Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Prof. Makame Mnyaa Mbarawa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkoani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

WAZIRI WA UJENZI, UCHUKUZI NA MAWASILIANO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia tena hapa leo kuendelea na kikao chetu hiki na mimi kupata fursa ya kuchangia au kutoa mchango wangu kwenye hoja iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nimshukuru Mheshimiwa Spika wewe mwenyewe na Wenyeviti wote wa Bunge kwa uwezo na umahiri mkubwa mnaoonesha katika kuliendesha Bunge letu. Nachukua fursa hii kumpongeza kwa dhati Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu kwa umakini wake kwa kusimamia shughuli za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, napenda nimshukuru sana au niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote waliopata fursa ya kuchangia hoja yangu niliyowasilisha hapa Bungeni kwa michango yao mizuri na yenye lengo la kuboresha utekelezaji wa majukumu ya Wizara yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingi zimetolewa na hii ni dalili ya dhati inayoonesha kwamba Waheshimiwa Wabunge wana maono makubwa kwenye kuendeleza Sekta hii ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ili sekta hizi ziweze kuchangia katika maendeleo ya nchi yetu. Aidha, katika michango yao, imedhihirika wazi juu ya mahitaji makubwa ya miundombinu bora na ya kisasa kwenye huduma za usafiri wa anga, nchi kavu na majini ambazo ni muhimu sana kwa nchi yetu katika uchumi wa viwanda na uchumi wa kati ufikapo mwaka 2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba yangu imechangiwa na wachangiaji wengi ambapo wachangiaji 82 wamechangia kwa maandishi na 100 wamechangia kwa kuzungumza. Michango ya Waheshimiwa Wabunge wote ilikuwa mizuri sana na iliyosheheni mapendekezo, ushauri na busara namna bora ya kuendeleza sekta hizi za ujenzi, uchukuzi na mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, siyo rahisi kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge wote kwa kina na kutosheleza kwa muda huu mfupi nilionao ninaahidi kwamba hoja zote tutazijibu kwa maandishi na kuwapatia Waheshimiwa Wabunge wote majibu ya hoja hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri na Kamati ya Bunge ya Miundombinu umezingatiwa, hivyo napenda nitumie muda huu mfupi nilionao kutoa ufafanuzi kwa baadhi ya hoja tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, michango yangu itajikita kwenye sehemu tatu; kwanza, kwenye Sekta ya Anga, Sekta ya Usafiri wa Nchi Kavu halafu Sekta ya Usafiri wa Majini.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo asubuhi kwenye kuchangia, Mheshimiwa Mlinga hapa amezungumzia kuhusu ujio wa ndege kubwa iliyokuja jana kwenye kiwanja cha Dar es Salaam, lakini yeye amezungumza Kibunge, mimi leo kwa sababu nasimamia sekta, nitazungumzia zaidi kiupande wa sekta ya anga.

Mheshimiwa Naibu Spika, jana kulikuwa na ndege ambayo ilikuwa inatoka Dubai kwenda Mauritius. Ni ndege ya Airbus 380 – 800, ndege ambayo ilkuwa ni Flight No. AK 700 01E. Ndege hii baada ya kufika kwenye kisiwa cha Madagaska walipata taarifa kwamba hali ya hewa Mauritius ni mbaya. Kwa kawaida ukipata taarifa hiyo unakwenda kwenye uwanja wa ndege ulio karibu nao.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa marubani baada ya kupima viwanja vya ndege vyote vilivyopo karibu, ukiwa Madagascar kiwanja chake cha kwanza cha karibu inakuwa ni Madagascar wenyewe, cha pili pale ni Zimbabwe. Zimbabwe pale kuna Mozambique, vilevile kuna Namibia kuna South Africa. Baada ya kuangalia yote wakaamua waje watue kiwanja cha ndege cha Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndege hii inachukua abiria 868, ni ndege kubwa duniani. Kwa jana ilikuwa na abiria 503. Ndege ile ilikuja Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam na ikatua vizuri na historia katika nchi yetu ama nchi nyingi za Afrika kutua Airbus 380; kwa niaba ya Serikali kwanza nawashukuru sana wafanyakazi wa kiwanja cha ndege cha JNIA, wafanyakazi wa TCA kwa kazi nzuri waliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii haikuja bure, isipokuwa sasa ulimwengu unatambua kwamba viwanja vyetu vya ndege hasa vya kimataifa ina vigezo vya kisasa, vigezo bora na vigezo vya kimataifa. Vinginevyo kama ingekuwa hatuna vigezo hivyo, ndege ile isingekuja Dar es Salaam na wafanyakazi walifanya kazi kubwa kwa sababu kipindi cha saa saba mpaka saa 11 inakuwa ni peak hours, panajaa sana pale, lakini wafanyakazi wale walifanya vizuri, immigration ilifanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawapongeza sana kwa kazi hii nzuri, tuendelee kushirikiana ili tuhakikishe kwamba tunajenga sekta hizi kwa maslahi ya Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niende kwenye sekta moja kwa moja. Kama tunavyojua, mwaka 2017/2018 tulipata takribani abiria milioni 4,950 waliotumia usafiri wa anga. Usafiri wa anga ni muhimu sana kwanza kwenye sekta yenyewe ya anga, pili kwenye sekta ya biashara na tatu, sekta ya utalii. Sekta ya utalii kwenye usafiri wa anga ni muhimu sana. Ndege hizi zikija Tanzania zinachukua Watanzania, ama zinasafirisha Watanzania, lakini pia tunasafirisha watalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya utalii ni sekta ambayo inachangia sana kwenye pesa za kigeni na ni sekta ambayo inachangia sana ajira hapa Tanzania. Kwa vile ni dhamira ya Serikali na sekta yetu kuhakikisha kwamba tunatoa huduma kwenye usafiri wa anga, lakini wakati huo huo tunahakikisha kwamba sekta ya utalii tunaiboresha zaidi. Kwa kuangalia hivyo, kuna baadhi ya maeneo ya nchi yetu bado sekta ya utalii haijaendelea sana, kwa mfano, upande wa nyanda za juu, tuna mbuga nzuri za wanyama lakini watalii bado kule hawajawa wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye kanda ya Magharibi kule, tuna Game Reserve nzuri sana. Kwa mfano tuna ile tunaita BBK, Biharamulo Game Reserve, tuna Burigi Game Reserve, tuna Ibada Game Reserve na nyinginezo, lakini bado watalii wengi wameshindwa kwenda kwa sababu kule hakuna viwanja vya ndege au barabara nzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kulijua hilo, sasa tumekuja na mpango mkakati ambapo kila kwenye maeneo haya ya uvutiaji wa utalii tutajenga kiwanja cha ndege, tutajenga barabara na ndiyo mmeona sasa mwaka huu tumepanga pesa kwa ajili ya kiwanja cha ndege cha Iringa pamoja na barabara yenyewe ya kutoka Iringa mpaka Ruaha National Park, tunaijenga kwa kiwango cha lami barabara yenye urefu wa kilometa 104. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo tunajenga Kiwanja cha Geita ili kuhakikisha sasa tunatoa au tunakuza sekta ya utalii hasa kwenye Kanda ya Magharibi. Ili kuhakikisha kwamba anga letu liko salama, Serikali kupitia TCA tumeamua kununua rada nne za kisasa kwa ajili ya ndege za abiria. Rada hizo zitagharimu takriban shilingi bilioni 67.3, rada hizo zitajengwa moja pale Dar es Salaam JNIA; ya pili, itajengwa Songwe; ya tatu, itajengwa KIA; na ya nne, itajengwa huko Mwanza. Hatukusimamia hapo tu kwa sababu kuna baadhi ya viwanja vya ndege sasa hivi ndege zimekuwa nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Zanzibar Kiwanja cha Abeid Amani Karume traffic imekuwa kubwa. Kwa kawaida ikishafikia hatua hiyo, tunaweka vifaa vya kisasa ambavyo tunaita instrument landing system kama alivyosema Mheshimiwa Zungu juzi, kwa vile Zanzibar tunajenga vifaa hivyo na tutatumia takribani shilingi bilioni 3.6. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimezungumzia usalama wa anga yetu, tukiweka rada hizi tunazozizungumza, kwanza anga yetu kwa upande wa ndege za abiria itakuwa salama sana. Pili, kuna eneo kula ya Mashariki chini ya Pemba kule na Zanzibar, ndege zilizokuwa zinapita pale zilikuwa zinaangaliwa na anga ya Kenya. Sasa baada ya kuweka rada hizi, ndege zile tutakuwa tunaziangalia sisi wenyewe na kuziongoza sisi wenyewe na tutaweza kupata mapato yanayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, kwenye viwanja vyetu huko kwenye madini na kwenye mbuga za wanyama, kuna airport ndogo ndogo nyingi. Sasa hivi hatuna uwezo wa kuziona, lakini baada ya kukamilika rada hizi nne, tutaweza kuona anga lote Tanzania na tutaweza kuangalia mali zetu inavyostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ni kwa upande wa usalama wa anga, lakini unaweza kuwa na usalama wa anga huko mzuri lakini kama viwanja vyako haviko vizuri, hiyo siyo sahihi. Kwa kulijua hilo sasa, Serikali tumeamua kwanza kujenga jengo la abiria pale kwenye Uwanja wa Dar es Salaam, JNIA, jengo namba tatu ambalo lenyewe litakuwa na uwezo wa kuchukua abiria milioni sita kwa mwaka. Jengo lenyewe litakuwa na uwezo wa kupaki ndege 21 kwa wakati mmoja, ndege aina ya Airbus 320. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jengo la abiria namba mbili tulililonalo sasa hivi lina uwezo wa kuchukua abiria milioni mbili tu na ndiyo ukienda Dar es Salaam kuanzia saa 7.00 mpaka saa 11.00, peak hours pale watu wamejaa; lakini mwisho wa mwaka huu, jengo la abiria namba tatu likikamilika, tunaamini tatizo hilo litaisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu Mtwara tunataka kuifanya hub ya upande wa Kusini, tunapanua Uwanja wa Ndege wa Mtwara ambapo sasa ndege ya Airbus 320 inaweza kutua. Gharama ya ujenzi huo itakuwa takribani shilingi bilioni 53.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi zitakazofanyika pale ni kutanua uwanja wa ndege na kuwa na urefu wa kilometa 2.8, kujenga jengo la kuegeshea ndege, kujenga vifaa vya kuongozea ndege, pia kujenga parking kwa ajili ya magari na barabara ya kuingilia kwenye kiwanja cha ndege. Hivi tunavyozungumza, mkandarasi wa kazi hiyo tumempata ambaye ni Beijing Construction Engineering Group. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa Kiwanja cha Ndege cha Mwanza, nia ya Serikali kufanya kiwanja hiki kiwe kiwanja cha kimataifa sasa. Tunatanua Uwanja wa Ndege wa Mwanza na umefikia kilometa 3.5. Ndege kama iliyotua Dar es Salaam jana, ninaamini na Mwanza inaweza kutua yaani ndege ya Airbus 380.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Mwanza kazi zinazofanyika, tunajenga jengo la kuongozea ndege, tunajenga eneo la maegesho ya ndege, tunakarabati taa za kuongozea ndege na tunaongeza ndege kwa ajili ya ndege na kuengesha ndege za abiria, mwisho tutahakikisha kwamba tunajenga jengo la abiria. Kwa sababu huwezi kuwa na kiwanja cha ndege kizuri kama kile bila kuwa na jengo la abiria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi inayoendelea sasa hivi inagharimu takriban shilingi bilioni 85. Tuna kazi vile vile huko Sumbawanga, tunaongeza urefu wa Kiwanja cha Ndege Sumbawanga ambapo tunaongeza kiwe na urefu wa kilometa 1.75 ambapo gharama huko itatumia shilingi bilioni 55.6. Pale tunajenga jengo la abiria, tunajenga eneo la kugeuzia ndege au maegesho ya ndege. Pia tutajenga taa za kuongozea ndege na huko vilevile Mkandarasi tumeshampata. Kazi tunayofanya sasa hivi ni kulipa fidia kwa wananchi wale wanaostahili fidia kama sheria inavyoelekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafanya kazi hiyo ya kujenga uwanja wa ndege Shinyanga ambao kazi inayofanyika ni kutanua uwanja wa ndege mpaka kufikia kilomita mbili na Mkandarasi yupo na pale tutajenga jengo la abiria. Vilevile gharama ya kiwanja hicho ni shilingi bilioni 49.

Mheshimiwa Naibu Spika, huko Songwe kazi inayoendelea sasa hivi ni kujenga jengo la abiria na gharama ni shilingi bilioni 11.5, lakini tunajua kilio cha muda mrefu cha watu wa huko Songwe ambao wanahitaji taa za kuongozea ndege, kwa vile sasa hivi tumempata mkandarasi ambaye atajenga taa ama ataweka taa kwenye kiwanja kile na taa hizo zitatumika kuongoza ndege saa 24 kwa siku, siku saba kwa wiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mradi kama huo huko Musoma wa kuhakikisha na kiwanja cha Musoma sasa ndege yetu ya Bombardier inaweza kutua na Mkandarasi tayari tumeshampata, isipokuwa sasa hivi tuko kwenye mazungumzo na tunaamini kwamba hivi karibuni tutamaliza kuhakikisha kazi hiyo inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna kazi vilevile ya kujenga Kiwanja cha Ndege cha Iringa kama nilivyosema, kwa sababu nia ya Serikali sasa ni kuboresha utalii kwenye Ruaha National Park na tunajenga barabara kutoka Iringa mpaka huko kwenye park ambayo ina urefu wa kilometa 104. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya uwanja wa ndege inandelea huko mkoa wa Geita na kama nilivyosema, nia kubwa ya Serikali ni kuhakiksha sasa tunaanzisha ule utalii kwenye Kanda ya Magharibi. Kama nilivyosema, kule kuna game reserve kubwa na utalii wa kule hasa sasa hivi ni utalii wa picha ambao ni utalii umechukua nguvu sasa duniani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimezungumzia viwanja vya ndege kwa ufupi, naomba nijikite kidogo kwenye Shirika la Air Tanzania. Nia ya Serikali kama nilivyosema huwezi ukawa na viwanja vya ndege, huwezi ukawa na anga lililokuwa salama kama huna shirika lako la ndege. Kwa kulijua hilo, Serikali imenunua ndege sita ambapo ndege tatu zimefika nchini na zinafanya kazi. Mwaka huu tunategemea vilevile ndege tatu ambazo zitawasili. Ndege ya kwanza ni Boeing 787 yenye uwezo wa kuchukua abiria 262 ambapo ndege hii itakwenda masafa marefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndege nyingine mbili zenye uwezo wa kila moja kuchukua abiria 132 ni Bombardier CSeries 300 zitawasili ndege mbili hizi na tunaamini zitaanza kufanya kazi nzuri. Kwa kawaida huwezi kuwa na ndege moja ya masafa marefu na ikafanya kazi vizuri. Kwa vile kwenye bajeti hii tumeshapanga kununua ndege nyingine ya Boeing 787 ili tuwe na ndege mbili. Kwa mfano, tukiamua tunaenda Guangzhou, ndege moja inatoka Guangzhou inakuja Dar es Salaam na nyingine zinapishana, inatoka Dar es Salaam inaenda Guangzhou. Hivyo ndivyo utaratibu unavyokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, shirika letu la ndege limeanza kufanya kazi na linafanya kazi vizuri. Hivi tunavyozungumza, Shirika letu la Ndege linakwenda Dar es Salaam, hapa Dodoma na Wabunge wengi mnapanda ndege ya shirika letu la ndege, ni jambo zuri sana. Tabora, Kigoma, Mwanza, Bukoba, Kilimanjro, Zanzibar, Songwe na huko Hayahaya, Comoro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni tutaanza safari za kwenda Mpanda, Tanga, Entebe huko Uganda na Bujumbura, Burundi. Kuanzia mwaka 2017 Shirikala la Air Tanzania Julai mpaka Machi, 2018 tumeweza kusafirisha abiria 150,518 ikilinganishwa na mwaka 2017 kwa kipindi kama hicho ambacho tulisafirisha abiria 104,207. Hili ni ongezeko la asilimia 46. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kumekuwa na kuongezeka kwa mapato ghafi ambayo tumeongeza kutoka shilingi bilioni 34.4 mpaka shilingi bilioni 43.8. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja hapa Wabunge wengi walipiga kelele kwamba Shirika la Air Tanzania halina business plan. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla Air Tanzania tunazo business plan ndiyo hizi hapa tunazotumia. Naomba mhakikishe kwamba tunakwenda kwa mipango na tunayo business plan. Business plan siyo msahafu, kila baada ya muda lazima ibadilishwe, kwa vile tutaendelea kuboresha business plan yetu hii kutokana na mahitaji ya soko na mahitaji ya Watanzania na wateja wetuwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja moja ilitokea juzi hapa; je, kwa nini ATCL isikodi ndege (leasing)? Kwa nini tunanunua ndege mpya?

Mheshimiwa Naibu Spika, kununua ndege mpya ni rahisi kama ndege hizo zinakuwa zinatumika kwa muda mrefu. Kampuni nyingi za ndege kwa mfano Kenya Airways, RwandAir, Ethiopia Airways, Emirates, zote zinanunua ndege mpya. Wana-lease ndege ama wanakodi ndege tu kwa sababu maalum ya msingi. Kama imetokea route mpya wanataka kwenda, ndiyo wananunua ndege mpya, lakini kawaida, wana-lease.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukinunua ndege mpya unapata faida kubwa kwa sababu discount ni kubwa. Hii inakupa faida kwenye uendeshaji wako wa ndege yako kwa sababu ndege mpya gharama zake za matengenezo ni ndogo ukilinganisha na ndege iliyozeeka. Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge hili tulielewe.

Waheshimiwa Wabunge, nitatoa mfano mmoja, nita- compare ku-lease ndege na kununua ndege mpya na nitaangalia mfano kama nitakodi ndege ya Bombardier Q400 na nitaangalia ndege mpya ita-cost kiasi gani? Kuna njia mbili za kukodi ndege. Aina ya kwanza tunaita dry lease, maana yake unakodi ndege bila marubani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Njia ya pili tunaita wet lease. Ukichukua wet Lease maana yake unakodi ndege pamoja na marubani. Kitaalam, njia rahisi ya kukodi ndege ni dry lease ambapo unakodi ndege yako bila ya marubani, bila wahudumu na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bei ya wastani ya kukodi ndege kwa mwezi ni dola 200,000 mpaka 250,000 hiyo ya kwanza; ya pili, gharama ya matengenezo kwa mwezi, dola za Kimarekani 18,000. Kuna withholding tax ya TRA, ukikodi ndege unatakiwa ulipe dola 25,000 kwa mwezi. Jumla kwa mwezi mmoja unatakiwa angalau uwe na dola 300,000 ukikodi ndege. Kwa mwaka unatakiwa uwe na dola milioni tatu na nusu ukikodi ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukichukua na bima unatakiwa uwe na dola milioni nne kwa mwaka mmoja. Sasa ndege za Air Tanzania kipindi chake cha kuishi (life cycle) ni miaka 35. Sasa kwa muda wa miaka 35 huo, ukiendelea kukodi ndege utatumia takriban dola milioni 140, lakini sisi tunanunua ndege moja ambayo list price yake ni kama dola milioni 35. List price nasema, ile price ambayo iko kwenye mtandao. Kwa vile kukodi ndege ni rahisi kuliko kununua; samahani kukodi ndege ni gharama kubwa kuliko kununua, ndiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tena, kukodi ndege ni gharama kubwa kuliko kununua kwa sababu gani? Narejea, kwa sababu ndege moja ya Air Tanzania ambayo tumenunua itaishi miaka 35. Ukikodi kwa muda huo utatumia dola za Kimarekani milioni 140, wakati ukinunua ndege mpya itakuwa gharama yako ni dola milioni 35. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa dola milioni 35 umenunua, dola milioni 140 umekodi, ipi faida? Mnataka Serikali iende wapi? Ikanunue au ikakodi? Waheshimiwa Wabunge, ninyi ndiyo mnawakilisha Watanzania, mnataka tukanunue au tukakodi ndege? Watanzania wametusikia na majibu wanayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sitazungumzia wet lease kwa sababu bei yake ni mbaya zaidi. Nitazungumzia hiyo tu, nafikiri hiyo hapo imetosha, tuendelee mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kawaida mashirika yanakodi ndege tu kama kuna matumizi ya muda mrefu kama nilivyosema. Kama leo imetokea route kwa mfano Dar es Salaam – Bombay na hatuna ndege, pale ndiyo unakodi ndege, lakini wakati huo huo unaagiza ndege yako. Ndivyo yanavyofanya mashirika ya ndege yote. Huwezi kwenda kukodi ndege kama unataka kutumia ndege muda mrefu. Kama nilivyosema Rwanda wana ndege nane, zote wamenunua. Sasa sisi tutafanya nini? Lazima tununue ndege na ndege kununua ni rahisi kuliko kukodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, niwaulize ninyi ni mashahidi, mmeshakuwa Bungeni huu ni mwaka wa saba sasa. Kila Mbunge akianza kuja Bungeni anafikiria kununua nyumba. Kwa nini hamfikirii kukodi nyumba kule mnakotoka? Kwa sababu kukodi nyumba ni bei ghai kuliko kununua. Ukizungumza kununua na kukodi huwezi ukalinganisha hata siku moja. (Makofi)

Kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge, hili jambo liko hivyo, Serikali tumefanya maamuzi sahihi ya kununua ndege na tutaendele akufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja nyingine wanasema kwa nini tunanunua ndege kutoka makampuni mbalimbali? Hali hii itasababisha kuwa na gharama nyingi za matengenezo. Tukinunua ndege, tunaangalia ndege ambayo italeta faida kwa Shirika la Ndege, italeta faida kwa Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vigezo maalum vinatumika katika kununua ndege. Kigezo cha kwanza, unaangalia hiyo ndege yako inakwenda wapi? Yaani runway, kiwanja chako cha ndege kina urefu gani? Huwezi kwa mfano, leo unataka kwenda pengine Kiwanja cha Ndege cha Tabora ukasema upeleke jet engine, haiwezekani! Kile kiwanja kimetengenezwa kwa urefu wa kilometa 1.8, ni ndege ya turbo propeller engine ndiyo itakayokwenda tu, hiyo ya kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kigezo cha pili, unanunua ndege kutokana na hali ya hewa ya eneo lako. Hiyo ni muhimu sana na temperature ya kiwanja cha ndege, ndege yako inakokwenda. Eneo la tatu unaloliangalia ni mwinuko wa kiwanja cha ndege kule unakokwenda. Watu wengi tunakuwa na historia, tunapata simu au tunaambiwa kwamba Fastjet leo imekwenda Songwe na imeacha abiria.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wengi hawajui kwa sababu gani inaacha abiria? Kiwanja cha Ndege cha Songwe kile wakati mwingine hali ya hewa inabadilika sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Fastjet haina uwezo wa kuchukua mzigo ule na abiria wale kwa wakati ule, ndiyo unakuta baadhi ya abiria wanaachwa na baadhi ya mizigo inaachwa. Ni kwa sababu kiwanja cha ndege kile wakati mwingine hasa mchana hivi hakiwezi kuchukua ndege ya Fastjet na mzigo wote. Kwa hiyo, ukichagua ndege yako lazima hiyo uiweke kwenye akili vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu unaangalia ndege yako, je, ndege hiyo inataka kwenda sekta gani? Kwa mfano, kama unataka kwenda Mumbai – India, inabidi utafute ndege ambayo itakupa faida kwa kwenda Mumbai. Huwezi kuchukua ndege ambayo ukienda Mumbai unapata hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, tunanunua ndege kutokana na kule tunakokwenda. Mfano mzuri, ni Ethiopian Airlines today.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri leo Ethiopian Airways, ni shirika kubwa lakini wana Airbus, Boeing na Bombardier. Wana ndege zote hizi. Wakija Dar es Salaam wale wanaosafiri na Ethiopian Airways, usiku inakuja Bombardier hapa. Kwa sababu wanaona need ya kuja Dar es Salaam au mahitaji ya Dar es Salaam ni Bombardier, siyo ndege nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi kununua ndege tu kama unavyonunua njugu za aina moja, hapana. Unanunua ndege kutokana na soko lako na mahitaji. Hiyo ni muhimu sana Waheshimiwa Wabunge na Watanzania tuelewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalofanya sisi Serikali au wanalofanya Air Tanzania ni jambo sahihi na hatukurupuki tu. Tunatumia utaalam wa kutosha na tunafanya maamuzi sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakupa mifano mizuri, Kenya Airways wana Airbus, Boeing, Embria halafu wana Fokker 50, kwa sababu huwezi kununua ndege za aina moja. Unanunua ndege kutokana na mahitaji na sekta kuhakikisha kwamba unapata faida. Otherwise, ukinunua ndege za aina moja, unataka Airbus, utafanya nini? Bukoba haiwezi kwenda Airbus kwa sababu Airbus hawana ndege ya propeller. Pemba, Tanga haiwezi kwenda Airbus. Tutawafanya nini Watanzania hawa sasa? Hatuendi hivyo bwana! Au Pemba naambiwa. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja je, tumepata taarifa kuwa ATCL imeondolewa kwenye IATA kwa sababu ya madeni?

Waheshimiwa Wabunge, ATCL kweli iliondolewa kwenye IATA lakini siyo leo, ni mwaka 2008. Kazi tunayofanya sasa hivi Serikali ni kuirudisha ATCL kwenye IATA ambayo itawezesha kufanya booking popote pale duniani. Tunategemea kabla ya mwisho wa mwaka huu tutakuwa tumeingia kwenye mfumo, kwa sababu Serikali imejipanga na ninaamini Waheshimiwa Wabunge mtapitisha bajeti yetu tuhakikishe kwamba tunaingia kwenye mfumo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, kuna hoja nyingine inasema, Taarifa ya Ukaguzi wa CAG juu ya ATCL haijawasilishwa Bungeni ili ichambuliwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika jitihada zake za kufufua ATCL ilibaini kuwa hesabu za ATCL zilikuwa hazijakaguliwa toka mwaka 2007 mpaka 2015. Kazi tuliyoifanya Serikali ilimuagiza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu kufanya ukaguzi wa hesabu ya ATCL kuanzia mwaka 2007/2008 mpaka 2014/2015. Kazi hiyo imekamilika na ripoti imepelekwa kwenye Bodi ya ATCL. Kazi inayoendelea sasa hivi ni kufanya ukaguzi wa mwaka 2015/2016 na 2016/2017. Nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba ATCL inasimama. Lazima tuhakikishe kila senti tunayoingiza kwenye ATCL inatumika vizuri. Tukiweka shilingi tano tuhakikishe kwamba shilingi tano inatumika kwa maslahi ya ATCL na Watanzania. Kwa hiyo, naomba niwahakikishe Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali tumejipanga na tutalisimamia jambo hili vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo sasa kwenye sekta ya anga naomba niingie kidogo nizungumzie kwenye sekta ya usafiri wa nchi kavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sote ni mashahidi kwamba Serikali ya Awamu ya Tano tunajenga reli ya kisasa ya kiwango cha standard gauge kutoka Dar es Salaam – Makutupora – Tabora – Isaka – Mwanza; Tabora – Kigoma; Tabora – Mpanda. Hiyo ndiyo central line ambayo ninaijua na Serikali tunaijua hiyo na tunaifanya hiyo kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuanzia, tumeanza Dar es Salaam – Morogoro kilometa 300; Morogoro - Makutupora kilometa 422. Tunajenga treni ambayo katika nchi zetu hizi za East Africa ndiyo treni ya kwanza kwa sababu treni hii itakuwa inatembea na umeme, itakuwa na uwezo wa kwenda speed ya kilometa 160 kwa saa. Maana yake nini? Ni kwamba unatoka Dar es Salaam leo mpaka Dodoma kwa masaa yako mawili na nusu au matatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika nchi zote za jirani, ukienda Kenya wanajenga treni yenye speed ya 120, ukienda Ethiopia 120; speed kama hii unaiona South Africa kwenye Gautrain speed 160 lakini wana kilometa 80 tu wao pale mjini tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tumejipanga na gharama ya ujenzi huu kutoka Dar es Salaam mpaka Makutupora ni shilingi trilioni 7.016. Pesa ipo na wakandarasi wanafanya kazi. Awamu ya kwanza kutoka Dar es Salaam mpaka Morogoro itamalizika mwezi Novemba mwakani. Awamu ya Pili itamalizika mwaka 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera na msukumo wa Serikali ya Awamu ya Tano ni kujenga reli ya kati na matawi yake yote kama nilivyosema. Tabora kwa upande wa Tabora – Kigoma tayari sasa hivi tunamalizia upembuzi yakinifu ambao unafanywa na kampuni ya COY kutoka Denmark. Tunahakikisha kwamba tunatafuta fedha kwa ajili ya ujenzi huo. Hatuwezi kuanza ujenzi bila ya kuwa na feasibility study. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema kwa upande wa Tabora – Kigoma upembuzi wa kina, sehemu utakamilika mwezi Juni, 2018, miezi miwili inayokuja. Baada ya hapo ndiyo tutaanza kujipanga kuweza kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi. Huwezi kuanza ujenzi kama huna feasibility study. Utajua shilingi ngapi? Si utakwenda kupigwa tu? Waheshimiwa Wabunge, tumejipanga na tutaifanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna reli ya Dar es Salaam – Isaka – Rusumo – Kigali ambapo tunaanzia Isaka – Rusumo – Kigali kilometa 572. Reli hii imegawanyika sehemu mbili. Kuna Isaka – Rusumo ambapo Serikali ya Tanzania itajenga na Rusumo - Kigali Serikali ya Rwanda itajenga. Reli hii ina faida kubwa sana kwa sababu itahudumia mzigo wa Kigali



yenyewe, pia itahudumia mzigo wa Congo Kaskazini ambayo ni maeneo ya Goma na Bukavu.

Mhesimiwa Naibu Spika, kutoka Dar es Salaam leo mpaka Kigali ni masaa au ni kilometa 1,491. Kwa mwendo wa standard gauge au kwa kutumia standard gauge utatumia masaa 15, lakini mzigo ukitoka Mombasa, Malaba ambao unaenda Uganda mpaka Kigali ni kilometa 1,792 utatumia masaa 24 hasa ukiangalia reli ya Kenya ya mzigo ni kilometa 80 kwa saa. Sasa itakuwa jambo la kichekesho kwamba mtu wa Rwanda ambaye ana mzigo wake kutoka Dar es Salaam mpaka Kigali ambaye anaweza kutumia masaa kama 15 aende akapitie Mombasa ambako atatumia masaa 24, hiyo kwa biashara haiingii akilini hata siku moja. Mfanyabiashara yeyote anahakikisha kwamba anatumia njia fupi kusafirisha mzigo wake ambayo itampatia faida zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nimesema tutapata mzigo wa Congo hasa kule sehemu ya Kaskazini? Ni kwa sababu kutoka Kigali mpaka Bukavu ni kilometa 225 na barabara iko nzuri sana unaenda masaa matatu umefika, kwa vile mzigo ukitoka Dar es Salaam mpaka Bukavu utatumia masaa 18. Mzigo huo huo ukitoka Mombasa mpaka Bukavu utatumia masaa 27 kwa reli ya Kenya. Mfanyabiashara wa Congo especially eneo la Kaskazini hataweza kutumia reli ya Kenya, atatumia reli ya Tanzania kwa sababu ndiyo njia rahisi. Hii hata huhitaji tochi wala huitaji rocket science, ni simple, one plus one inakupa mbili. Wala haina mjadala hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi Rwanda wanatumia Bandari ya Dar es Salaam na kuna zaidi ya tani milioni 1.1, asilimia 98 ya mzigo huu unapita barabarani, lakini unatumia bandari ya Dar es Salaam. Kule Bukavu Kongo kule kuna mzigo tani 772,000. Sasa ukichukua maeneo haya mawili, Rwanda na Kaskazini Kongo kuna takriban tani milioni mbili za mzigo ambazo zitapita Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, hii reli tunayoijenga itafika kwenye machimbo ya Nickel kule Kabanga ambapo kwenye machimbo yale kuna tani milioni 36.3, inahitaji reli hii inayotoka Dar es Salaam ikapita Isaka, Isaka ikaenda Rusumo, Rusumo - Kigali. Kabla hujafika Rusumo, unachepuka unakwenda Kabanga kwenye machimbo. Kwa hiyo, plan ya Serikali ni hiyo lakini wakati huo reli ya kati tunaijenga, hasa Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, hii ya Kigoma nataka nayo niizungumze kidogo. Kutoka Kigoma tukijenga standard gauge mpaka Dar es Salaam, utatumia masaa kumi. Ni karibu Kigoma, lakini kutoka Kigoma mpaka Kalemie ni kilometa kama 120 kuvuka lile ziwa pale, lakini kwa meli ya mzigo utatumia masaa matano. Hii ni uzoevu kutoka Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitoka Pemba kwenda Zanzibar ni distance hii tu, lakini kwa meli ya mizigo unatumia masaa manne au matano, wale mashahidi si ndio; kwa meli ya mzigo siyo meli ya abiria. Ukienda ukishusha na kupakia mzigo wako utatumia kama masaa manane kupakia na kuteremsha mzigo. Halafu kutoka Kigoma au Kalemie unaenda Lubumbashi kwa sababu mzigo mkubwa pale uko kwenye Kasanga kule, sehemu ya kule Kusini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutoka Kigoma mpaka Lubumbashi ni kilometa 664 na bahati mbaya sana reli ya pale imekufa. Hii ya Tanzania ni nzuri kuliko ya pale, inaenda kilometa 25 kwa saa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mzigo ukipitia njia ya kule utachukua karibu masaa 41. Kule kuna tani milioni tatu sasa hivi ambapo Tanzania sisi tunapata tani 764,000. Mzigo mwingine unaenda Afrika Kusini, mzigo mwingine unaenda Durban, mwingine unaenda Namibia na mwingine unaenda Angola.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyosema, mahesabu siyo tatizo, tuko tayari kujenga reli ya kutoka Tabora mpaka Kigoma. Tunalosubiri ni hiyo feasibility study ifanyike ili tujue mahesabu kiasi gani, tuanze kutafuta fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na maoni kwamba Serikali tujenge reli kwa kutumia mfumo wa PPP. Ni kweli Serikali tunapenda sana mfumo wa PPP, ni mfumo mzuri, lakini katika historia ya ujenzi wa reli katika Afrika, hasa reli za standard gauge haijawahi kujengwa kwa kutumia mfumo wa PPP.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kenya wamechukua mkopo kutoka China; Ethiopia wamechukua mkopo kutoka China; Nigeria wanajenga standard gauge, wamechukua mkopo kutoka China; Morocco wamechukua mkopo na wao kutoka mabenki na Serikali. Kwenye miradi mikubwa kama hii, siyo rahisi kupata PPP kama watu wanavyofikiria. Serikali tuko tayari kushirikiana na mtu yeyote yule tuweze kufanya PPP lakini siyo rahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niongelee sekta ya bandari, usafiri wa nchi kavu. Bandari yetu inafanya kazi vizuri, mzigo umeongezeka. Kama nilivyosema, kutoka mwezi Julai, 2017 mpaka mwezi Machi, 2018 tumesafirisha takriban tani milioni 9.822 ukilinganisha na kipindi kama hicho mwaka 2016/2017. Hili ni ongezeko la asilimia 14.6. Mizigo ya nchi za jirani mwaka huu tumesafirisha mizigo tani milioni 3.9 ikilinganishwa na tani milioni 3.1 mwaka 2016/2017.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mapato mwaka 2017 kuanzia mwezi Julai mpaka mwezi Desemba bandari wameweza kupata mapato ya shilingi bilioni 14.79 wakati matumizi yamekuwa shilingi bilioni 139, salio takriban shilingi bilioni 280. Kwa kipindi kama hicho mwaka uliopita kulikuwa na salio la shilingi bilioni 83 tu. Kwa vile bandari inafanya kazi vizuri na naomba Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wenzangu tuendelee kui-support Bandari ya Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo miradi mingi sasa hivi tunatekeleza Bandari ya Dar es Salaam tukianzia pale Dar es Salaam penyewe. Kwanza sasa hivi tunafanya ukarabati na kuongeza kina cha maji kutoka Gati Namba Moja mpaka Namba Saba. Vilevile tunajenga gati maalum sasa kwa ajili ya kupakilia na kupakulia magari ambapo kasi inaenda vizuri. Hivi karibuni tutaanza kutekeleza mradi mwingine kwa ajili ya kujenga eneo la kugeuzia meli na kuongeza gango la Bandari ya Dar es Salaam. Mradi unaoendelea hivi sasa unagharimu takriban shilingi za Kitanzania shilingi bilioni 377.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna kazi tunaendelea nayo huko Mtwara, tunajenga gati jipya watu wa Mtwara wanajua. Gati hilo lina urefu wa mita 300 na tutatumia takriban shilingi bilioni 137 kwa kazi ile. Kasi inaenda vizuri na tunategemea kazi itamalizika vizuri. Tuna kazi huko Lindi tunajenga gati la Lindi na limefiki asilimia 70. Tuna kazi huko Kigoma tunajenga Bandari za Kigoma tatu; Kigoma wenyewe, Ujiji na Tiberizi, zote tunazijenga. Tumetenga pesa bajeti ya mwaka huu na kazi nzuri inaendelea. Tuna kazi hivyo hivyo huko Mwanza inaendelea kuboresha gati yetu ya Mwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa usafiri wa majini, tunajenga meli mpya sasa huko Ziwa Tanganyika yenye uwezo wa kuchukua abiria 600 na tani za mzigo tani 400. Tunafanya kazi hiyo hiyo huko Lake Victoria ambapo tunajenga meli ya kuchukua abiria 1,200 na itachukua mzigo wa tani 200 na magari 25.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafanya kazi kama hiyo huko Lake Nyasa, tunajenga meli ya kuchukua abiria 200 halafu na tani 200 za mzigo. Vilevile tunafanya ukarabati wa MV. Liemba, MV. Victoria na Meli nyingine zote tunazifanyia ukarabati tuhakikishe kwamba sasa hivi zinafanya vizuri. (Makofi)

Mhshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kuboresha usafiri wa majini tunataka kujenga kivuko kwa ajili ya ndugu zetu wa huko Nyamisati na Mafia. Tayari tumetenga kwenye bajeti hii shilingi bilioni tatu kwa kujenga landing craft mpya ambayo itatumika kwa watu wa Mafia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hayo ndiyo maelezo machache kuhusu usafiri wa majini. Naomba nizungumzie kidogo kuhusu usafiri wa nchi kavu. Tokea juzi kulikuwa na mazungumzo mengi hapa kuhusu TARURA na maoni ya Waheshimiwa Wabunge tumeyapokea, tunaheshimu na tutayafanyia kazi. Naomba nitoe maelezo kidogo na ninyi mpate picha ya Mfuko wa Barabara unafanya kazi vipi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mfuko wa Fedha za Barabara kwa kawaida unagharamia miradi ya barabara kuu na barabara za mikoa ambazo zinasimamiwa TANROADS halafu barabara za Wilaya ambazo zinasimamiwa na TARURA. Inatoa fedha kwenye TARURA na TANROADS huku asilimia nafikiri 70 huku 30. Vilevile kuna vigezo maalum vinatumika katika kutoa pesa. Kigezo cha kwanza tunachotumia, tunaangalia urefu wa mtandao wa barabara; kigezo cha pili, tunaangalia je, barabara hizo ni za lami, changarawe au udongo? Kigezo cha tatu tunachoangalia, tunatumia hali ya barabara yenyewe ikoje (conditions)? Kigezo cha nne, tunatumia wastani wa idadi ya magari na uzito wa magari yanayopita kwenye barabara hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, TANROARD au mtandao wa barabara unaosimamiwa na TANROAD una jumla kilometa 36,257.97. Kati ya kilometa hizo, kilometa 9,264.57 ni za lami, kilometa 25,303.4 ni za changarawe na kilometa 1,690 ni za udongo. Mtandao wa barabara unaosimamiwa na TARURA una jumla ya kilomita 108,946.19. Kati ya kilometa hizo, kilomita 1,449.55 ndizo za lami ukilinganisha na TANROADS wenye kilometa 9,000 za mahitaji kwa kutengeneza au matengenezo ya barabara ya TANROADS ni makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, TARURA vilevile inahudumia kilometa 24,405 za changarawe pamoja na kilometa 85,091.24 za udongo. Kwa vile ukilinganisha tu mtandao TANROADS wanasimamia barabara kubwa sana za lami kuliko TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, matengenezo ya barabara za lami ni gharama zaidi kuliko matengenezo aina nyingine ya barabara. TANROADS yenye kilometa 9,264 za lami inahitaji fedha nyingi kuliko TARURA yenye urefu wa kilometa 1,449.55 za lami kwa sasa. Aidha, upana wa barabara zinazosimamiwa na TANROADS ni mita 8.5 mpaka mita 9.5. Upana wa barabara unaosimamiwa na TARURA ni mita 4.5 mpaka mita 6.0. Hii inafanya TANROADS ihitaji fedha nyingi kwa ajili ya matengenezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, idadi ya magari yanayotumia barabara kila siku, barabara kuu za mikoa idadi ya magari ni kati ya 300 mpaka 52,000. Ukichukua barabara ya New Bagamoyo Road ndiyo hayo. Wakati barabara za Wilaya nyingine ni kati ya magari matano mpaka 50 kwa siku. Kwa hiyo, wingi wa magari husababisha barabara kuharibika zaidi na kuhitaji zaidi fedha za matengenezo zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, uzito wa magari yanayopita katika barabara zinazotumika na TANROADS ni tani 55 wakati barabara za Wilaya zote ni tani 10. Uzito wa magari husababisha barabara kuharibika haraka kwa vile barabara inayosimamiwa na TANROADS zinahitaji pesa nyingi. Tumetoa ushauri ambao tunasema, tumejaribu kuangalia ushauri wa kuongeza tozo la mafuta kuangalia kama tutapata pesa zaidi kwa ajili ya TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tunasema tutafute vianzo vipya ikiwa ni pamoja na tozo ya maegesho ya magari mjini, ukaguzi wa magari, tozo ya magari mazito, tozo ya barabara na tozo ya matumizi ya barabara kulingana na uzito na umbali wa magari. Hivi ndiyo baadhi ya vyanzo vyote ambavyo tunapendekeza tuone jinsi gani tutaweza kuongeza pesa za TANROADS na pesa kwa ajili ya kukarabati barabara za TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema leo asubuhi Mheshimiwa Naibu Waziri, tunazo barabara nyingi tunazijenga kwa kiwango cha lami hivi sasa. Barabara tunazojenga kwa kiwango cha lami ambazo nyingi zinaunganisha mikoa na mikoa kwa mfano sasa hivi tunajenga barabara kutoka Sumbawanga – Matai – Kasanga Port yenye urefu wa kilometa 112; tunajenga barabara ya Ushirombo - Lusahunga yenye urefu wa kilometa 110; barabara kutoka Kidatu - Ifakara yenye urefu wa kilometa 65; barabara kutoka Tabora - Sikonge yenye urefu kilometa 30; tunajenga barabara kutoka Usesula - Komanga yenye urefu wa kilometa 115.5; barabara kutoka Komanga mpaka Kasinde yenye urefu wa kilometa 112.8; barabara ya kutoka Kasinde - Mpanda kilometa 111.7.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tunajenga barabara inayotoka Mara kwenda Arusha - Makutano - Sanzate kilometa 50; barabara kutoka Waso mpaka Sare Junction kilometa 50; barabara ambayo inatoka Mpanda mpaka kuelekea huko Kigoma ambayo tumeanzia kwanza Mpanda - Vikonge kilometa 35; barabara kutoka Kisole - Bulamba kilometa 50, barabara kutoka Maswa - Bariadi kilometa 49.5; barabara kutoka Kidahwe - Kasulu kilometa 63; barabara kutoka Nyakanazi - Kakonko kilometa 50; barabara kutoka Nduta – Kibondo - Kabingo inayojumuisha barabara ya kupita Kibondo Mjini kilometa 87.7 na tunajenga barabara ya Uvinza - Malagarasi yenye kilometa 51.1.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara vilevile itaanza maandalizi ya ujenzi wa kiwango cha lami kwa barabara kutoka Tanga mpaka Pangani yenye urefu wa kilometa 50; huko Geita- Bulyanhulu Junction kilometa 58.3; barabara kutoka Bulyanhulu Junction mpaka Kahama kilometa 61.7; tunatayarisha ujenzi wa barabara kutoka Kazilambwa mpaka Chagu kilometa 42; tuna mpango wa kujenga barabara ya kutoka Ludewa – Kilosa kilometa 24; tuna mpango wa kujenga barabara kutoka Norangi – Itigi - Mkiwa kilometa 56.9; na tunajenga barabara kutoka Lusaunga - Lusaumo kilometa 91.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile tuna mpango wa kujenga barabara ya Kibaoni - Stalike kilometa 71; tuna mpango wa kujenga barabara kutoka Vikonge - Mangunga mpaka Uvinza kilometa 159; tunafanya upanuzi wa barabara ya kwenda Kiwanja cha Ndege Mwanza na tuna mpango wa kujenga barabara ya kutoka Nyangunge mpaka Simiyu - Mara - Boda yenye urefu wa kilometa 100.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna miradi mingi siwezi kuitaja yote, lakini tuna kazi kubwa tunahakikisha kwamba mikoa yote ya Tanzania tunaifungua ili kuhakikisha Watanzania wanapata miundombinu hii ya kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama mnavyojua pia tunajenga huko Dar es Salaam TAZARA flyover ambayo tutatumia takribani shilingi bilioni 99. Tunajenga Ubungo interchanges ambayo tunatumia takriban shilingi bilioni 177; tunajenga daraja huko Momba, tunajenga daraja huko Magara, Sibiti, Lukuledi, Wami Juu, Simiyu, Sukuma mkoani Mwanza na daraja la Salenda Dar es Salaam; tunafanya feasibility study kwa ajili ya daraja la Mtera, Kigogo Busisi na Malagarasi Chini huko Kigoma.

Mheshimiwa naibu Spika, tuna miradi mingi sana ya barabara ambayo yote mnaweza kuiona kwenye kitabu changu cha hotuba ya bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya mawasiliano muhimu sana kwa nchi yetu. Sekta ya mawasiliano ndiyo uchumi wa nchi yetu, ni maendeleo na ndiyo maisha ya Watanzania. Bila mawasiliano kwa kweli maisha kidogo yanaweza kuleta shida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia Desemba, 2017 tulikuwa na wateja wa simu takribani milioni 50; watumiaji wa internet takriban milioni 23. Watanzania ambao wanatuma pesa kwenye mitandao mbalimbali takribani kuna akaunti milioni 22. Pesa zilizotumwa kwenye mtandao mwaka 2017 ni takriban shilingi trilioni 104.3. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli kama nilivyosema, sekta ya mawasiliano ni muhimu sana na ni sekta ambayo inapeleka uchumi wetu kwenye hali ya juu. Kwa upande wa mawsiliano vijijini kama Naibu Waziri alivyosema leo, kwa kipindi tulichopita tumejenga Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote umepeleka mawasiliano kwenye Kata 551, vijijini 1,954.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepeleka mawasiliano vijijini pamoja na makampuni yote takribani vijiji 5,751. Mwaka 2018/2019 utakuwa ni mwaka ambao utaleta maendeleo makubwa kwenye sekta ya mawasiliano. Naomba tu Watanzania waitumie miundombinu hii kwa maslahi ya maendeleo, wasiitumie mindombinu ya mawasiliano kwa kupeleka message za uchochezi, kupeleka picha chafu na kufanya ulaghai na mambo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo, naomba kutoa hoja.