Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwa dakika tano hizi nitajikita kwenye maeneo mawili. Kwanza kabisa nipende kupata kauli ya Serikali kupitia kwa Mheshimiwa Waziri, ni suala ambalo tumekuwa tukilishughulikia mara kwa mara. Tuna kivuko kinachounganisha Kisiwa cha Ukerewe na Kisiwa cha Ukala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kivuko hiki kinahudumia zaidi ya wananchi 50,000, kimekuwa kinaleta shida mara kwa mara na nimekuwa nawasiliana na Wizara. Sipendi siku moja tuje hapa kuomba rambirambi kwa sababu ya wananchi waliozama katika kivuko kile. Naomba nipate kauli ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka jana tumeahidiwa kwamba mpaka mwezi Desemba mashine mbili zilizokuwa zimeagizwa zingefungwa kwenye kivuko kile lakini mpaka sasa hakuna kinachoendelea. Niombe kauli ya Serikali mashine kwa ajili ya kivuko cha MV Nyerere kinachofanya kazi kati ya Bugolola na Ukala zinafungwa lini na kivuko hiki kiweze kuwa katika utendaji kazi mzuri na ulio salama kwa wakazi wa eneo lile?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine katika maeneo hayo hayo ya vivuko tuna Kisiwa cha Ilugwa. Wananchi wanasafiri zaidi ya masaa manne kuja Ukerewe. Wana-risk sana, wanasafiri kwa kutumia mitumbwi. Serikali ina mkakati gani kutupatia kivuko kwa ajili ya eneo lile?

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nataka nichangie ni juu ya Kampuni ya Huduma za Meli. Kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 75, anaongelea juu ya kampuni hii. Mwaka 1999 kampuni hii ilibinafsishwa, lakini baada ya kubinafsishwa na kukosa watu wa kuichukua iliendelea kufanya kazi. Bahati mbaya sana kwamba vile vifaa na mashine kwa ajili ya matengenezo vilibinafsishwa lakini wale watumishi waliobaki kwenye kampuni hii walijikongoja wakaendelea kufanya kazi pamoja na kwamba kulikuwa na matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ni nini, watumishi hawa waliobaki wakiwa wanafanya kazi kwenye kampuni hii wana miezi 23 sasa hawajalipwa mishahara. Hebu tuweze kutafakari kama ni sisi hawa watumishi wanaweza kuishi vipi? Inawezekana kweli kuna watu wamefanya vibaya kwenye kampuni ile, lakini basi Serikali iweze kufanya uchambuzi; ina vyombo vyake; ijue ni watu gani hawajafanya vizuri, watu gani wamehujumu kampuni ile na wasio na makosa waendelee na kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kukaa na watumishi miezi 23 hawajalipwa mishahara halafu tutegemee waendeshe kampuni hii wakiwa na tija na ufanisi, si kweli. Wakati wanasikia kwamba kuna trilioni moja sijui point tano imepotea halafu wao miezi 23 hawajalipwa mishahara hawawezi kuelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni muhimu sana Serikali iangalie namna gani ya kufanya watumishi hawa wapate haki yao ili waweze kufanya kazi katika mazingira yaliyo salama. Ni jambo jema kwamba sasa tuna Mtendaji Mkuu, Mkurugenzi ambaye wamemteua mwaka jana, ni mtu makini, mchapakazi, mbunifu, basi Serikali impe support.

Mheshimiwa Mwenyekiti, badala ya kumteua kumpa kampuni ile ambayo ilikuwa inaelekea kufa halafu wakam- dump wakamtelekeza pale hawatakuwa wamemsaidia, wampe nguvu, wamtie moyo, wampe msaada wa karibu ili aweze kusaidia kwenye kampuni hii ili iweze kufanya kazi kwa sababu ni kampuni muhimu sana kwa usafiri unaounganisha Ukerewe, Mwanza lakini na maeneo mengine; Ziwa Tanganyika, Ziwa Nyasa, basi Serikali ifanye kile ambacho inapaswa kufanya wafanyakazi hawa waweze kulipwa mshahara wao waweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.