Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuishukuru Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri ambazo imeendelea kuzifanya. Serikali yetu kupitia Wizara hii imekuwa ikitenda haki. Niseme kabisa kwamba hata katika Wilaya yetu ya Mbogwe TANROAD kwa maana ya Mkoa wa Geita chini ya uongozi wa Meneja wa Mkoa, Bwana Haruna Senkuku na Wasaidizi wake wamefanya kazi nzuri sana katika kuhakikisha kwamba Wilaya yetu mpya ya Mbogwe inapata barabara za Mkoa na kuifungua katika upya wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo hiyo barabara kutoka Butengoromasa kupita Iparamasa - Mbogwe mpaka Masumbwe. Barabara hii tumeomba ikapandishwa hadhi na zaidi sana tunaomba Wizara iendelee na mchakato wa kuweza kuifanyia usanifu wa kina na upembuzi yakinifu ili kusudi ikiwezekana iweze kujengwa kwa kiwango cha lami ili kuweza kufungua mawasiliano ya muda wote wakati wa masika na wakati wa kiangazi, barabara hii iweze kupitika kwa urahisi na kuweza kuleta maendeleo kwa wananchi wa Wilaya ya Mbogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisemee pia kuhusu barabara iliyopandishwa hadhi ya kutokea Ushirombo kwenda Makao Makuu ya Wilaya ya Mbogwe kuelekea Mkoani Geita. Hapa namwomba Mheshimiwa Waziri atusikilize vizuri kwa maana ya kwamba barabara hii tulikuwa tumeomba ichukuliwe na TANROAD kutoka Ushirombo kupita Bwera kwenda mpaka Wigo ambapo barabara hii inakutana na barabara ya kutoka Kahama kwenda Geita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, TANROAD wamechukua sehemu ya barabara hii. Sasa nikaiomba Wizara, kwa nini isitusaidie kuchukua tena hiki kipande cha kutokea Iboya kwenda Wigo ili kusudi barabara hii iwawezeshe Wanambogwe kwenda Mkoani Geita Makao Makuu ya Mkoa wetu wa Geita?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba tu Mheshimiwa Waziri atumie wataalam wake waende kukagua hii barabara, ikiwezekana basi ikamilishwe kwa sababu imechukuliwa kipande kwa kupitia Bodi ya Barabara ya Mkoa wa Geita. Tulikuwa tumeomba hii barabara ipandishwe lakini Wizara kwa busara zao wamechukua nusu. Tunaomba tu Wizara ichukue hatua za ziada ili kuweza kuikamilisha hii barabara, itakuwa imefanya jambo la msingi sana.

Mheshimwi Mwenyekiti, naomba pia Wizara itutazame tena kwa upya ili Mkoa wetu wa Geita uweze kuunganishwa na Mkoa wa Tabora kupitia Wilaya ya jirani kwetu kwa ndugu yangu, Mheshimiwa Elias Kwandikwa. Huyu ni jirani yangu na naomba sasa kwa kweli waangalie uwezekano wa kutupandishia hii barabara kutoka Masumbwe kupitia Ushetu kwenda Kaliua mpaka Urambo. Hii barabara itatusaidia sana Wana-Geita kuweza kuunganishwa na Mkoa wa Tabora na Katavi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naamini kabisa kwamba kwa uangalizi mzuri wa Mheshimiwa Profesa Mbarawa, barabara hii itapandishwa na itatusaidia sana katika kuhakikisha kwamba Mkoa wetu Mpya wa Geita na wenyewe unaenda kwa kasi katika nchi yetu hii ambayo tunaitarajia kuwa nchi ya viwanda katika muda mchache ujao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tena kuhusiana wa ukurasa wa 33 wa Hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Kuna utaratibu wa kujenga daraja la Busisi Kigongo. Daraja hili liko katika barabara ya Geita Usagara. Daraja hili kwa kweli endapo Serikali itafanikiwa kulikamilisha, naamini kwamba barabara hii ya kutoka Geita - Kagera mpaka Musoma Mkoani Mara, itakuwa ni ufumbuzi mkubwa sana katika suala zima katika ukuzaji wa uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini kwamba daraja hili endapo Mungu akitujalia likakamilika litakuwa ni sehemu ya Utalii, maana ni sehemu ambayo kwa kweli kimsingi ujenzi ukikamilika litakuwa ni la aina yake, kama ambavyo sasa hivi kuna daraja hilo la Kigamboni, hata hili la Kilombero pamoja na daraja la Mkapa, yamekuwa ni madaraja ambayo ni ya mfano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu wazi kwamba habari ya Wizara hii siyo ya kubahatisha. Kikwetu huwa tunasema hii ni Wizara ya mashikolomageni. Hii Wizara ni ya vitu vipya. Wizara hii imekuwa ikituletea flyovers, madaraja ambayo hayajawahi kuonekana katika Afrika Mashariki na Kati. Kwa hiyo, nawaombea Mungu aendelee kuwapa ujasiri, waendelee mbele, watutendee haki kwa kututoa kimasomaso.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku za nyuma tulikuwa tunaonekana kama watoto yatima, nchi kubwa kama Tanzania inakosa ndege. Kwa maana hiyo, kwa kweli tulikuwa tunadhalilika, wakati mwingine tunapita nchi jirani ya Kenya kwenda Dar es Salaam. Unatoka Mwanza unakwenda Nairobi, halafu ndiyo unakwenda kuzunguka kwenda Dar es Salaam. Ilikuwa ni aibu kubwa. Kutokana na ujasiri wa Wizara hii pamoja na wakala mbalimbali akiwemo Bwana Mfugale, Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema jambo hili kwa nia njema kabisa na ninaamini kila Mtanzania mwenye nia njema atawaombeeni kwa Mungu ili kusudi kwa kweli wapate thawabu hata siku ya mwisho, maana wanatuletea mambo mapya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala zima la ujenzi wa reli ya standard gauge. Hatua iliyofikiwa na Serikali ni nzuri na niseme tu kwamba hata ile reli ya kutokea Isaka kwenda Kigali Rwanda mpaka Msongati, naomba Mheshimiwa Waziri wetu aiangalie reli hiyo na yenyewe iweze kuchukuliwa hatua tuone mwelekeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tunayo reli ya kutokea Dar es Salaam mpaka Arusha pamoja na Mkoani Mara, Serikali ilione hilo ili nchi yetu iweze kupiga hatua kwa hatua, kwa maana kwamba kuwe na balance ya maendeleo sehemu katika mbalimbali za nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.