Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuwashukuru Wabunge wote waliochangia katika Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ya mwaka 2018/2019 kwa kauli na maandishi. Naishukuru Kamati yangu ya Kudumu ya Bunge ya Huduma ya Maendeleo ya Jamii kwa maoni na ushauri walioutoa kupitia hotuba ya Kamati hiyo ambayo imewasilishwa mapema leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba michango yote iliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge ni muhimu sana kwa maendeleo ya sekta ya habari, utamaduni, sanaa na michezo. Pia namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri Mheshimiwa Juliana Shonza kwa kuyatolea maelezo baadhi ya maswali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba yangu imechangiwa na jumla ya Waheshimiwa 41, ambapo waliochangia kwa maandishi ni Waheshimiwa 23 na kwa kauli ni Waheshimiwa 18. Wabunge hawa 41 wamezalisha hoja na maswali 214, hivyo basi majibu na ufafanuzi tutakaotoa utajikita kwenye baadhi tu ya hoja za Kamati na baadhi tu ya hoja za Waheshimiwa Wabunge na nitaeleza kwa kifupi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya Kamati ya kwanza ambayo nimeona ni muhimu kuijibu ni kwamba, lini Serikali itakamilisha uundaji wa Bodi ya Ithibati na Baraza Huru la Habari. Ningependa nieleze tu kwamba pamoja na kwamba mwaka huu wa fedha tumeshaomba fedha kwa ajili ya uanzishwaji wa Bodi ya Ithibati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, bado mchakato huu unavihusu sana vyombo vya habari vyenyewe, kwa sababu Serikali ikikimbia sana ikaanzisha Bodi ya Ithibati, ikaanzisha Baraza Huru la vyombo vya Habari, kesho tutaambiwa hilo ni baraza lenu nyie wenyewe, sisi haituhusu. Naviomba vyombo vya habari vijitokeze na vyombo vyao mbalimbali ili tuweze kukamilisha zoezi hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo kubwa la hii sheria ni kutaka vyombo vya habari vijiendeshe vyenyewe, viwe self governing, tunataka tuwe na self governing media industry na itaunda Baraza Huru la Habari. Kutakuwa na Bodi ya Ithibati na Kamati ya Malalamiko na Mfuko wa Habari kwa ajili ya Maendeleo ya hii Tasnia. Inaitambua tasnia hii sheria mpya, kuwa ni taaluma na wana taaluma hawa wawe na sifa stahili kuanzia Diploma na kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa lilipokuja hapa Bungeni, ndipo utata ukajitokeza kwamba sasa hawa waliosoma hawapo, lakini tunajua wapo wengi, ndipo kikatolewa kipindi cha miaka mitano kuruhusu Waheshimiwa ndugu zetu Waandishi wa Habari waweze kusoma, lakini nina uhakika hata tukianza kesho Waandishi wenye Diploma, wenye Degree wako wengi sana. Nawaomba Waheshimiwa Waandishi wa Habari wenyewe wawe mstari wa mbele. Tukiunda sisi, zitaanza hizo ngonjera za kwamba hiyo ni Kamati ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine lilikuwa Kanuni za Sheria za Habari hazijatungwa mpaka leo. Hii ni hoja ya Kamati, lakini kwa heshima kubwa kabisa naomba kusema kwamba Wizara ilishakamilisha Kanuni za Sheria ya Habari na kanuni hizo zilichapishwa kwenye Gazeti la Serikali mwaka jana mwezi Februari tarehe tatu na zilishaanza kutumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ilikuwa ni Serikali iweke mkakati wa kuwa na Kanzidata Wataalam wote wa Kiswahili nchini ili watumike kama Wakalimani katika maeneo mbalimbali hasa mikutano ya Kimataifa. Kwenye hotuba yetu iko wazi na huu ni ubunifu mkubwa wa Wizara ambao tayari tumeshaanza kuutekeleza. Tunachotaka tu ni kutoa wito kwa Waheshimiwa Wabunge ambao tunaelewa, baadhi yenu hapa ni mabingwa wa lugha ya Kiswahili kwa kusomea, naomba na ninyi mjitokeze kujisajili katika tovuti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwepo na suala la wizi wa kazi. Suala hili tumelifanyia kazi sana na nimelieleza kwenye hotuba yangu kwamba tumefanya kaguzi mara kwa mara katika sehemu mbalimbali korofi na tumeweza kukamata kazi nyingi za sanaa ambazo zinaingia kinyemela kuweza kuumiza vijana wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Mkoa wa Dar es Salaam tuna kesi tunayoisema sana ambayo tulifanikiwa kesi ya jinai namba 414 ya mwaka 2011 ambapo Mahakama ya Wilaya ya Ilala ilitoa hukumu ya kutaka kazi ambazo zilikuwa zimeingia kinyemela, zinauzwa kinyemela kuwaumiza wasanii, ziweze kuharibiwa chini ya usimamizi wa Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli tulilipongeza sana Jeshi la Polisi kwa kazi kubwa iliyofanyika na Mahakama kufanya uamuzi huo haraka. Kwa hiyo, tunafanya hiyo juhudi kubwa kuhakikisha kwamba wasanii hawaendelei kunyonywa. Sasa hivi tunaipitia Sheria ya Haki Miliki na nina uhakika italeta sura nzuri tu baada ya muda siyo mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwepo na suala la mapato ya Uwanja wa Taifa na Uwanja wa Uhuru kwamba yasichanganywe. Kamati kwa kweli tunashukuru sana kwa hoja hii, lakini ningependa tu nisisitize pengine tupate maelekezo mengine ya wazi kabisa ya Kamati pesa yote inakusanywa kwa njia ya kielektroniki. Mapato yote ya hivi viwanja na kwa sababu fedha yote hii inakwenda Mfuko Mkuu, wahusika kule wanaona kabisa hii ni Uwanja wa Taifa, hii ni Uwanja wa Uhuru kwa sababu hakuna anayeshika hela taslimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninachoomba tu ni kwamba kama Wizara kwa kweli tuna kifungu kimoja tu cha kukusanya mapato hayo kwa jina la Uwanja wa Taifa na code yake tena ni 140259, lakini kama ni muhimu sana tupate code ya pili itawezekana, lakini kwa kweli tunakusanya hiyo pesa lakini imetoka wapi, inaeleweka kabisa kwa mtu anayepokea kwenye Mfuko Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala kwamba uchunguzi ufanywe kuhusu fedha za Mchina, yaani kuna Wachina wanapewa fedha zinazokatwa katika kila mchezo na Bunge lako Tukufu lipewe taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii hoja imesisitizwa sana na Kamati yangu. Ningependa nilieleze ili pengine nieleweke vizuri pole pole, kwamba katika mgawanyo wa fedha unaofanyika kwa asilimia, hakuna kipengele cha fedha ya Mchina au Wachina, sijawahi kuona mimi tangu niingie kama kiongozi wa Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ila ninaambiwa huko nyuma kulikuwepo na utaratibu wa kuwalipa Wachina. Kuna technical team ipo pale uwanja wa Taifa ilikuwa inalipwa kwa kazi iliyokuwa inafanyika, ni huko nyuma, lakini sasa hivi sijaona wala Afisa Masuuli wangu Katibu Mkuu hajawahi hata siku moja akaidhinisha hela iende kwa Mchina au Wachina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishuhudie tu kitu kimoja, kwamba tukishapata mapato mgawanyo ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tunatoa asilimia 18 ya VAT na asilimia tano ya Selcom ambao ndio waliokuwa service providers. Ikishatolewa hii kinachobaki ndio asilimia 100. Sasa mgawanyo unakuwa kama ifuatavyo:- asilimia 15 ni ya uwanja ambayo pia hatukai nayo tunaipeleka Mfuko Mkuu, asilimia tano ni ya TFF, asilimia 40 ni ya timu mwenyeji, asilimia 20 ni ya timu ngeni, asilimia tisa ni bodi ya ligi, asilimia saba gharama za mchezo na hizo gharama za mchezo na hiyo pesa inakwenda TFF huko huko, asilimia moja inaenda BMT na asilimia tatu DRFA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, pengine nitumie nafasi hii vile vile kumwelezea Mheshimiwa Kadutu, alisema sana kwamba BMT inapata hela nyingi hapo. Hapana si asilimia 15 ni asilimia moja tu na kwamba hiyo moja pengine tuipe TFF lakini TFF hapa wana asilimia tano kuna asilimia saba gharama za mchezo; ndio hao TFF, kuna asilimia tisa bodi ya ligi; hao hao ndio TFF, BMT asilimia moja. Kwa hiyo, nafikiri nimejieleza, limeeleweka kuhusu hayo malipo ya Mchina; hayapo tena na kama yalikuwepo hapo nyuma ilikuwa ni utaratibu wa kuwalipa wale technical team ya kichina iliyopo pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lilikuwepo lingine la uwepo wa udhibiti wa mapato yatokanayo na uuzaji wa tiketi kwa njia ya kielektroniki. Nashukuru sana, hili wazo zuri, Kamati yangu kwa kweli ni makini sana. Wizara kwa kutambua umuhimu wa kudhibiti mapato imeshakamilisha mchakato ulio wazi wa kumpata mtoa huduma ya kukusanya mapato kwa mfumo wa kielektroniki katika uwanja wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo huo tutauunganisha na mfumo wa Serikali wa ukusanyaji mapato (Government Payment Gateway System) ili kuimarisha udhibiti wa mapato. Hili tunaahidi na nadhani tutakapokutana na Kamati tena wataona hicho kimefanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwepo kwa maandalizi mazuri ya Timu ya Taifa ili ziweze kushiriki kikamilifu kwenye mashindano na kurudi na ushindi. Waheshimiwa Wabunge wengi sana nitashindwa wengine kuwataja, wengi kwa maandishi na kwa kuongea hapa, wamelalamikia sana hilo na kwamba Serikali ipo ipo tu, hatufanyi chochote kuhusu hizi timu zinaenda tu; hiyo si picha ya kweli. Mheshimiwa Chumi, Mheshimiwa Mwamoto, Mheshimiwa Ngeleja, Mheshimiwa Sima na Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea hilo na wametoa na mfano vilevile kuhusu timu yetu ilipokwenda Australia kwenye Jumuiya ya Madola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba ukichukulia michezo iliyokwisha juzi ya riadha, ndondi na michezo mingine Australia, wawakilishi wetu waliandaliwa vizuri, hivyo naomba niwasisitizie hilo na tumeiandaa sisi Serikali. Tulipewa nafasi 34 lakini tukaamua sisi wenyewe kwa ajili ya kujali viwango waende 22 tu. Kushindwa kupata medali ni kawaida ya mchezo, asiyekubali kushindwa si mshindani. Tulishindwa na timu ambazo zilijiandaa vizuri kutupita sisi, lakini tulijiandaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano wa timu ya table tennis. Ilikuwa na wachezaji wanne; watoto wa kike wawili na watoto wa kiume wawili, wazuri sana. Wamefanya mazoezi hapa nyumbani, tukawapeleka China ambako kuna mabingwa wazuri sana wa table tennis, wamekaa China kufanya mazoezi kwa siku 80. Jamani kama Serikali tufanye nini zaidi ya hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewapeleka wameenda wamerudi, wameenda huko Australia; na watoto hawa wamecheza vizuri wameenda round ya kwanza, ya pili, round ya tatu ndiyo wameondolewa. Tusiwalaumu, tusiwakatishe tamaa kwa kauli zinazotoka kwenye hili Bunge kwamba tulipeleka vilaza kule. Hapana ni vijana waliokuwa wameandaliwa vizuri kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na mwanariadha mmoja wa mbio, Ally Gullam nafikiri kutoka Zanzibar, ambaye mbali na mazoezi hapa nchini ilibidi tumpeleke Brunei kwenda kufanya mazoezi ya ziada chini ya mwanariadha maarufu nchini hapa Suleiman Nyambui. Suleiman Nyambui sasa hivi ni kocha wa Taifa wa riadha wa hilo taifa la Brunei. Kafanya mazoezi huko, kijana wetu amejitahidi ameshindwa. Nina uhakika tutaendelea kufanya hivyo huyu bwana mdogo hatimaye atashinda, practice makes perfect. Tutaendelea kufanya mazoezi, atashinda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanariadha wetu wa mbio za marathon, bwana Said Makula nafikiri wote mlimuangalia. Mimi nilikuwa naangalia sana pale amekuwa wa tatu mpaka kilometa 41 marathon, tumepata sasa na sisi bronze, akaanguka. Amemaliza kilometa 41, kabakiza tu kilometa 42.2 akaanguka bahati mbaya. Akakimbizwa hospitali kuangalia oxygen ilikuwa imepungua kichwani.

Hakuanguka peke yake, walianguka wengi wa Ireland na kadhalika kutokana na attitude ya sehemu hiyo. Kwa hiyo, ni kijana alijitahidi, tulikuwa tuwe namba tatu pale lakini sijui shetani gani aliingia pale, basi kijana wetu akaanguka akakimbizwa hospitali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwingine Kassim Mbwana aliyekuwa tegemeo letu kubwa sana kwenye boxing na alisema anaahidi kwamba akifika atatuletea gold. Amefika kule bahati mbaya sana wenzake wote waliokwenda kule Kenya, Uganda na South Africa wakapewa wapiganaji wa ajabu ajabu huko; yeye peke yake mchezo wa kwanza akapewa apambane na bingwa wa Commonwealth ambaye alipata dhahabu mchezo uliopita na huyo kijana ana silver ya Olympic, ni bingwa kutoka India.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wakasema ni maafa wengine wakaanza kusema jitoe wewe cheza cheza kidogo tu ukimbie lakini yule kijana amecheza mpaka round ya mwisho, ametolewa kwa point za Majaji. Yule mshindi amepata Majaji watatu wa kwetu amepata Majaji wawili. Anastahili pongezi za hili Bunge badala ya kuwakatisha tamaa hawa vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kwa sababu wamelalamika sana Waheshimiwa Wabunge, naomba niseme zaidi hapo. Hata soka la Tanzania linapanda, soka linapanda. Mimi naona kabisa kuna maendeleo makubwa. Msisahau Serengeti Boys mwaka jana ilituinua kwenye viti hapa Watanzania, ilifuta mkosi wa nchi hii, miaka 37 hatuendi hata semifinals za AFCON. Hawa vijana wameenda fainali za AFCON mwaka jana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu angalia dozi wanayotoa kwa timu, sita bila, Serengeti hao; sasa hivi ni mafanikio tu. Kwa kweli tuwape nguvu hawa vijana; kwa sababu tumegundua kwamba kufanikiwa katika michezo ni mazoezi na kuwekeza. Hakuna tena kwenda sijui wapi mkachezeshwe usiku na hirizi, hamna. Ni mazoezi tu na ndio maana tunafanikiwa vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimbie tu kueleza vile vile kwamba pengine Wizara mwaka huu itaongeza zaidi kampeni ya kuelezea mafanikio yetu. Kwa mfano mwaka jana tulifanya vizuri sana, katika riadha. Ukimwacha mwanariadha wetu huyu Simbu ambaye alipata medali ya shaba London Marathon mwaka jana, lakini tulikuwa na kijana ambaye nimeona ni-note hapa niwaeleze Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana kuna kijana anaitwa Cecilia Panga, ambaye Beijing International Marathon alipata gold medal. Ni binti, sawa yupo jeshini lakini ndiye aliyetuletea Tanzania hiyo gold medal. Kuna binti mwingine Madgalena Shauri alikuwa wa tano Hamburg Marathon ambayo ilihusisha wakimbiaji 25,000. Ukiwa wa tano hapo lazima ushikwe mkono kusema kijana umefanya vizuri. Tulikuwa na mwingine Emmanuel Giliki Gesamuda alipata gold medal Shanghai International Marathon.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushindi wote huu tunapata lakini huwa tunakaa kimya, safari hii sikai kimya itabidi tu tupige sound sana hapa tunapopata mafanikio yoyote. Hii ni kwa sababu tukikaa kimya tutaonekana kwamba hakuna kinachofanyika, mengi yanafanyika na yote ni juhudi ya Serikali si kama, kuna Mheshimiwa Mbunge mmoja anasema kwamba hiyo ni juhudi binafsi, hapana. Juhudi binafsi gani, Serikali ndio ina-create hiyo enabling environment tunafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa kuna hoja ya kufufua vyuo vya michezo nchini ili viweze kuendelea kutoa mafunzo kwa Walimu wa michezo. Vyuo vya Ualimu vya shahada na stahada ya elimu ya michezo na sanaa vipo chini ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Ninaomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, tunaongea vizuri sana na Wizara ya Elimu na Mheshimiwa Waziri kuhusu kuvirejesha angalau tuanze polepole baadhi ya vyuo sasa viendelee na ile mitaala ya nyuma ya michezo na sanaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Elimu kwa kuwa very proactive na tayari tumeshakaa mara ya kwanza, wanaendelea wataalam wetu kuliangalia hili suala kwa undani. Wizara ya Habari sisi tuna chuo pekee cha Maendeleo ya Michezo, Malya kinachotoa stashahada ya michezo katika nyanja za uongozi na utawala katika michezo, elimu ya ufundishaji michezo na elimu kwa michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tu Mheshimiwa Waziri wa Elimu aliposikia ametajwa kuhusu chuo hiki ambacho wala hakisimamii, lakini tayari amesema kuna umuhimu sana watendaji wetu wakae chini waangalie hiki chuo kama Wizara ya Elimu nayo ifanye nini. Kwa hiyo, yote haya ni maendeleo makubwa na nina uhakika tutafika mbali sana katika ushirikiano huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na hoja nyingine, iliyotolewa na Mheshimiwa Silafu Maufi kwamba kwa nini bajeti ya Wizara imeshuka sana na vilevile Kamati yangu ya Bunge nayo imeongelea hivyo hivyo. Naomba niseme hapana. Nafikiri pengine ilikuwa ni makosa tu ya kuandika kwa sababu Kamati hii ya Kudumu ya Bunge imenisaidia sana, imeisaidia sana Wizara kupata bajeti kubwa zaidi. Bajeti ya Wizara kwa mwaka wa fedha wa 2018/2019 ni shilingi bilioni 33.35 ikilinganishwa na ya mwaka jana iliyokuwa shilingi bilioni 28.21, ni ongezeko kubwa, ongezeko la asilimia kumi na nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lilikuwepo suala pia ambalo ameuliza Mheshimiwa Maufi kwamba sababu za bajeti ya mishahara ya Wizara kupungua. Nimewaelezea kwa kirefu kwenye hotuba yangu ukurasa wa 14 kwamba sababu ni kuhama kwa Idara ya Maendeleo ya Vijana kwenda Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado watu wengi wanadhani Idara ya Vijana ipo Wizara ya Habari, hapana imeenda Ofisi ya Waziri Mkuu. Kutokana na kuhama kwa ile idara ambayo ilikuwa kubwa ndiyo maana kumetokea kitu kama hicho. Vile vile kuna mambo mengine pia ya vyeti feki na wengi wametoka kwa hiyo lazima mishahara itaonesha upungufu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chaneli ya Bunge ionekane mubashara kwenye chaneli zote. Hii hoja ni ya Mheshimiwa Devotha Minja na imeungwa mkono na Waheshimiwa Wabunge wengi tu, lakini kwa ajili ya muda nashindwa kupanga majina sasa hivi hapa. Ningeomba tu nisisitize kwamba wahusika wa hii Chaneli ya Bunge ni Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na nina uhakika anayehusika zaidi hapa ni Spika si mimi, kwa sababu ndio anayesimamia hiyo chaneli, ni ya kwake, ni ya Bunge la Jamhuri ya Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini Mbunge akihoji kukosoa Serikali baadhi ya taarifa zinahaririwa na kutoonekana kwenye chaneli hiyo wakati zinaonekana kwenye hansard. Lah! Hii ni tuhuma nzito sana Mheshimiwa Devotha Minja, hili haliko kwangu, vile vile bado linaelekezwa kwa Mheshimiwa Spika ninyi ndio mwenye hansard na hiyo Chaneli ya Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini magazeti yanasajiliwa upya kila mwaka. Nataka niseme tu kwa kifupi sana kwamba chini ya Sheria mpya ya Magazeti, Sheria ya Huduma za Habari Na. 12 ya mwaka 2016, kwa kweli magazeti husajiliwa mara moja tu na kupewa leseni ya uchapishaji kila mwaka. Pengine alikuwa ana maana hiyo kwamba leseni ya uchapishaji kwa nini iwe kila mwaka. Sheria hii ilipitishwa na Bunge hili Tukufu kwa lengo la kuimarisha sekta ya habari na kuondoa ubabaishaji uliokuwepo. Kuna watu walikuwa wanakaa tu na vichwa vya majina ya magazeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilibidi Mkurugenzi wa Maelezo mwaka jana afute vichwa vya magazeti 200, vimekaa tu ooh “Mwakyembe Leo” sijui ‘Devotha Kesho” yaani jina tu la gazeti liko pale wakati halina kazi. Ndiyo maana tunasema kwamba kuonyesha upo live na uko serious, si kwamba inatokea opportunity imetokea sasa nafasi uanze kuandika mambo yako kumshambulia mtu ndio unaanzisha hilo gazeti, unaanza kulifanyia kazi. Ndio maana tukasema hapana kama upo serious basi hata kama ada ni ndogo lakini kila mwaka ulipe, lakini leseni unabaki nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba kwa nini vyombo vya habari vinavyokosoa Serikali vinafungiwa, Serikali ingalie upya suala la kufungia magazeti. Ukweli kwa heshima na taadhima, hili suala limeulizwa vilevile na Mheshimiwa Lucy Owenya na Mheshimiwa Aida Joseph Khenani. Sheria ya Huduma za Habari imeeleza wazi makosa yanayostahili kupewa adhabu iwapo vyombo vya habari vitakiuka sheria hiyo. Vyombo vya habari vinavyofungiwa vimekiuka sheria na ni pale ambapo suala la usalama wa nchi limeguswa. Hata Dkt. Ally Yusuph anasema Serikali isifungie magazeti na redio, Waziri avilee vyombo vya habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemwelewa. Nataka nimweleze kwamba tunawalea vizuri waandishi wa habari kwa sababu hatujawahi hata siku moja kuchukua hatua bila kukaa na vyombo vya habari mara tano, sita, saba; ndugu zetu angalieni hiki sio sahihi. Kulikuwepo na aina fulani ya fikra katika nchi yetu kwamba uhuru unaweza ukawa usiwe na mipaka. Sasa hao tunaona sasa wamezidi kiasi lazima sasa tuwafundishe kwa kuwafungia kwa muda na wengi wanaporudi wanaenda vizuri tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ni kulea vile vile tunapeleka waandishi wa habari nje ya nchi kwenda kusoma. Kwa mfano mwaka jana tumepeleka vijana 10 China waandishi wa habari, wawili kutoka Serikali na wanane kutoka private media, kwenye hilo hatufanyi kabisa upendeleo. Mwaka huu tumeshapata nafasi za masomo China na Sweden na nawahakikishia tutakuwa na waandishi wa habari wa vyombo binafsi wengi zaidi kupita wa Serikali kwa sababu wote wanatimiza lengo kubwa la kikatiba la kuhabarisha umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Devotha Minja vile vile na Mheshimiwa Lucy Owenya wanasema kwa nini Serikali haitoi tamko pale waandishi wanapotekwa na wengine kupotea. Lah! Sasa Mheshimiwa Minja ananipa mtihani mgumu sana na ametoa mfano kwa mfano mwandishi wa Guardian.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ushauri kwa mfano huu alioutoa wa mwandishi wa Guardian; hebu naomba yeye mwenyewe aulizie vizuri alikuwa wapi maana nisingependa mimi kuwa sasa chanzo cha kuharibia majina watu hapa. Yeye mwenyewe aulizie alikuwa wapi, atapata majibu tu huko Guardian maana yupo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana tumefika kipindi ambacho kuna watu wengine wanajiteka wenyewe. Sasa mimi Waziri mzima nikakurupuka kutoa statement wakati suala lenyewe ni la jinai linahusu polisi, nafikiri polisi wakishapeleleza basi na sisi tunaweza tukatoa kauli. Tunaheshimu na kuthamini sana waandishi wetu, mchango wao ni mkubwa katika maendeleo ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa George Lubeleje, anasema Serikali ina mpango gani wa kuboresha maslahi ya wafanyakazi wa TBC na Maafisa Habari wa Idara ya Habari Maelezo. Mheshimiwa Lubeleje, kaka yangu namheshimu sana, namshukuru sana kwa mapenzi makubwa aliyonayo kwa waandishi wa habari wa TBC na wengine wa Idara ya Habari Maelezo. Nadhani tuwe wakweli; watumishi wa Idara ya Habari Maelezo, watumishi wa TBC, hawa ni waajiriwa wa Serikali ambao maslahi yao huboreshwa sambamba na watumishi wengine wa Serikali. Mimi sioni kama wana matatizo makubwa hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwe mkweli na nilishashutumiwa sana katika Bunge hili kwa kusema ukweli, kwamba watu ambao ni wa kuwaonea huruma ni waandishi wa habari ambao wako kwenye vyombo binafsi. Kuna waandishi wanapata, si kima cha chini, ni chini ya kima cha chini cha mshahara, ni mishahara ya kitumwa wanayopewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili, mwandishi wa habari abishe aende nyumbani kwake mke wake atamkuta amekasirika kwa sababu nyumbani hajaacha kitu. Hakuna mkataba wa kazi, vijana wangu wanachezewa sana, hawawekewi bima, hakuna kuwekewa pesa kwenye Mifuko ya Jamii; ndiyo maana sheria hii mpya, nawaomba waandishi wa habari jitokezeni mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachoogopa sisi tukiunda Media Council hapa watasema ni ya kwetu Serikali; waunde Media Council yao tutawasaidia. Chini ya sheria hii wana uhakika wa kuwa na ajira inayowalinda wao wenyewe. Waandishi wa habari wengi hawaelewi wanapiga kelele ya wamiliki, ndiyo shida hiyo tuliyonayo. Nashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lijualikali anasema kuna ubaguzi mkubwa katika kutoa adhabu katika baadhi ya magazeti, magazeti mengine yanafungiwa. Kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari, kama nilivyosema, kuna namna mbili za utoaji wa adhabu; kama kosa linaathiri usalama wa Taifa kwa kuihusisha Serikali au viongozi wa kitaifa ambao hawawezi kujitetea, Waziri anaweza kutumia kifungu cha 59 cha sheria dhidi ya gazeti husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ni mtu binafsi, akidhalilishwa na gazeti hiyo ni kesi ya kudhalilishwa, ni kesi ya defamation, anaweza kulalamika Idara ya Habari Maelezo ili hatua za kimaadili zichukuliwe, lakini vile vile anaweza kabisa kwenda mahakamani kupitia kifungu cha 41 cha sheria kudai fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa si Maelezo wala Wizara ambayo imepokea malalamiko rasmi ya viongozi au mtu yeyote kunyanyaswa na gazeti tusichukue hatua. Tulipata kesi moja ya gazeti moja linasemwa sana hapa, tuliwaita Wahariri, tumewaandikia onyo la mwisho lakini haikuwa onyo kwamba wametishia kitu chochote, walimchafua mwenzao kwamba utapelekwa mahakamani na hii ni kinyume cha maadili; huo wajibu tunaufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usikivu wa TBC Nkasi Kusini, kandokando ya Ziwa Nyasa; namwomba Mheshimiwa Desderius John Mipata kuwa ndugu yangu akae mkao wa usikivu mzuri tu kwa sababu katika bajeti tuliyoweka sasa hivi tunaweka transmitter mpya Mbeya, transmitter mpya Dodoma, lakini vilevile namhakikishia kwamba katika bajeti hii inayokuja eneo lake pia lipo kati ya maeneo ambayo tumeyapa kipaumbele, ikiwemo Zanzibar na Simiyu vilevile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usikivu wa Redio Zanzibar, Mheshimiwa Machano Othman; kama nilivyosema katika bajeti ya mwaka huu ambayo naomba aipitishe leo Mheshimiwa Machano Othman, tuna Zanzibar, Songwe, Simiyu, Njombe, Katavi kuweza kuyafikia na nina uhakika tutayafikia. Tumeshapata uzoefu wa maeneo tuliyopitia sasa hivi; Rombo, Kibondo, Nyasa, Longido na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kusajiliwa na kulipwa tozo kwa blogu; Mheshimiwa Devota amelalamikia kuhusu suala la kulipa tozo kwa blogu mbalimbali kwamba tunaonea; lakini si yeye tu, Waheshimiwa Wabunge wengi wamelalamikia sana hizi kanuni mpya tulizozitoa. Nataka nitoe taarifa tu kwamba wakati humu sisi tunaongea, taarifa nimeipata dakika kumi zilizopita kwamba usajili wa watoa huduma za maudhui mtandaoni, maombi tuliyopokea mpaka sasa ni 86 na tumesha-approve moja ambayo vigezo vyote vimekamilika. Wengine wanaendelea kusaidiwa, kuelekezwa ili warekebishe karatasi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tumechukua hatua hiyo? Waheshimiwa Wabunge naomba kwa sababu ninyi ndio wawakilishi wa wananchi, vyombo hivi sasa duniani vinabeba nafasi sawa na vyombo rasmi vya habari katika kuhabarisha. Nina uhakika ndani ya mwaka mmoja, miwili,
mitatu ijayo, vitakuwa vyombo vikubwa zaidi vya kuhabarisha kuliko hata vyombo rasmi tulivyonavyo kama TV, magazeti na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wetu Tanzania vyombo hivi; blogu, majukwaa mitandaoni, redio na TV mtandaoni vimeanza pole pole kuwa vyombo muhimu na vikubwa vya kuhabarisha na kuhabarishana na kutaarifu na kutaarifiana. Leo hii itisha press conference Mheshimiwa Mbunge, vyombo vitakavyokuwa mbele yako pale, vyombo rasmi vitakuwa vinne, lakini utashangaa microphones mara nne ya pale au mara tatu, mara mbili ni vyombo hivi vya kimtandao. Vimeanza kuwa ni vikubwa, vimeanza kuwa ni muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ni kwamba tofauti na wenzao wale wachache, hawana utambulisho rasmi kuwa ni wanahabari, hilo la kwanza. Hawana miiko wala masharti rasmi ya kazi, wao ilimradi kimetoka, wapo pale wanachukua habari. Hawabanwi na maadili yoyote katika kazi wanayofanya; hawalipi kodi pamoja na kwamba wanashindana na vyombo rasmi vinavyolipa kodi kugombea matangazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani, tuwe fair, let us be fair. Tunachokifanya sisi sio peke yetu, tumefanya utafiti nchi nyingi zimefanya hivyo na lazima tuwahi, tusije tukajikuta tumetengeneza dude kubwa likatushinda mbele ya safari. Watu wengi siku hizi ndugu zangu, si Tanzania tu, wanaweza akakaa siku moja, mbili, tatu, hata wiki nzima hajasoma gazeti wala hajaangalia TV, yeye yuko bize na twitter, anaangalia tu kuna nini kwenye instagram, kuna nini kwenye mitandao, inamtosha, imemhabarisha, sasa hivi ndiyo imeendelea hiyo trend sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi vyombo vina changamoto kubwa vile vile, vimekuwa sasa mainstream katika kuhabarisha umma, lazima viwe na maadili, viwe na miiko. Sababu, tatizo kubwa la vyombo vya mitandaoni ni fake news, kama wanavyosema Wamarekani, ni taarifa za
upotoshaji, za uongo, kwa sababu hao watu wamechukua, ni kikundi tu cha kuongea, unaongea unachotaka, lakini kuna watu wanachukulia kwa nguvu sana kwamba ni ukweli. Kuna nchi zimekaribia kwenda vitani kwa ajili ya taarifa fake, taarifa za uongo katika vyombo hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu, na kwa mujibu wa taarifa ya mwaka 2017 ya Freedom House, wote mnaijua hiyo; ni chombo cha wanaharakati wa kidemokrasia, wanasema asilimia 75 ya nchi duniani zote zimechukua hatua kudhibiti maudhui katika mitandao; lazima zidhibiti. Wao wanasema wanalinda watoto, sisi ndio hatuna watoto? Nasi tuna watoto. Kwa hiyo na sisi tumesukumwa na sababu hizo hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu nyingine upande wa Tanzania ni hitaji la wanahabari mitandaoni kutaka nao watambuliwe kama wanahabari. Imetokea wakati amekuja Rais wa FIFA hapa, Infantino, anataka waandishi wa habari 20 tu wenye press cards, hawa hawana. Wakasema, Waziri tunataka na sisi tutambuliwe, tukasema lakini ninyi sijui ni watu gani, sijui na ninyi ni waandishi, nao wanataka watambuliwe kama ni formal media institutions. Sasa tulichokifanya ni hicho, ni kuwaweka nao kuwa wanatambuliwa kama wanahabari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukisoma taarifa ya Reporters Without Borders, nao ni wanaharakati wa demokrasia hawa, wanataja nchi nyingi ambazo zimeweka masharti katika kutumia mitandao. Nchi nyingi ambazo ni kongwe kidemokrasia zimo humo; Marekani, Australia, Uingereza, Canada, India na kadhalika, ambao hoja yao kuu ni kuwalinda watoto. Sasa sisi hatuna watoto jamani, sisi ndio hatuna watoto?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata sisi Tanzania tuna wajibu wa kuweka mazingira ya matumizi salama ya mitandao ama sivyo, kama nilivyosema kwenye kitabu changu, ukurasa wa 64, teknolojia badala ya kuitumia, itatutumia na ni madhara makubwa sana mbele ya safari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu vyombo hivi vinafanya kazi ya Kikatiba ndiyo maana kwa kweli tumesema tuchukue hatua. hivyo basi, kanuni zetu zinatambua kazi yao, hawa wenzetu wa blogu na kadhalika na zinawaingiza kwenye mfumo ule ule wa maadili wa vyombo vingine vya habari na kama kuna tatizo tuongee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye mitandao ni kwamba tunawatoza dola 925 kwa mwaka, hapana, kiingilio ni shilingi laki moja. Sema muda sina, lakini naweza kuonesha tunavyowatoza wale wenye vyombo vyenyewe vilivyokaa, wao tunawatoza shilingi laki moja, lakini vyombo rasmi tunavitoza, kama TV kweli iko pale, ni dola 5,000, hawa laki moja, wengine dola 5,000. Sasa tufike tu-argue lakini tukiwa na facts tayari. Baadaye nikiulizwa nitatoa, ninazo hizo figures tayari lakini nikizitoa sasa hivi nitatumia muda mrefu mno na nafikiri sasa hivi nitapigiwa kengele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naambiwa fungiafungia kwa wasanii, msanii mzuri, anafanya kazi nzuri, akikosea mnamfungia. Mimi nashindwa kuelewa, hivi tungefungia wasanii 20, nafikiri hii nchi ingepasuka. Sisi ni walezi, kama wenzetu ni walezi ninyi ndani ya nyumba, mtoto anakosea unamuimbia nyimbo kumsifu, sisi wengine ni walezi ambao mtoto akikosea lazima ajue kwamba kuna adhabu. Kwa sababu wengine wataendelea kufanya hivyo na hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ameeleza vizuri Mheshimiwa Naibu Waziri hapa; tuna utaratibu mzuri sana kisheria, usitoe wimbo wowote bila kwanza kupata opinion, ushauri wa BASATA, BASATA ni walezi; hakuna anayefanya. Nchi hii imezoea, utii wa sheria bila shuruti ni kitu cha ajabu, siku hizi imekuwa yaani lazima mtu afanye anavyotaka. Sasa tukiingia kwenye sheria maneno yanaweza kuwa mengi sana. Hakuna mtu tuliyemfungia tukasema wewe sasa sio msanii tena, tunataka vijana waelewe wana wajibu kwa hii jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mheshimiwa Amina Mollel ameeleza hapa, jana amenionesha picha ya ajabu sana inazunguka kwenye mitandao. Wako kwenye steji jamaa anatoza pesa nyingi, laki mbili watu kuingia mle ndani lakini mule wanaitwa watu wasimame wavue nguo, mengine siwezi kusema, hii ni TV, lakini hayo mambo hatuwezi kukubali nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuja hapa na kitu very controversial tunakifanyia utafiti ndani ya Wizara yangu. Wenye pesa Ulaya wengi ni mashoga, wameanzisha foundations, yametawanywa kila nchi Afrika. Sasa hivi Tanzania tumekuwa earmarked kama kitovu kizuri cha kuwa ndiyo centre ya huduma za mashoga katika Bara la Afrika, hatuwezi kukubali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upuuzi huu upitie kwenye mitandao, usipitie kwenye mitandao sisi tutadhibiti; wakubwa wakasirike, wasikasirike, hili ni Taifa letu lina maadili yake na utamaduni wake. Mwalimu alisema; sitasahau hilo; Taifa lisilo na utamaduni wake ni taifa mfu na sisi sio taifa mfu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la visimbuzi, imetoka kwa Mheshimiwa Chumi, kwamba ni kwa nini havioneshi hizi TV stations zetu tano, sita, saba ambazo ni Free to Air. Hili suala liko Mahakamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa harakaharaka, naona kengele ya kwanza imelia. Mheshimiwa Shekilindi amesema Serikali iwasimamie wasanii wasidhulumiwe. Kwa kweli dhuluma ilikuwepo kubwa sana kwa kutumia middlemen, watu wenye pesa wamewachezea sana wasanii wetu Tanzania. Hili limeanza kubadilika, tumeanza kuwa-empower wasanii wetu kwa kutumia TEHAMA, wasitumie middlemen.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba msome kitabu change nimeeleza vizuri njia tulizotumia, lakini wachukulie vijana wazuri kama akina marehemu Kanumba, amefariki Kanumba kila mtu anajua ni milionea, hapana, waliotajirika ni wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii mwanasanaa mzuri mzee Majuto anaumwa, anaomba pesa mimi nachanga kutoka mfukoni. Leo hii nusu ya mabango ya biashara ni ya Majuto, matangazo ya biashara kwenye TV ni Majuto. Naomba sasa nitumie nafasi hii kusema nimeunda Kamati ya Wanasheria, tunaanza na kesi ya mzee Majuto. Mashirika yote, kampuni zote zilizoingia mkataba na Majuto tutapitia hiyo mikataba kama ameonewa lazima ilipwe familia yake; tumeshachoka. Tukishamaliza Majuto tutarudi kwa Kanumba, na msanii yeyote ambaye anaona aliingia mkataba wa kipumbavu aje atuone. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaudhi lakini ndiyo hivyo. Leo mzee yuko hospitali anakosa shilingi laki tano, mimi Waziri nitume, pesa yenyewe ndiyo hiyo mnaelewa maisha yalivyo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja tu nitakalolaumiwa na wananchi, kwamba Mheshimiwa Amina Mollel amesema kuna Mtanzania aliyetoroka kambi. Ni kweli kabisa, tumepata aibu, kati ya vijana wetu waliokwenda Australia kwenye mashindano ya Commonwealth mmoja amejongo huko, amepotea huko, hakurudi na jina lake kweli kama alivyosema Mheshimiwa Amina Mollel, ni Fatihiya Hassan Pazi wa Ukonga, Dar es Salaam, ambaye alikuwa mmoja wa wachezaji wetu wa table tennis, mzuri sana katika table tennis.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulimpeleka China kama nilivyosema siku themanini kuimarisha kazi yake na walifanya kazi nzuri sana, baada ya kumaliza mchezo tarehe 11, Aprili, tarehe 12 hakuonekana. Kiongozi wetu, Dkt. Singo ambaye alikuwa nao alijua kabisa huyu hajapata ajali maana alikuwa ametoatoa nguo zake zote safi akaacha tu traksuti mle ndani, na vile vile jana yake alikuwa amenunua pia na sim card ya kule, kwa hiyo ilikuwa ni maandalizi tu ya kupotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini alivyokwenda polisi kuripoti akakutana na wenzetu wa Kenya wakisema nao wawili wamepotea; Uganda nao wawili wamepotea. Aliyekuja ameinamisha shingo kabisa alikuwa ni mtu kutoka Cameroon, wanane walikuwa wameondoka kwenye kambi yake. Tumesharipoti hili suala mambo ya nje na uhamiaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.