Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchangia hotuba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Tunduru Kusini lipo pembezoni mwa mpaka katika Mto Ruvuma hivyo wananchi wengi wa Tunduru wanaenda Msumbiji kupitia Mto Ruvuma, ninaomba kijengwe kivuko katika Mto Ruvuma sehemu ya Chamba au Makade ili wananchi waweze kutumia badala ya kutumia mitumbwi ambayo inahatarisha maisha ya wananchi hao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu barabara za ulinzi, miaka ya 1970 mpaka 1980 kulikuwa na barabara ya ulinzi ilitoka Mtwara mpaka Mbamba bay, barabara hii ilikuwa inasaidia kufanya patrol kwa Wanajeshi wa JWTZ kwa ajili ya kulinda mipaka yetu. Barabara hii imekufa kabisa haionekani kabisa, barabara hii ilisaidia sana hasa wananchi wanaoishi kandokando ya Mto Ruvuma. Barabara hii ilitumika sana na askari wetu pamoja na wananchi kusafirisha mazao kwenda kwenye masoko. Sasa hivi wananchi wanazunguka sana kutoka kijiji kimoja kwenda kingine kwa kuwa barabara hii imekufa kabisa na imesababisha ongezeko la magendo sana kutokana na njia maalum inayounganisha vijiji vilivyo kando kando na Mto Ruvuma. Hivyo basi, ninaomba barabara ile ifufuliwe ili kuongeza ulinzi wa mipaka yetu kwa kuwa Watanzania wa vijiji hivyo wanaingiliana sana na wananchi wa Msumbiji na wamepata mahitaji yao ya kila siku kutoka Tanzania hasa Tunduru Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, matengenezo ya barabara ya Tunduru – Nalasi - Chamba na Nalasi – Mtwara Pachani; barabara hizi ni za vumbi na zina milima ambayo kila mwaka ukitengeneza kwa kifusi cha kawaida zinatumika miezi sita. Kwa hiyo, tunaomba barabara hizi zitengenezwe kwa kiwango cha changarawe hasa barabara ya Tunduru – Chamba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mawasiliano ya simu, tunaomba mitandao ya simu katika vijiji vya Misyaje, Nasomba, Lukala, Makande, Msinji, Semeni na Azimio upatikanaji wa mawasiliano umekuwa wa shida, hivyo tunaomba minara ya simu ijengwe katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa reli ya Mtwara Corridor, reli hii ni muhimu sana katika Kanda ya Kusini kwa vile kuna makaa ya mawe na chuma kitasafirishwa katika reli hii pamoja na mazao ya korosho, kahawa, tumbaku, mahindi na maharage jambo ambalo litakuza bandari ya Mtwara na Bandari ya Mbamba bay. Hivyo naomba sana ujenzi huu kwa maana ya upembuzi yakinifu ufanyike kwa kina ili ujenzi uanze muda mfupi ujao kwa sababu barabara za Kusini zinaharibika haraka kwa sababu ya kupitisha malori makubwa ya makaa ya mawe, korosho na mahindi.