Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa hii nafasi adimu. Nianze kwa kuipongeza Wizara inafanya vizuri sana hasa kwa kuboresha bandari nafikiri kwa kiasi kikubwa hii itapunguza gharama ya malighafi zinazokuja kutoka nje zikiwemo mbolea, lakini vilevile itapunguza gharama za bidhaa zetu ambazo tunasafirisha kwenda nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuboresha hii bandari yetu lakini inakabiliwa na ushindani mkubwa sana hasa na bandari za jirani. Ninapendekeza Serikali iangalie namna gani iboreshe TAZARA, TAZARA kwa kiasi kikubwa ni standard gauge; speed ya treni pale ni kilometa 110 kwa saa. Tukiboresha hii ambayo maboresho yake sidhani kama yanahitaji hela nyingi, labda Serikali ijaribu kutuambia ni kiasi gani itaboresha Menejimenti ya TAZARA na vilevile namna gani itaondoa ukiritimba ili TAZARA iendeshwe kibiashara, kwa sasa hivi TAZARA haiendeshwi kibiashara na nina wasiwasi mpaka leo wafanyakazi wa TAZARA wanalipwa na hela kutoka Serikalini, wanalipwa na walipakodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiboresha TAZARA tutakuwa tumejiweka katika position nzuri sana ya kiushindani lakini vilevile tukijenga bandari kavu Mbeya ili mizigo ambayo ni zaidi ya asilimia 70 inayokwenda nchi za nje inapitia barabara hiyo, iondokane na kuharibu barabara zetu. Tukishajenga bandari kavu pale, mbolea zote kwa ajili ya nyanda za juu kusini na mizigo yote ya kutoka Congo, Malawi na Zambia yote isipitie barabara hizo, itue pale ili ipunguze gharama na vilevile itaongeza ushindani. Vilevile ningependekeza tujenge reli ya kuanzia Mbeya kwenda Ziwa Nyasa ili tuwe na ushindani mzuri na Bandari za Msumbiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwenye barabara nilikuwa ninaomba sana Serikali iangalie namna ya kuboresha barabara zetu ambazo zilikuwa ni ahadi za Mheshimiwa Rais, barabara ya Mbalizi – Makongolosi, Mbalizi
– Shigamba – Isongole na barabara ya Isyonje – Kikondo – Makete mpaka Njombe vilevile barabara ya bypass ili iweze kuondoa msongamano wa magari pale Mbeya Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kwenye Kiwanja cha Ndege cha Songwe; hiki kiwanja kimetengewa hela nyingi lakini mpaka leo hatuna taa pale za kuongozea ndege na hakuna uzio. Naiomba sana Serikali iangalie ni namna gani itaboresha Uwanja wa Ndege wa Songwe kwa kuwekea taa za kuongozea ndege vilevile na uzio. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tuna bidhaa nyingi ambazo zinahitajika kwenda nchi za nje kutoka nchi jirani, lakini vilevile kutoka Mbeya yakiwemo maparachichi na matunda mengine lakini yanasafirishwa mpaka Dar es Salaam na haya yana masoko nje. Ukienda kwenye supermarket za Uingereza leo hii utapata bidhaa kutoka Mbeya, lakini zinakwenda kwa gharama kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la fidia, suala la fidia waliopisha ujenzi Uwanja wa Ndege wa Mbeya mpaka leo halijashughulikiwa. Wananchi wale wanalalamika miaka mingi na Mheshimiwa Waziri tumeongea naye mara nyingi na imo kwenye ripoti ya Kamati ya Kudumu ya Miundombinu ambayo nao walipendekeza hawa wananchi walipwe. Ni shilingi milioni 800 tu lakini usumbufu uliopo ni mkubwa na ninashangaa kwa nini wananchi wale mpaka leo wanadhulumiwa pesa zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna wananchi ambao katika ripoti yao walipewa fidia ya shilingi 2000 au shilingi 5000 kwa maheka na maheka. Sasa hili wizara ingeangalia hawa TAA wahakikishe wanawalipa wale wananchi hizo shilingi milioni 800 ambazo wanadai. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala la TARURA, TARURA zinaendana na TANROADS, lakini mgao wa pesa zinazoenda TARURA ni ndogo mno. Kwenye Jimbo langu tuna kilometa zaidi ya 1,000 mtandao wa barabara lakini bajeti yake ni kama shilingi milioni 1.6. TARURA wakiongezewa pesa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, asante sana.