Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze mchango wangu kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na leo niweze kuchangia hotuba hii. Mchango wangu kwa leo naomba nianze na sera ya kuunganisha mikoa kwa barabara za lami. Ni wakati muafaka sasa sera hii iwekewe lengo, kwa maana haijulikani ni kwa muda gani sera hii itakamilika kwani hadi leo utekelezaji wake haueleweki. Mikoa mingine tumeanza kuunganisha Wilaya wakati mikoa mingine bado. Mfano, Mkoa wa Lindi na Ruvuma na Lindi na Morogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, mawasiliano kwa karne hii ni jambo muhimu sana, lakini kutokupewa fedha za maendeleo ni kurudisha nyuma sekta hii, kwani sehemu kubwa ya nchi yetu mawasiliano ya simu ni duni sana. Pamoja na kuwepo kwa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (USCAF), ni jambo la kusikitisha sana kuona fedha za mfuko huu nazo hazipatikani kwa wakati jambo linaloondoa dhana ya kuundwa kwa mfuko huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, USCAF wanashindwa kutekeleza miradi yao kwa kutopewa fedha zao toka Hazina. Mfano katika Jimbo la Liwale lenye kata 20 ni sehemu chache sana kuna mawasiliano ya simu kwenye baadhi ya kata. Hali ni mbaya sana katika Kata za Mpigamiti, Lilombe, Miru, Ndapata, Mlembwe, Mkutano na Ngongowele. Kata hizi hali ya mawasiliano ni mbaya sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Nangurukuru, Liwale ni barabara iliyotajwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015. Hata hivyo, barabara hii ni kiungo muhimu sana kwa uchumi wa Kanda ya Kusini kwa ujumla. Pamoja na barabara ya Nangurukuru - Liwale lipo pia daraja la Mbwemkuru linalounganisha Wilaya ya Nachingwea na Liwale. Vilevile nashukuru barabara ya Liwale - Nachingwea angalau imetengewa fedha kwa ajili ya upembuzi yakinifu. Ni ombi langu, fedha hizo zifike kwa wakati. Pia kuna daraja linaunganisha Kilwa - Liwale katika Kijiji cha Nanjilinji. Naomba ipewe kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, taasisi zote zilizo chini ya Wizara hii ni bora zikapewa fedha zake kwa wakati ili ziweze kufanya vizuri. Taasisi hizi ni kama USCAF, TTCL, Bandari, MSCL na TAZARA. Taasisi hizi zinakwama sana kwa sababu ya upungufu wa mitaji na fedha za kutekeleza miradi yake ya maendeleo mfano USCAF, wana sababu gani ya kushindwa kutekeleza miradi yao kwa ukosefu wa fedha wakati fedha toka kwenye vyanzo vyao zinapatikana? Vilevile Serikali ilipe malimbikizo ya mishahara ya wafanyakazi wa MSCL ili wafanyakazi wawe na moto wa kufufua shirika hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya viwanja vya mikoa ina makundi mawili; kuna vilivyotajwa kimoja kimoja na vingine vimewekwa kwa pamoja. Ninachotaka kujua, ni kwa nini iko hivi? Vile vilivyo pamoja tutajuaje vimejirudia pia kwenye madaraja ya mikoa na barabara za baadhi ya mikoa? Naomba kupata ufafanuzi juu ya jambo hili. Katika bajeti hii Mkoa wa Lindi miradi yake yote iko kwenye makundi hayo hapo juu, yaani yale ya jumla, fedha za Mkoa wa Lindi ni kidogo sana. Barabara ya Masasi – Nachingwea - Nanganga, upembuzi yakinifu umekamilika, lakini ni bajeti ya pili sasa barabara haitengewi fedha wakati huo huo ziko barabara zimekuja nyuma lakini zimepewa fedha za ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naliomba Shirika la Reli kuwalipa askari polisi waliowatumia kusindikiza treni kati ya mwaka 2016/2017 ambao bado wanadai. Askari hawa walifanya kazi kwa uaminifu, lakini malipo yao yamekuwa kitendawili. Gharama za ujenzi wa barabara zimekuwa kubwa kwa sababu ya sheria zetu ambazo kwa kiwango kikubwa hazina faida yoyote. Mfano, Sheria ya Madini, Sheria ya Maji, Sheria ya Mazingira na kadhalika. Mkandarasi hulazimika kuweka gharama za ununuzi wa madini kwa maana ya kifusi na Halmashauri kudai ushuru wa kifusi hicho. Kama vile haitoshi, watu wa mazingira nao wanadai fidia ya uharibifu wa mazingira unaotokana na ujenzi huo kwa kuacha au kufukia mashimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali ingeondoa tozo hizi ili kupunguza gharama za ujenzi wa barabara hizo, kwani hayo maduhuli yote ni ya Serikali moja. Hivyo Serikali ifanye marekebisho ya sheria hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ujenzi wa reli ya kisasa, naungana na ushauri wa Kamati kuwa Serikali ingeangalia sasa kushirikisha watu binafsi au kuomba wahisani kwani kutegemea fedha za ndani pekee kutaifanya Serikali kushindwa kuhudumia sekta nyingine au Wizara nyingine. Hivyo ujenzi unaoendelea sasa kwenye sehemu zilizobaki, jambo hili lingefikiriwa kwa manufaa ya Taifa kwa jumla ikiwezekana hata kukopa mkopo wa masharti nafuu. Kwa sababu ya kiuchumi, kipande cha Isaka na kile cha Kigoma Serikali ingeanza na kuacha Kigoma badala ya Isaka kwani route ya Kigoma ina vivutio vingi vya kiuchumi kuliko Isaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, malipo kwa wakandarasi ni bora yakafanywa kwa wakati kwani kulipa madeni haya kwa riba ni kupoteza fedha za walipa kodi. Wakandarasi wa kigeni wanafaidika sana na riba kuliko hata faida wanayoipata kwenye mkataba husika. Hakuna sababu ya kuingia mkataba na mkandarasi wakati hakuna fedha za kutekeleza mkataba husika.