Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DKT. DAMAS D. NDUMBARO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi hii ili nami nichangie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kutekeleza ipasavyo Ilani ya Chama cha Mapinduzi, hasa katika sekta hii ambayo tunaiongea hivi leo. Ni wazi kwamba Ilani ya Chama cha Mapinduzi na Ilani ya CHADEMA zote zinaongelea kufufua Shirika la Ndege la Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza hilo, Serikali ya Chama cha Mapinduzi kupitia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi imenunua ndege sita. Siyo hilo tu, katika bajeti ambayo Mheshimiwa Waziri ameisoma hapa, kuna viwanja 16 vya ndege ambavyo vitatengenezwa. Viwanja hivi vitasaidia hizi huduma za ndege. (Makofi)

Mheshimwa Mwenyekiti, sisi wengine Majimbo yetu yako mbali sana, umbali wa kutoka hapa Dodoma kwenda Songea ni mkubwa, hizi ndege zitatusaidia sana kufanya mawasiliano. Kama kuna mtu anaona ndege hizi hazimsaidii, basi tuweke bayana kwamba viwanja vya ndege katika Jimbo lake visitengenezwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sisi watu wa mikoa ya kusini tuna kila sababu ya kuipongeza Wizara; Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri, kwa kukamilisha Barabara muhimu sana inayojulikana kwa jina la Mtwara Corridor.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa ukitoka Mtwara unapita Masasi, Tunduru, Namtumbo, Songea, mpaka Mbinga, barabara hiyo imekamilika kwa kiwango cha lami. Kipande kilichosalia cha Mbinga – Mbamba Bay tayari mkandarasi ameshasaini na tunaamini barabara hiyo itakamilika haraka ili kufungua fursa zilizopo katika Kanda ya Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hiyo barabara ya Mtwara Corridor kuna kipande kidogo kimoja kimebaki cha kilometa 11, nayo ni bypass ya Songea Mjini kutoka Kata ya Seed Farm kupitia Kata ya Msamala na hatimaye Kata ya Luwiko. Ili kuhakikisha kwamba Mtwara Corridor inakamilika kwa ukamilifu kabisa, lazima kipande hicho kikamilike. Mheshimiwa Waziri, nimesoma hotuba yako kwa makini sana, sijaona hizo kilometa 11. Hivyo, ni rai yangu kwamba kilometa hizo 11 ziweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango wa usafiri katika Ukanda wa Kusini kuna mpango wa kujenga reli kutoka Bandari ya Mtwara mpaka Mbamba Bay ili kuweza kuhudumia Liganga na Mchuchuma, Miji ya Songea, Miji ya Masasi na miji mingine. Fedha iliyotengwa katika kitabu hiki kwa mradi huu bado ni ndogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wote wa Ukanda wa Kusini wakiongozwa na wananchi wa Jimbo la Songea Mjini wana hamu ya kuiona reli hii ikijengwa, ikifanya kazi, ikitoa huduma na ikiunganisha Tanzania na nchi mbili; ya Msumbiji pamoja na ya Malawi. Kwa hiyo, tunatarajia hili nalo Mheshimiwa Waziri atalichukua alifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Songea, wananchi ambao wameachia maeneo yao wanadai fidia katika upanuzi huo. Naomba kumkumbusha Waziri, Mheshimiwa Profesa Mbarawa na Naibu Mawaziri, kwamba naomba hilo nalo litiliwe maanani ili tuondoe kero hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, niipongeze tena Serikali ya Chama cha Mapinduzi, naomba kuunga mkono hoja.