Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Zainab Mndolwa Amir

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZAINABU M. AMIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kutoa mchango wangu. Awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunipa afya njema ili nami niweze kuchangia katika hotuba hii ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi yake nzuri anayoifanya pamoja na Naibu Mawaziri wake na wafanyakazi wa Wizara wote kwa ujumla. Nampongeza kwa sababu tunaona msongamano Mkoani Dar-es-Salaam umepungua kwa kupata mwendokasi na sasa hivi katika bajeti hii nimeona barabara mbalimbali zimetengewa bajeti ya matengenezo ili kuepuka msongamano huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kuna changamoto nyingi zinajitokeza. Bajeti hii imepangwa na kwenye vitabu inaridhisha na inaonekana ni nzuri sana, Dar- es-Salaam ni uso wa nchi yetu kwa sababu watu mbalimbali wanavyotoka nchi za nje hufikia Dar-es-Salaam na baadaye ndio wanakuja mikoani, kwa hiyo, naomba bajeti iliyotengwa ifike kwa wakati. Vilevile tunamwomba sana Mheshimiwa Waziri atutafutie wakandarasi ambao wana kiwango cha hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona barabara yetu ya Kilwa ilitengenezwa chini ya kiwango baada ya muda mfupi imeharibika na hapa tumeona pia itatengenezwa kwa mwendokasi. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri mkandarasi atakayempata aiboreshe ile Barabara ya Kilwa iwe yenye ubora kwa sababu ilitengenezwa mara ya mwanzo lakini haikuwa nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuzungumzia kuhusu Kivuko cha Magogoni. Ni muda mrefu sana wananchi wa Dar es Salaam, hususan waishio Kigamboni walikuwa na tatizo la kivuko na msongamano wa magari lakini tunashukuru Serikali ikatujengea Daraja la Nyerere. Napenda kueleza Bunge lako Tukufu, wananchi wa Kigamboni bado wana changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili uvuke katika daraja lile kwa gari ndogo tu ni shilingi 2,000 ukizingatia wananchi wake wengi shughuli zao zote ziko ng’ambo ya bahari, lazima wavuke asubuhi wawapeleke watoto shule, ofisi nyingi ziko ng’ambo ya bahari, hospitali pia, changamoto ni nyingi na kwamba ni ghali mno kuvuka katika daraja lile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa gari ndogo ni Sh.2,000, mtu akivuka tu kwenda na kurudi Sh.4,000. Wakati mwingine watu pia wanakuwa na wagonjwa hospitalini wanaenda mara tatu kwa siku, gharama ya kivuko ni kubwa mno Mheshimiwa Waziri. Namwomba pamoja na Wizara ya TAMISEMI, ingawa nilishauliza swali hili kwamba NSSF nao walijenga lakini ninachokiona kwa Daraja la Kigamboni, wananchi wa Kigamboni wamepewa mzigo mkubwa sana. Hawana faraja na lile daraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulijua kwamba wananchi wa Kigamboni wamepata faraja kwa uwepo wa daraja lile angalau watavuka labda kwa bei nafuu, lakini kwa bei ya Sh.2,000 kwa gari ndogo na gari kubwa mpaka Sh.7,000 mpaka Sh.15,000 ni ghali mno. Naiomba Wizara hii kwa kushirikiana na TAMISEMI waliangalie hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi imefikia wakati wananchi wa Kigamboni ambao wanatumia vyombo vya moto, magari yao hawavuki nayo. Ukienda katika Kata ya Kigamboni utakuta watu wengi wameweka parking za magari, anaweka gari lake anavuka kwa panton kwa shilingi 200, anaenda kufanya shughuli zake mjini kisha anarudi analipa shilingi 1,000. Kwa hiyo, anakwepa kuvuka kwenye daraja kwa sababu ni ghali mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba wafanye utaratibu kabisa, Mheshimiwa Dkt. Ndugulile analifahamu hili, wananchi wa Kigamboni wanafurahia daraja, lakini daraja lile halina neema kwao. Wanasema maisha bora kwa watu wa Kigamboni kwenye daraja lile hayapo ni ghali mno. Kwa sababu, hata kama ni mshahara Sh. 4,000 mtu anavuka kila siku kwenda na kurudi, mwisho wa mwezi aki-calculate ina maana unaishia kwenye usafiri. Nadhani katika madaraja yote Tanzania ni Daraja la Kigamboni tu ambalo watu hutozwa nauli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulitegemea kwamba watu wa Kigamboni watapata neema kwa sababu madaraja ni huduma kama huduma nyingine. Kama ni masuala ya kukusanya kodi basi lile daraja lingejengwa Ruvu au Wami kwa sababu ni magari mengi sana yanapita maeneo hayo na Serikali ingekusanya kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachokiomba Mheshimiwa Waziri, naona ananitazama lakini naomba aandike haya ninayozungumza na ayazingatie akishirikiana na TAMISEMI, wawaonee huruma wananchi wanaoishi Kigamboni kwa sababu daraja lile halina manufaa kwao, ni ghali mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wapunguze na ikiwezekana wavuke hata kwa kutumia smart card, hata kama wakiambiwa shilingi 10,000 kwa mwezi au shilingi 20,000 hata mtu akivuka mara tano mara kumi lakini ana kadi maalum ili kupunguza gharama ile. Wakati mwingine wanashindwa kabisa magari yao huacha ng’ambo na kwenda kwa kutumia panton. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kuchangia kuhusu barabara zetu. Tumeona Serikali imejitahidi kwa kiwango kikubwa na imeona jambo la muhimu barabara ya Dar es Salaam – Morogoro na sisi ni mashahidi tunapita kila siku katika barabara zile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku moja niliuliza hapa kwamba ni lini Serikali itafanya mkakati wa kukarabati barabara zetu na mojawapo ni eneo korofi sana la Chalinze hadi Mlandizi. Nikajibiwa kwamba eneo lile ni korofi kwa sababu inapita mizigo mizito lakini mimi ninachosema siyo mizigo mizito tu pia kiwango cha barabara ni cha hali ya chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani mkandarasi aliyejenga maeneo yale hakuzingatia eneo lenyewe husika labda lina maji ya aina gani ili atumie material husika. Kwa sababu kama ni mzigo mzito umetokea Kurasini bandarini, ukapita barabarani ukafika mpaka Mlandizi pale barabara angalau ni nzuri, lakini kutoka Mlandizi mpaka Chalinze ile barabara ni mbovu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo suala la mzigo mzito kwa sababu mzigo ni uleule uliotoka bandarini na ndiyo uleule uliopita katika eneo lile na ndio uliofika Chalinze na kwenda Chalinze ukaenda Morogoro au Tanga na barabara kule ni nzuri. Kwa hiyo, hapa tatizo ni wakandarasi wetu, wanajenga barabara chini ya viwango. Namwomba Mheshimiwa Waziri pindi atakapoanza kutengeneza hizi barabara atafute wakandarasi wenye viwango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuwawekee masharti hawa wakandarasi, ikiwa watajenga barabara chini ya kiwango na ikifikia muda fulani na tumewalipa pesa, kwa pesa zao wenyewe waweze kugharamia barabara zile kwa maana kwamba wazitengeneze kwa fedha zao kwa sababu wanapewa fedha lakini barabara ziko chini ya kiwango na kuipa Serikali hasara kila mara kwenda kukarabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona katika taarifa hii kwamba barabara ya Chalinze mpaka Mlandizi kuna kilometa kama 12 zimeshaanza kukarabatiwa toka Machi lakini mimi napita mara kwa mara, ukarabati unaofanyika pale ni kuziba viraka. Kuziba viraka siyo kwamba ndiyo unatengeneza barabara, barabara ile ina mabonde kama matuta ya viazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotakiwa ile barabara ijengwe kwa kiwango hata kama ni cha zege ili kuhimili mizigo mizito inayopita. Kwa sababu wanakarabati kwa kuweka viraka kusema ukweli bado tutapiga mark time, bado hatujatengeneza barabara zetu. Naiomba Serikali, kama mnavyosema Serikali hii ni sikivu, iwe sikivu kweli, haya yaliyoandikwa yatekelezwe kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara nyingi zina matatizo pia. Kuna barabara ya kutoka Magole - Gairo ni mbovu. Mnaona maeneo ya Magubike tukipita barabara ni mbovu, naomba Serikali yetu pia itengeneze barabara hizo. Barabara nyingine ziko kwenye kingo za milima angalau Serikali wakati wanajenga zile barabara kuu zile waweke pavements ili wakati wa mvua kubwa mmomonyoko usiathiri barabara zetu na kuleta matatizo.

Kwa hiyo, haya aliyoyaandika Mheshimiwa Waziri katika kitabu hiki ni mazuri lakini changamoto zinakuja utekelezaji upo? Serikali itoe fedha kwa wakati na wakandarasi wanaoomba nawaomba wazingatie ubora na viwango vyao ili waweze kutengeneza barabara zetu ziwe za viwango na siyo kutengeneza barabara ili mradi barabara tu na kuipa Serikali hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Waziri haya yote yaliyoandikwa yawe yanatekelezeka maana nimeona Waheshimiwa Wabunge wenzangu wengi hapa wamechangia wakisema kwamba mambo mengi yalikuwepo bajeti zilizopita lakini mpaka leo ni ahadi tu kwenye vitabu lakini utekelezaji wake ni wa chini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Waziri, Mheshimiwa Profesa Mbarawa, kama ni Serikali sikivu aishauri iweze kukarabati na kujenga barabara zetu kwenye kiwango kinachohitajika ili kuepuka ukarabati wa mara kwa mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Mbarawa, kama ni Serikali sikivu naomba aishauri iweze kukarabati na kujenga barabara zetu kwenye kiwango kinachohitajika ili kuepuka ukarabati wa mara kwa mara. Ukarabati huu wa mara kwa mara huipa Serikali hasara pia na badala ya kwenda mbele tunarudi nyuma. Badala ya kujenga barabara nyingine, tunarudi kujenga barabara ambazo zilishajengwa na zimejengwa chini ya kiwango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo nashukuru sana kwa mchango huu namwomba Mheshimiwa Waziri yatekelezwe kwa wakati na Serikali itoe fedha kwa wakati kama ilivyoahidi na kama ilivyoandika ili barabara zetu ziwe za kiwango.