Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chifu wetu nikushukuru kwa kunipa fursa hii ambayo naitafuta muda mrefu, mambo yanakuwa magumu hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile sikuwahi kuzungumza toka tumeanza Bunge hili la bajeti, naomba nitoe maneno ya utangulizi juu ya amani kwa Watanzania wote. Suala la amani Waheshimiwa Wabunge si jambo la kikundi fulani au si jambo la Wabunge peke yake amani, dhamana ya amani ni ya wananchi na Watanzania wote. Tunafanya makosa sana kudhani sisi wanasiasa ndiyo wenye dhamana ya amani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi niseme wazi mimi sikufurahishwa na mjadala wa kuwajadili viongozi wa dini. Sisi ni sehemu yake na wao ni sehemu yetu. Kila wakati viongozi wa dini wanatuhubiri tuache mambo mabaya, mnaambiwa muache kuzini, wizi, rushwa mnashangilia lakini mkiambiwa jambo linalogusa mambo yenu mengine mnakuja juu. Tumerogwa na nani Watanzania kudhani kwamba viongozi wa dini wanachokisema ni cha uongo? Leo hii unakwenda unanyenyekea kwa jina la Baba, la Mwana na la Roho Mtakatifu, lakini ukiambiwa jambo hili halifai, unakuja juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania tuache kwani wao ni sehemu yetu. Mbona sisi tukifanya humu tunakuwa wakali na kupelekana Kamati ya Maadili, wapi sasa wao watajadili, wao hawana Kamati ya Maadili, wao kupitia majukwaa ya Makanisa na Misikiti ndiyo uongozi tulionao. Kila siku tukipata mafanikio tunakwenda kunyenyekea kuombewa. Hakuna mtu humu hajaombewa baada ya kupata Ubunge hapa, lakini leo viongozi wetu wa dini tunawabeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili sijalifurahia kabisa na mimi niko tayari kutokuelewana na wengine. Najua 2020 tutakutana huko tukiwaombeeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, kwanza hii habari ya dakika tano mimi niseme tu sikubaliani nayo, muda mdogo sana huu kueleza mambo mbalimbali ya majimbo yetu na nianze na ujenzi wa barabara ya Urambo – Kaliua. Barabara hii ina kilomita 28 na inajengwa na mkandarasi mzalendo. Mimi nasema huyu mkandarasi mzalendo hana uzalendo. Haiwezekani karibu miezi nane anashughulika na usafi tu kama wa kilomita mbili. Mimi ningekuwa mwamuzi leo tunamnyanga’anya kazi hii. Hatuwezi kukaa na mtu ambaye uzalendo wake una mashaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina nia njema tu kwamba kilomita chini ya 30 tuwape wazawa wafanye kazi lakini kazi zenyewe hawafanyi. Magari kutoka Kigoma na sehemu nyingine yanazama eneo la tukio mkandarasi yupo pale wala hajali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkandarasi gani hana uwezo hata wa kujenga kambi? Mvua zinanyesha za kwao, kila jambo baya wao, wapo pale. Mheshimiwa Waziri alikuja hawajali kabisa habari ya Waziri, wana kiburi kutoka wapi? Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri na Naibu Mawaziri, wananchi wa Wilaya ya Kaliua wamechoshwa na jambo hili. Hatuwezi kukubali, tutafanya utaratibu tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisema tofauti mnanielewa, kama hawezi sisi tutatafuta njia ya kumfanya asifanye kazi na tuko tayari kwa lolote hatuwezi kuvumilia. Kwa hiyo, tunataka sasa baada ya bajeti hii tuone mabadiliko pale na mimi kila siku napita pale pamoja na kwamba njia siyo nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani suala la amani kila mmoja alizingatie, wote tuwe na dhamana ya amani. Ahsante.