Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nianze kuchangia Wizara hii muhimu kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu na wananchi wetu na eneo la kuunganisha mikoa yetu kwa barabara za lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sera ya makusudi iliyokuwa imefikiwa ili makao makuu ya mikoa yote yaweze kuunganishwa kwa barabara za lami. Kamati kwenye hotuba yake imesema vizuri sana iko zaidi ya mikoa 15 ambayo bado haijaunganishwa. Niunganishe kwenye orodha ile Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Manyara haujaunganishwa na Mkoa wa Arusha na Mkoa Mara haujaunganishwa. Malengo ya sera hii ilikuwa ni mwisho iwe 2017/2018, leo tunaingia 2018/2019 karibu robo ya mikoa haijaunganishwa, nadhani tunapaswa kuongeza kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ni ukweli kwamba bado kuna barabara nyingine ndogo ndogo labda ndani ya wilaya, barabara za kwenda hata kwenye vitongoji, hata njia za ng’ombe zinawekwa lami lakini mikoa bado haijaunganishwa. Kama kweli tumedhamiria kuunganisha mikoa hebu tuanze kufanya kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kuunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu ni barabara ya Oldeani Junction - Mang’ola - Matala - Mwanhuzi. Barabara inayosemekana ya Karatu - Mbulu – Haydom - Mto Sibiti - Mwanhuzi hiyo ni barabara nyingine na barabara hizi zote mbili zina umuhimu wake tusichanganye. Pale Mang’ola ambako barabara hii inapita kuna gesi muhimu sana ya helium ambayo imegundulika, utaisafirisha kwa barabara hii ya Oldeani Junction - Mang’ola - Matala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kama ni kweli hiyo reli wanayoisema ya Tanga – Arusha - Musoma itajengwa hiyo ndiyo barabara ya kupitishia vifaa vya ujenzi. Kwa hiyo, barabara ya Oldeani Junction - Mang’ola ni barabara muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, pale Mang’ola kila siku inayotoka kwa Mungu kuna tani 150 za vitunguu maji vinasafirishwa kuja Arusha. Kwa hiyo, ni barabara ambayo naomba isiachwe kwa sababu tu tunasema barabara ni hii ya Karatu – Mbulu – Haydom, hiyo ni barabara nyingine na ni muhimu na kila barabara ina umuhimu wa aina yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niende kwenye eneo la uwanja wa ndege, nashukuru Benki ya Dunia imeweka hela na naamini itakuja kwa ajili ya upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Lake Manyara. Wananchi wako tayari, miaka miwili imepita Wizara wameshaweka alama za uwanja lakini mpaka sasa hivi wananchi hawajui kinachoendelea. Kwa kuwa fedha zile zimetengwa na nina uhakika ni fedha za uhakika basi waende wakawaambie wananchi juu ya kile ambacho kinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo pia kuhusu Uwanja wa Ndege wa Songwe ni muhimu sana kwa maendeleo ya Nyanda za Juu Kusini. Hata hivyo, uwanja huu haukamiliki zaidi ya miaka 10, kuna tatizo gani? Tumetoka juzi pale Kamati ya Uwekezaji ya Mitaji ya Umma, mambo yanayoendelea kwenye Uwanja wa Ndege wa Songwe ni aibu. Mkandarasi ameshabadilishwa zaidi ya mara tatu, hivi taratibu za manunuzi ya hawa wakandarasi zikoje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkandarasi wa kwanza hovyo, wa pili hovyo, wa tatu naye ameshamaliza pesa kazi imesimama, tunawateuaje hawa makandarasi? Mkandarasi wa mwisho huyu Shapriya ameshindwa kumaliza kazi lakini ameshalipwa fedha zaidi ya shilingi bilioni 1.4. Wanawezaje kumpa mkandarasi fedha ambazo siyo za kwake na leo ameshindwa kufanya kazi? Kwenye kitabu wametenga shilingi bilioni tatu ya kwenda Songwe, huyu mtu aliyechukua hii shilingi bilioni 1.4 wana mpango gani naye? Pana shida kubwa sana pale Mbeya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo kuhusu reli. Tunashukuru sana, ni mkakati mzuri lakini tusiishie kwenye reli ya kati. Hii reli inayosemwa ya Tanga – Arusha - Musoma imekuwepo tangu mimi niko mtoto wa shule. Kila siku upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na mabilioni yanakwenda. Kuna hiyo reli ya Kusini, yuko mwenzangu amesema kama inawezekana na kama tuna sifa hebu twendeni tukakope ili hizi reli zote zikajengwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Waziri atusaidie, alikuja mbele ya Bunge hili akasema deni la Taifa limekuwa kubwa kwa sababu pia tunakopa fedha za ujenzi wa reli ya standard gauge lakini pia kuna kauli inasema…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. QAMBALO W. QULWI: Tunajenga kwa fedha za ndani, hebu atuambie kauli ya Serikali ni nini juu ya ujenzi wa reli hii?