Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Mara nyingi nimekuwa nikieleza hapa kwamba huduma ya simu katika Wilaya ya Rombo hasa maeneo ya Useri, Tarakea, Ukanda wa Chini na Mkuu kuna muingiliano mkubwa sana kati ya mitandao yetu na mitandao ya Kenya hususan Safaricom. Ukiwa Tarakea pale lazima uwe na laini ya huku kwetu Vodacom na uwe na Safaricom.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa nikijibiwa kwamba hii inatokana na mitandao yetu kuwa dhaifu. Sasa ni kwa nini Serikali isifanye mkakati wa makusudi wa kutatua tatizo hili kwa sababu wananchi wanajikuta wameingia kwenye utaratibu wa roaming bila wao kukusudia na matokeo yake wanatumia pesa nyingi sana. Naomba hili sasa lishughulikiwe nipate majibu kwamba tatizo hili litaisha lini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, kuna barabara kutoka Mamsera - Mahida – KNCU - Abiola ambayo ilichukuliwa na TANROADS, ilifanyiwa kazi kwa miaka kama miwili, mitatu hivi, lakini tangu mwaka wa fedha 2014/2015 barabara ile imetelekezwa mpaka sasa haijafanyiwa kazi yoyote. Tunataka kujua TANROADS imeamua kuiachia halmashauri barabara ile au bado iko chini ya TANROADS? Kama bado iko chini ya TANROADS basi ile barabara ishughulikiwe kwa sababu sasa haipitiki hata kwa tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, mimi nilipongeza uanzishwaji wa TARURA kwa sababu nilisema zile barabara za Halmashauri wakati mwingine zilikuwa zinatengenezwa kisiasa kwa Madiwani kila mmoja kuvutia upande wake, lakini fedha zinazotengwa kwa ajili ya TARURA ni ndogo. Jana nilikuwa naongea na Engineer wa TARURA kule kwangu anasema pesa walizonazo wana mkakati wa kutengeneza barabara mbili tu. Sasa nashangaa barabara nyingine za Wilaya nzima zitajengwa namna gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilitaka kusema, sisi Wabunge kazi yetu ni kuisimamia na kuishauri Serikali. Nimekuwa nikisikia malumbano mengi kuhusu Taarifa ya CAG, shilingi trilioni 1.5 na kadhalika. (Makofi)

Mimi nilikuwa nawashauri Wabunge wenzangu tuwe tunasoma hivi vitabu. Mwaka wa fedha wa 2015/2016 CAG alikuja pia na vitabu hapa na akasema mapato ya Serikali yalikuwa ni shilingi trilioni 21.9, matumizi shilingi trilioni 20.2 na akaonesha kwamba kulikuwa na shilingi trilioni 1.088 ambazo zilikuwa zinahitaji maelezo, hayakutoka. Sasa hiki kinachoulizwa sasa hivi tunakijadili kisiasa wakati ni wajibu wetu kuhakikisha kwamba fedha hizi zinaonekana ili hii miradi ya maendeleo ambayo tunapigia kelele hapa iweze kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hayo, hizi sio fedha zetu ni fedha za wananchi. Mimi nawaomba Wabunge wenzangu, tunapojaribu mambo ya kitaifa tuyajadili tukijua kwamba tunajadili kwa niaba ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho napenda kusema hakuna Mbunge yeyote wa upinzani ambaye anakataa ufufuaji wa ATCL, ambaye anakataa miradi inayojengwa ya reli, barabara na kadhalika kwa sababu ziko kwenye Ilani. Tunachokisema hapa ni kwamba tunashauri ufufuaji huu uende kwa namna ambayo baadae Taifa halitapata hasara. Kama ni ununuaji wa ndege basi taratibu zifuatwe, kama ni management, management ziangaliwe, kama ni utengenezaji wa route, route ziangaliwe, hicho ndicho tunachoshauri, lakini hakuna Mbunge yeyote wa upinzani ambaye anasema shirika lile lisifufuliwe au tusitengeneze reli au mradi mwingine wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, infact sisi tunataka maendeleo na hii miradi ikifanikiwa ni kwa faida ya Taifa hili. Moja tu tunalosema, tunatahadharisha miradi hii wataalam wasikilizwe, wataalam washauriwe, ushauri wa kitaalam ukubalike ili Taifa lisipoteze pesa kidogo za wananchi bila sababu yoyote ya msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana mimi namshauri Rais na namshauri tena kwamba Mheshimiwa Rais cha kufanya aagize wataalam wapeleke documents zote zitakazoonesha kwamba shilingi trilioni 1.5 zimetumika na siyo vinginevyo. Hapa hatusemi kwamba kuna mtu kaiba, tunachosema Afisa Masuuli abebe makabrasha yake aende nayo kwa CAG aseme kwamba fedha nimezitumia hivi, CAG afunge hoja, kama Afisa Masuuli atashindwa fukuza kazi.