Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza Wizara kwa kazi nzuri inayoendelea kufanyika. Nashukuru kwa mgao wa magari ya ambulance, mgao wa Madaktari Bingwa na watumishi. Pamoja na pongezi hizi, naomba kutoa ushauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, matibabu ya cancer - Bugando; zipo taarifa kwamba zaidi ya asilimia 30 ya wagonjwa wa cancer - Ocean Road wanatoka Kanda ya Ziwa. Kutokana na takwimu hizo ni vyema Serikali ikaongeza bajeti ya vifaatiba kwa hospitali hii ili kupunguza msongamano wa wagonjwa wanaotoka Kanda ya Ziwa kwenda Dar es Salaam jambo ambalo litapunguza gharama na usumbufu lakini pia litasaidia kupunguza gharama kubwa kwa mgonjwa inayotolewa hivi sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Hospitali ya Rufaa ya Geita; kwanza naipongeza Serikali kwa kutenga fedha za ujenzi wa Hospitali ya Mkoa wa Geita. Hivi sasa wananchi wa Mji wa Geita wanapata taabu sana kwa kukosa hospitali ya level ya Halmashauri ya Wilaya kwa kuwa hospitali yetu ya Wilaya/Mji ndiyo Hospitali ya Mkoa kwa sasa.

Naiomba Serikali kuhakikisha ujenzi wa Hospitali ya Mkoa ambayo ipo Mjini Geita na inasuasua kutokana na uhaba wa fedha. Naitaka Wizara kutofautisha inapozungumza kuhusu Hospitali ya Mkoa inamaanisha hospitali ipi kati ya Hospitali ya Geita Mjini na Hospitali ya Chato. Ni vizuri kutofautisha ili kutoa uelewa mpana wa wananchi kufahamu ni kipi kipaumbele cha Wizara kati ya hizi hospitali mbili za Mkoa ndani ya Mkoa mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upungufu wa watumishi; kwa muda mrefu Hospitali ya Mkoa wa Geita inaendelea kutokuwa na Madaktari Bingwa, hadi leo kuna Daktari Bingwa mmoja tu ambae ni surgeon, wale ambao Wizara iliwapeleka wote hawajafika. Pia kuna upungufu mkubwa wa manesi, wataalam wa kada za maabara, usingizi na madaktari wa kati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza sana TFDA kwa kuendelea kusimamia viwango vya chakula kwa Watanzania. TFDA wanatoza ada kwenye kila leseni ya bar, grocery na migahawa ya shilingi 100,000 kwa mwaka. Ada hii ambayo ambayo ni sharti ya mfanyabiashara kupata leseni katika Halmashauri zetu, kwa ujumla hakuna kazi ambayo TFDA wanafanya kwenye bar kwa kuwa vinywaji vyote vinavyouzwa bar au grocery ni vya kununua na havitengenezwi na muuzaji. Hata kama lengo ni mamlaka hii kukusanya fedha ili iweze kujiendesha, busara ingetumika angalau shilingi 20,000 kwa hoteli kubwa zenye bar na shilingi 10,000 kwa grocery au bar za mitaani kwa kuwa ada hizi zinaongeza gharama kwa wananchi bila sababu yoyote.

Naiomba Serikali ifahamu pamoja na ada ya TFDA kuna ada ya leseni, ushuru, TRA, michango ya mwenge, majengo, ukaguzi wa watu wa afya, usafi na kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu fedha za madeni ya watumishi; Jimbo langu kuna watumishi wengi Hospitali ya Mkoa ambao zamani walikuwa DC wana madeni makubwa na ya muda mrefu. Naiomba Wizara kulipa madeni yote kwa kuwa yameleta usumbufu mkubwa.