Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Issaay Zacharia Paulo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Basi, naomba nitumie dakika kumi pia. Kwanza nachukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kutujalia nafasi hii ya uwepo wetu hapa na jinsi ambavyo ametulinda hadi leo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, natoa shukrani za dhati kwa Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kutoka kwake Rais, Makamu wake, Waziri Mkuu na Mawaziri wote kwanza kwa kazi kubwa wanayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitachangia kwa staha sana. Kwanza nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri zaidi ya 14 waliofika Mbulu, lakini walipita katika barabara ya Magara na leo daraja la Magara linajengwa kwa fedha nyingi za Tanzania. Pia barabara zote za TANROADs; nawapongeza Watendaji wote wa TANROADs kwa jinsi ambavyo wanahangaika katika barabara zetu za Wilaya ya Mbulu, wakati wote kunapitika na wanajitahidi kufanya kazi hii mara mbili kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nina maombi Serikalini. La kwanza, naishukuru pia kwa mnara kule Nambisi umefunguliwa, Tarafa ambayo haikuwa na mawasiliano toka zamani na sasa wananchi wa Tarafa hiyo wamepata mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba mambo machache. La kwanza, naungana na Waheshimiwa Wabunge wote ambao walikuwa wanatetea fedha za Mfuko wa Barabara, TARURA wapewe asilimia 50 na Serikali Kuu 50, vinginevyo basi hata tutafute namna ya vyanzo vingine vya kusaidia TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu barabara zilizopokelewa na TARURA zimekuwa na jiografia ya maeneo magumu sana. Maeneo mengine ni yale yenye makorongo katika maeneo ya vijijini. Kwa mfano, kwenye Jimbo langu la Mbulu Mjini, kuna makorongo ambayo yanahitaji madaraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, korongo moja linaweza kuwa bajeti ya TARURA kwa Halmashauri yangu au kwa Jimbo langu la Mbulu Mjini. Sasa hawezi kufanya daraja au kivuko na maeneo hayo yamekuwa kikwazo katika huduma za jamii za afya, elimu na huduma nyingine za kijamii. Kwa hiyo, tunaomba sana, pengine ikiwezekana hata madaraja ya chuma kusaidia kwa namna gani kwa sasa maeneo haya kwa nchi nzima yanapata muunganiko wa kupata mtandao wa barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua nyingine pia, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, kila mwaka ametupa kilomita moja ama mita 500 katika mlima Magara. Waheshimiwa Mawaziri, ni mashahidi waliofika Mbulu, waliopita barabara ya Magara. Barabara ile kwa jiografia haipo Tanzania nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri zile kilomita moja au moja na nusu unayotoa kwa kilomita kama 40 inaweza kuwa takriban miaka kadhaa, wananchi wale wasihudumiwe kwenye hilo eneo. Kwa hiyo, tunaomba kwa bajeti ya mwaka huu kwa fedha walizotenga japo ni kidogo lakini watupe; na mwaka unaofuata watupe hata angalau kilomita tano za mlima ili mlima ule uweze kupitika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni barabara ya Karatu – Mbulu – Haydom mpaka Sibiti. Majimbo yanayopitiwa na barabara hii ni zaidi ya sita. Tunaomba sana Serikali itusaidie ni kwa namna gani barabara hii inapewa fedha mara moja kwa ajili ya usanifu ulioandikwa kwenye kitabu hiki, lakini na baadaye mpango wake wa kufanyiwa kazi kwa kiwango cha lami. Barabara hii inatoa huduma kwa Majimbo yasiyopungua sita au saba. Pia ina miji midogo takribani kama arobaini na kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Wakurugenzi wa Benki ya Ujerumani walikuwa wanasema barabara hii ni barabara muhimu, inapita kwenye miji mingi na jamii nyingi. Kwa hiyo, tunaomba sana kwa jinsi ambavyo Mheshimiwa Waziri ameandika kwenye kitabu hiki, lakini hakuna fedha zilizowekwa zaidi ya kuwategemea wahisani wa KfW. Kwa hiyo, tunaomba ili mtandao wa barabara katika eneo hili la bonde na juu ya Bonde la Ufa kwa maana ya Karatu, Mbulu na Haydom uweze kupatikana kuunganisha mikoa kama mitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo naomba sana kama ambavyo nimezungumza, ni ahadi za Mheshimiwa Rais. Tuna miaka mitatu sasa, katika ahadi zile za Mheshimiwa Rais, kwa mtandao wa barabara za TANROAD na Serikali Kuu, watusaidie kutekeleza zile ahadi ili ziweze kupungua kwa maeneo yote ya nchi nzima na tunajua ni maeneo makubwa sana ambayo tayari yana matatizo makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni eneo la minara. Sasa hivi kuna haja ya Mheshimiwa Waziri kufanya ziara kwa maeneo ambayo hajaenda, lakini pia kuchukua taarifa ya wataalam ambayo inaonesha ni maeneo gani hayana mawasiliano. Juzi Mheshimiwa Waziri alikuwa anatuhoji na kutuambia kila Mbunge yale maeneo ambayo yeye anaona ili alinganishe na yale ya Wizara kama yanafanana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawapongeza sana kwa mpango huu wa kushirikishana mawazo na kupokea mawazo ya Waheshimiwa Wabunge. Hata hivyo, niseme tu kwamba kumekuwa na desturi ya taasisi hizi zinazoweka minara kuweka minara mahali pamoja katika ushindani ule wa kukimbilia eneo moja. Basi Serikali isiwe inaruhusu uwekaji wa hiyo minara kwa maeneo yale. Tunaomba sana katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia barabara za miji Mikuu kama Dodoma. Sisi tunaoishi katika eneo hili la Mji wa Dodoma kuja Bungeni imekuwa tabu sana na kwenda kwenye maeneo tunayoishi. Tunaomba hata uchongaji wa kawaida wa barabara za changarawe, maeneo yote ambayo hayajafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme hili kwa sababu siku moja nilikuwa nasafiri asubuhi lakini gari lilifunga njia nikawa nimechelewa usafiri ule wa kwenda na Waheshimiwa Wabunge wenzangu. Kwa hiyo, inaonekana kwamba barabara hizi za Dodoma zinahitaji upanuzi wa kina na namna ambavyo uchongaji utawekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili la Dodoma linahitaji sasa ongezeko la alama za wapita kwa miguu. Magari yamekuwa mengi, wapita njia wamekuwa wengi, tumehamia kwenye huu mji kwa wingi wetu. Kwa hiyo, kuna haja ya wataalam kupitia upya mfumo mzima wa barabara za Dodoma ili ziweze kuwekewa alama kwa jinsi itakavyowezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nimwombe sana Mheshimiwa Mbarawa, kama Waziri mwenye dhamana, naomba anisikilize; yeye na Naibu Mawaziri wote, Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii, aje Mbulu apite barabara ya Magara aone jinsi ambavyo barabara hii inahitaji sana jitihada za haraka za Serikali ili iweze kutafutiwa ufumbuzi hasa eneo la Mlima kwa kiwango cha zege kwa sababu ni hatari sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale Mawaziri waliopita kwenye vikao vya Baraza la Mawaziri, wawe Mabalozi wetu wazuri kuizungumzia barabara hii ya Mbulu - Magara hadi Mbuyuni, kwa maana ya barabara ya Magara kwa sababu jiografia yake ni hatarishi na wananchi hawataacha kwa sababu ina ufupi wa kwenda Mkoani Manyara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, eneo hili Mheshimiwa Waziri aji-commit wakati anatoa mrejesho wake, atueleze anakuja lini Mbulu ili aone jinsi ambavyo tuna mahitaji makubwa na jiografia yake haipo katika Tanzania nzima kwa sasa? Japokuwa eneo hili ni eneo fupi, lakini ni tete na hatarishi. Viongozi wote, Mawaziri wote wale 14 waliopita pale walikuwa wanasema Mheshimiwa Mbunge pole sana, kwa kweli hatukujua wakati wote ulikuwa unapiga kelele na kulalamika Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru kwa ujenzi wa daraja na hata kwa hizo kilomita chache wanazoweka Mlimani, ila watuongezee kwenye bajeti, ninyi Mawaziri na Naibu Mawaziri wake wote wawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, tunaishukuru sana Serikali na tunawatakia kazi njema. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.