Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. JUSTIN J. MONKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu sana. Nianze kwa kuipongeza sana Serikali, hasa Wizara hii, kwa fedha ambayo imeshatutengea sisi Mkoa wa Singida katika kuboresha miundombinu ya barabara tuliyonayo. Tumeona wameanza kutenga fedha kwa ajili ya feasibility study ya barabara ya kutoka Singida kuelekea Katesh na Singida kuelekea Shelui, sisi wa Mkoa wa Singida tunafurahi sana katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunalo tatizo la reli yetu ambayo imeunganisha kutoka Manyoni kuja Singida Mjini. Reli hii haijafanya kazi tangu mwaka 2009 na kumekuwepo na dhana potofu kwamba baada ya kuwa sasa tumepata barabara za lami basi pengine reli hiyo ilikuwa haiwezi kuzalisha na haiwezi kupata mizigo. Tukumbuke Singida ni katikati ya nchi na sisi pale Singida kwa reli hii kufika pale maana yake tunaweza tukahudumia mizigo inayotoka Simiyu, Shinyanga na Mwanza ili kuweza kuendelea kuokoa barabara hizi ambazo zimekuwa zikiharibika kwa wakati mwingi ambao tumetumia malori kwenye barabara zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Singida Kaskazini pia tunazo barabara zenye shida. Ipo barabara ya kutoka Singida – Ilongero – Mtinko – Mudida inaelekea Haydom, ukiangalia katika kitabu cha Mheshimiwa Waziri barabara hii sasa naona imetengewa fedha ya kuanzia Karatu – Mbulu, ikishafika pale Haydom inakwenda Sibiti. Sasa barabara hii iko katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi, ilikuwa ni ahadi pia ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne na ahadi ya Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Tano.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Wizara iangalie namna ya kufanya feasibility study katika barabara hii ili kuja kuunganisha na Mji wetu wa Singida ili barabara itakapofunguliwa basi wananchi hawa waweze kupata huduma kwa sababu ni barabara muhimu sana inayounganisha miji mingi sana, lakini inaunganisha huduma za muhimu sana, hasa huduma za hospitali kikiwemo Kituo cha Afya cha Ilongero, Hospitali yetu ya Mtinko, lakini tunakwenda Nkungi, lakini kuna Hospitali ya Rufaa ya Haydom.

Mheshimiwa Naibu Spika, iko barabara muhimu sana katika Jimbo la Singida Kaskazini, barabara hii ni ya kimkakati hasa upande wa uchumi na barabara hii inatokea Singida Mjini, inapita katika Kata ya Kinyeto – Kinyagigi – Meria – Magojoa – Msange na inakwenda kuunganisha katika Kata ya Itaja katika Kijiji cha Sagara kwenye Barabara Kuu iendayo Katesh, Arusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ni muhimu sana kiuchumi, sisi ni wazalishaji wakubwa sana wa vitunguu na ni wazalishaji wakubwa sana wa alizeti, tunahitaji kuileta alizeti hii katika kiwanda kilichopo Singida Mjini, lakini pia tunahitaji kusafirisha vitunguu vyetu. Mpaka sasa wanunuzi walio wengi wanashindwa kufika katika maeneo yetu, tunashindwa kuwa na masoko ndani ya Halmashauri yetu kwa sababu barabara zetu ni mbovu na watu wanalazimika kutumia usafiri wa magari madogo madogo na hivyo badala ya wanunuzi kufika kwenye maeneo wanakuja tu wale wafanyabiashara wa kati.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii pia tuliiombea kwa Mheshimiwa Rais, ina urefu wa kilometa 42 tu na Mheshimiwa Rais alionesha utayari wa kuijenga katika kiwango cha lami. Kwa hiyo, niiombe sana Wizara iiweke katika mpango wa kufanyiwa feasibility study katika kipindi cha mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tunayo barabara moja ndogo, ina kilometa tano, sita, ambayo inatoka katika Kijiji cha Sagara inakwenda katika Kijiji cha Gairo na inakwenda kuunganisha katika Kijiji cha Pohama na kutoka hapo inakwenda tena kuunganisha katika Mji wa Katesh. Barabara hii ina matatizo na wananchi wanaoishi katika Vijiji vya Gairo wametengwa na eneo kwa sababu ukitokea Pohama kuna madimbwi na wakati huu wa mvua haipitiki kabisa. Lakini ukitoka Gairo kupanda hapa Sagara kuna mlima mkubwa ukiwa unapanda katika hilo Bonde la Ufa na barabara hii haipitiki kwa kweli kwa vyombo vya moto.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja, ahsante sana.