Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Waziri pamoja na team yake yote kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Lushoto ni eneo lenye milima na mabonde mengi na kwa hiyo tuliomba mnara kwa ajili ya kupata matangazo ya Redio ya Taifa yaani TBC. Hivyo basi tunaomba mnara huo ujengwe haraka. Pamoja na kwamba Serikali imetuahidi kutujengea mnara katika maeneo ya Kwebusani katika Kijiji cha Kwemashai, na tuliambiwa ujenzi huo umeanza lakini mpaka sasa bado ujenzi huo haujaanza. Naomba tufanyiwe haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiofichika kwamba kuna vijana wengi sana ambao wana vipaji mbalimbali hasa katika michezo, sanaa na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Lushoto ina vijana wengi ambao ni wachezaji wa mpira wa miguu. Cha kusikitisha vipaji vya vijana vinapotea bure na Serikali kupoteza nguvu kazi ya vijana hao. Hivyo basi niiombe Serikali ijenge chuo cha michezo katika Wilaya ya Lushoto pamoja na kiwanja hata kimoja tu. Sambamba na hilo kuna hawa vijana ambao ni wanasanaa na utamaduni. Lushoto ni Wilaya ambayo imebarikiwa kwa vipaji mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu Tukufu itume wataalam kwenda vijijini na wilayani kwa nia ya kwenda kuwabaini vijana wenye vipaji na kuwapa au kuwajengea uwezo ili waweze kutoka vijijini na kuwaleta mjini na kuwapa msaada ili nao waweze kujiajiri. Kama inavyojulikana kuwa michezo ni ajira, kwa hiyo tukiwasaidia vijana hawa Serikali itakuwa imepunguza asilimia kubwa sana ya tatizo la ajira hasa kwa vijana wetu hawa wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali kuwekeza katika michezo kuanzia shule za msingi hasa kwa kupeleka vifaa vya michezo katika shule zetu. Sambamba na hayo niiombe Serikali itoe VAT katika vifaa vya michezo ili vijana wetu waweze kumudu gharama za kununua vifaa hivyo vya michezo, kwa sababu ukizingatia Tanzania imeamka sana katika tasnia hii ya sanaa na michezo. Ni imani yangu kubwa kuwa tukiwatumia vizuri wasanii wetu hawa tutakuwa tunaingiza pesa nyingi hasa kwa kuwatumia kutangaza utaliii wetu nje na ndani ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niiombe Serikali kuwasimamia wasanii wetu ili wasidhulumiwe na matajiri ambao hawana nia nzuri na wasanii wetu. Msisitizo, tunaomba mnara wa Lushoto ufanyiwe bidii ili uweze kuisha haraka kwa sababu tumechoka kusikiliza redio za Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.