi kubwa sana kwa kutumia kodi za Wazanzibari kuhakikisha wanapata vitambulisho hivi ili viweze kuwasaidia katika majukumu yao ya kukuza uchumi. Kazi ya kwanza ambayo ni muhimu sana Serikali ya Zanzibar ilifanya ni kutoa vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi ili kuhakikisha Wazanzibari wanapata passport ya Mtanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kushangaza sana vitambulisho vya Mzanzibari kwa sasa huwezi kupatia passport ya Mtanzania. Ili upate passport ya Mtanzania unatakiwa lazima uwe na kitambulisho cha Mtanzania. Kinyume na miezi mitatu iliyopita kitambulisho hiki cha Mzanzibari unaweza kupata passport ya Mtanzania. Hii leo huwezi kupata passport ya Mtanzania kwa kutumia kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia system ya Uhamiaji, kitambulisho cha Mtanzania na kitambulisho cha Mzanzibari kimoja hapo ukikitumia unaweza kupata passport ya Mtanzania. Jambo la kushangaza sana Mheshimiwa Waziri na nimwombe sana hivi sasa anapokwenda na kitambulisho cha Mzanzibari Mkaazi kinaambiwa hakifahamiki na huwezi ku-issue passport.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo ni la kushangaza sana, hiki kitambulisho cha Mzanzibari ikiwa Serikali ya Zanzibar imetumia gharama na kodi za Wazanzibari kuhakikisha wanapata kitambulisho hiki ili kujikwamua na maisha yao, leo unawaambia haiwezekani kupata passport mpaka mtu awe na kitambulisho cha Mtanzania. Niombe sana Wizara kama kitambulisho hiki cha Mzanzibari Mkaazi kina tatizo, basi waweze kutuambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Wizara kama Serikali kama kitambulisho hiki kama kina tatizo wana uwezo wa kulitatua tatizo basi litatuliwe ili waliokuwa nacho kitambulisho hiki waweze kupata passport kwa kutumia kitambulisho hiki cha Mzanzibari. Wazanzibari wengi wamehamasika na wamechukua vitambulisho hivi vya Mzanzibari kwa nia nzuri ili waweze kupata passport ya Mtanzania na waweze kufanya kazi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashangaa sana kwa nini kitambulisho hiki kwa sasa huwezi kupata passport na ni kipindi kifupi ndiyo limeanza hili suala kwamba kwa kitambulisho hiki huwezi kupata passport. Vilevile ukitaka kitambulisho cha Mtanzania kwa upande wa Zanzibar zaidi ya siku 30 ndiyo unapata kitambulisho hiki cha Mtanzania. Kama hakuna uwezekano wa kuhakikisha kitambulisho chetu cha Mzanzibari unaweza kupata passport wapunguze muda ili Wazanzibari waweze kupata kitambulisho hiki cha Mtanzania kwa haraka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie jambo la pili kuhusu vituo vya polisi. Wakuu wetu wa vituo vya polisi wanapata shida sana. Mkuu wa Kituo cha Polisi anapewa mahabusu zaidi ya 40 ambao wanahitaji kula, lazima mkuu wa kituo kufanya maarifa wale mahabusu au watuhumiwa waweze kula kwa kutumia pesa zake mfukoni. Mkuu huyu wa kituo cha polisi atakuwa na uwezo gani wa kuwalisha mahabusu kila siku? Pesa za kula ndani ya vituo vyetu vya polisi haziendi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine unakwenda kituoni kushtaki, unaambiwa gari lipo lakini mafuta hakuna. Inabidi Mkuu wa Kituo atoe pesa za mafuta au Mkuu wa Kituo yule aweze kupata gari na aweze kwenda au Mkuu wa Kituo hana wewe uliyekwenda kushtaki kesi unatakiwa utoe pesa zako mfukoni kutia gari mafuta ili kesi yako iweze kushughulikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni la umeme. Hata na mimi mwenyewe nimeshawahi kuchangia umeme ndani ya kituo cha polisi, hawana pesa za umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.