Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Zainab Mndolwa Amir

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZAINAB M. AMIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mheshimiwa Ummy A. Mwalimu (Mbunge) pamoja na Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile (Mbunge) kwa juhudi kubwa wanazofanya katika kutekeleza majukumu yao kwa weledi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali iondoe malipo katika hospitali za Serikali kwa maiti ambazo zimehifadhi wa katika vyumba vya kuhifadhia maiti kwa kuwa wakati wa uhai wao walikuwa wanachangia Pato la Taifa kwa kulipa kodi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, watoto wote walio chini ya miaka mitano wapate huduma za afya bure kama ilivyo kwa wazee.

Mheshimiwa Naibu Spika, dawa za ugonjwa wa saratani ni ghali mno, hivyo nashauri Serikali ipunguze bei ya dawa hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kwa wale wagonjwa wasio na uwezo wa matibabu ya moyo hususani watoto, Serikali iweze kugharamia matibabu hayo. Kuna baadhi ya chanjo za watoto ambazo wakati wanachanjwa huwaletea homa kali sana. Nashauri Serikali ifanye maboresho kwa chanjo hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, akina mama wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano waendapo kliniki kuchunguzwa afya zao nashauri Serikali itoe vyakula vya lishe kama ilivyokuwa zamani.

Mheshimiwa Naibu Spika, huduma ya usafishaji figo ni gharama sana. Hivyo naishauri Serikali ipunguze gharama za tiba hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali iweke stand by generators katika hospitali zote za Wilaya ili kuweza kusaidia wagonjwa na wauguzi umeme unapokatika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hospitali nyingi majengo yake ni chakavu, ukarabati ufanyike katika hospitali hizo, naishauri Serikali iweke nyavu za kuzuia mbu katika wodi za Hospitali ya Muhimbili na ukarabati wa vyoo na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali iboreshe miundombinu ya hospitali zetu hususani upatikanaji wa huduma ya maji katika hospitali zetu nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, madaktari na wauguzi waongezwe mishahara na posho ili waweze kufanya kazi kwa weledi na kuondoa tatizo la rushwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali iboreshe kambi za wazee, kujenga/kukarabati nyumba zao, chakula cha kutosha na kuwapatia vifaa muhimu katika kambi zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, namuomba Mwenyezi Mungu awape afya njema na umri mrefu Waheshimiwa Ummy A. Mwalimu (Waziri) na Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile (Naibu Waziri) ili waweze kutekeleza majukumu yao ya kila siku katika Wizara hii ambayo kimsingi
ni tegemeo la Watanzania wote hususani katika masuala ya afya.