Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Ujenzi. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na ukarimu aliyetuwezesha kuwa na afya na uzima siku ya leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichukue nafasi hii kuipongeza na kuishukuru Serikali kupitia Wizara hii ya Ujenzi kwa kusikiliza ombi langu na kujibu shida za barabara yetu ya Ubena Zomozi – Ngerengere – Tununguo – Mvuha - Kisaki mpaka Selous kwa kuipandisha daraja kuwa ya mkoa na kutengewa fedha katika bajeti hii shilingi bilioni tano kwa ajili ya kutengeneza barabara hii na kuiboresha ili iweze kupitika mwaka mzima na kutumika pia kupeleka vifaa vya ujenzi katika mradi Mto Rufiji. Vilevile nashukuru Serikali kwa kutenga fedha kwa matengenezo mbalimbali katika barabara ya Bigwa – Kisaki, Madamu – Kinole - Msomvinzi – Mikese na madaraja na sehemu korofi katika Jimbo letu la Morogoro Kusini Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na matengenezo hayo ya barabara ya Bigwa - Kisaki lakini barabara hii ni muhimu kwa uchumi wa nchi na wananchi wa Morogoro Kusini Mashariki, Morogoro Vijijini, Morogoro na Taifa kwa ujumla. Nasema ni muhimu kwa sababu ni barabara inayounganisha Makao Makuu ya Wilaya Mvuha. Pia ni barabara inayokwenda katika Mbuga yetu ya Selous kwa lango la Kisaki. Ni barabara inayounganisha Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Pwani kupitia Kisaki - Stiegler’s Gorge na kufika Kibiti, Rufiji na kurahisisha mawasiliano na muingiliano wa watu wetu kati ya Morogoro na Mikoa ya Pwani, Lindi na Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ipo katika Ilani ya CCM kutengenezwa kwa kiwango cha lami kwa umbali wa kilometa 78 toka Morogoro - Bigwa – Mvuha. Pia ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne na aliyekuwa Waziri wa Ujenzi wa wakati huo ambaye kwa sasa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kuwa barabara hii itatengenezwa kwa kiwango cha lami. Naiomba sana Serikali yangu ya CCM kutengeneza barabara hii kwa kiwango cha lami ili kuinua uchumi wa watu wa Mororgoro Vijijini na Taifa kwa ujumla na kutusaidia watu wa Morogoro Vijijini kufikisha bidhaa zetu za mazao ya kilimo kwenye masoko kwa urahisi na kuinua utalii katika pori na Mbuga yetu ya Selous.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii imebeba imani ya wananchi wangu kama Mbunge, Chama cha Mapinduzi, Serikali yangu na Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kuwa tukiahidi tutatekeleza na kuzingatia Ilani na sera zetu za kuunganishwa kwa kiwango cha lami. Upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umeshamalizika muda mrefu na wananchi walishapisha na kuondoka katika maeneo yao kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii zaidi ya miaka mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa sijaona dalili za kuanza ujenzi huo wa kiwango cha lami na tumebakiwa na miaka miwili kufika mwaka 2020 kipindi cha mwisho kutekeleza Ilani ya Chama chetu CCM ikiwamo hii barabara ya Bigwa – Kisaki kutengenezwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa masikitiko makubwa sijaona katika bajeti hii barabara za mkoa kwa mkoa kutengenezwa kwa kiwango cha lami kati ya Mkoa wa Mororgoro na Pwani. Pia barabara hii inakwenda kwenye mradi mkubwa wa umeme wa Stiegler’s ambao una manufaa makubwa kitaifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili nataka kuiomba Serikali kupandisha hadhi barabara ya Ngerengere – Diguzi- Matuli – Kwaba - Mkulazi mpaka Kidunda ili iwe katika ngazi ya mkoa kwa sababu pamoja na uwepo wa TARURA, lakini ni changa na barabara hii ni ndefu ina urefu wa kilometa 75 na ina miradi mikubwa miwili ya kitaifa ya Bwawa la Kidunda na ujenzi wa Kiwanda cha Sukari cha Mkulazi. Barabara hii haipo kwenye mipango ya bajeti hii wakati miradi ya ujenzi wa Bwawa la Kidunda na ujenzi wa Kiwanda cha Sukari cha Mkulazi inatelekezwa mwaka huu. Naiomba Serikali kutenga fedha za matengenezo ya barabara hii ili kuweka mazingira wezeshi na rafiki kwa uwekezaji wa viwanda katika Kata ya Mkulazi na Matuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ni suala la mawasiliano; hatuna mawasiliano ya simu katika Kata ya Mkulazi, Matuli, Tununguo, Seregete A&B pamoja na Kata za Kibuko, Tomondo, Tegetelo na Ludewa. Naomba sana mawasiliano kwenye kata hizi na mkazo zaidi katika Kata ya Matuli na Mkulazi sababu ni kata zenye miradi mikubwa ya kielelezo ya ujenzi wa Bwawa la Kidunda na Kiwanda cha Sukari Mkulazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja.