Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nichangie katika hoja iliyoko mezani. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai. Nawashukuru wapiga kura wa Urambo ambao wameniwezesha kuwa hapa na nawahakikishia sitawaangusha.
Vile vile nachukua nafasi hii kuishukuru familia yangu inayoongozwa na Mheshimiwa Mzee Sitta, kwa kuniwezesha kufanya kazi ninayoifanya sasa hivi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu muda ni mfupi na mengi ninayo ya kuongea, pengine naweza kushindwa kumalizia; kwanza kabisa, naomba nianze na kutoa maombi na shukurani. Kwanza shukurani kwa Mheshimiwa Dkt. Magufuli, amefanya kazi kubwa sana kuteua Baraza zuri, linafanya kazi sana. Nawapongeza Waheshimiwa Mawaziri wote na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo mmeonesha tayari kwamba mnaiweza. Hongereni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye maombi kwanza halafu ndiyo nieleze ninayoyataka. Mimi najikita katika zao la tumbaku tu, sina jambo lingine. Ndugu zangu, kwa Mkoa wa Tabora tumbaku ndiyo maisha, tumbaku ndio siasa. Kama sitataja tumbaku, sitawatendea haki wanyonge; wakulima walioko Urambo na Mkoa mzima wa Tabora. Mheshimiwa Waziri Mwigulu Nchemba, nakuheshimu sana na najua unaiweza hiyo kazi, ombi langu kwako, huu ni wakati muafaka ambapo masoko ya tumbaku huanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kawaida huwa masoko ya tumbaku yanaanza mwezi wa Nne. Nakuomba Mheshimiwa Waziri, katika kipindi hiki cha Bunge ukipata mwanya, uje Tabora ukutane na wakulima wa Urambo, Sikonge, Uyui, Nzega na Ulyankulu, ukutane na wakulima wote, uongee nao ujionee mwenyewe mateso wanayoyapata. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, asilimia 60 ya tumbaku inatoka Mkoa wa Tabora na kwa msingi huo, ni vizuri Mheshimiwa Waziri ukafika Tabora kwanza ukutane na wakulima wenyewe watakutafutia uwakilishi wao; pili, ukutane na Vyama vya Msingi; na tatu, utakutana na wanunuzi wenyewe. Uwasikie kila watu na vilio vyao ambavyo vinasababisha hali ya mkulima isipande hata siku moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hatuna haja ya kumbembeleza mkulima alime, yeye mwenyewe anahitaji fedha; ukimwezesha masoko ukamwezesha na pembejeo, inatosha, huna haja ya kumbembeleza. Wewe mwezeshe tu, kwa sababu masoko ndiyo kishawishi kikubwa cha mtu alime. Halafu pili, pembejeo zinazofika kwa wakati na bei nafuu. Kwa hiyo, naishauri Serikali yetu kwa kupitia Wizara ya Kilimo ishughulikie masoko kwanza, ndiyo kilio kikubwa cha walima tumbaku. Hilo ombi la kwanza, ufike wewe mwenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitashukuru pia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa heshima kabisa, nakuomba kama ulivyokwenda Mtwara na Lindi ukaona korosho, tunakuomba na wewe Mheshimiwa Waziri Mkuu, uje Tabora uone makato wanayokatwa wakulima. Naamini kabisa, yako mengine utatoka umeagiza huko huko yapunguzwe ili kumpunguzia mkulima makato ambayo yanamfanya aendelee kuwa maskini, katika pembejeo na pia katika bei ya tumbaku yenyewe. Karibuni sana na nitashukuru Mheshimiwa Waziri atakapokuwa ana-wind up atueleze anakuja lini, angalau akituambia yuko tayari na sisi tujiandae kumpokea. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, namwomba Waziri katika ku-wind up, hebu atusaidie, mpaka sasa hivi, Serikali imejitahidi imetafuta wanunuzi kutoka Japan na kadhalika. Bado hawatoshi. Tuna wanunuzi wakubwa watatu kule wamejikita, wamekuwa kitu kimoja. Wewe uliona biashara gani ambayo haina ushindani? Wote wanatoka na lugha moja; si hasara tu kwa mkulima hiyo? Wameshaelewana! (Makofi)
Mheshimiwa Waziri, utakapokuwa una-wind up tunaomba utueleze, mpaka sasa hivi Serikali imefikia hatua gani ya kutafuta wanunuzi wengine wa tumbaku ili zao liwe na ushindani na mkulima naye apate anachostahili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ambalo naomba ujibu wakati unapo-wind up, ni jinsi gani ambavyo Serikali inalifikiria suala la kuwa na Kiwanda cha Tumbaku Tabora? Mkoa wa Tabora unaotoa asilimia 60 ya tumbaku, halafu cha ajabu, inabebwa na magari yanaharibu barabara yanapeleka Morogoro. Sisi tunataka kiwanda kijengwe pale pale. Siyo hivyo tu, ubaya wake ni kwamba, wanunuzi wajanja sana, wanaipima tumbaku ikiwa Urambo au Tabora kwa ujumla; ikifika Morogoro wanapima tena. Kwa hiyo, ile bei anayopewa mkulima ni ile ambayo wamepima Morogoro. Ni haki hii? Gari ikiharibika njiani, ikikaa wiki nzima! Kwa hiyo, Serikali inasemaje kuhusu kujenga Kiwanda cha Tumbaku Mkoa wa Tabora? (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia cha ajabu jamani ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, mliona zao gani lina grade 72? Tumbaku eti ina grade 72! Miaka ya nyuma ilikuwa grade saba; sasa hivi wamenyumbuisha mpaka zimekuwa sasa eti grade 72. Wewe uliona wapi? Shina la tumbaku ni majani 12 mpaka 16; eti majani 12 - 16 yana grade 72, si uonevu tu huo! Kwa hiyo, Mheshimiwa utuambie mtapunguzaje grade za tumbaku utakapokuwa una-wind up. Huu ni uonevu wa hali ya juu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia hivi sasa ninavyoongea, Urambo na naamini Wabunge wenzangu, kwenu masoko ya tumbaku hayajaanza. Kwa kawaida Masoko ya tumbaku yanaanza mwezi wa Nne na kuitendea haki mara nyingi, iishe mwezi wa Nane na ikizidi kabisa mwezi wa Tisa mwisho. Mwaka 2015 wameendelea mpaka mwezi wa Kumi na Moja. Unajua tatizo lake ni nini? Inavyozidi kukawia na thamani inazidi kushuka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashangaa! Naomba Mheshimiwa Waziri utakapokuwa una-wind up utuambie, kwa nini bodi mpaka sasa hivi hawajaenda kuhimiza uanzaji wa masoko ya tumbaku na kwamba mtaiwezeshaje Bodi ya Tumbaku ili ifanye kazi kikamilifu ili kweli masoko ya tumbaku yaanze kwa wakati na yaende kwa haraka? Sasa hivi masoko ya tumbaku yanaweza kufanyika hata mara moja tu kwa mwezi, ambapo miaka ambayo ilikuwa inafanya vizuri, ilikuwa na masoko hata mara tatu au mara nne kwa mwezi, jambo ambalo lilikuwa linawasaidia sana wakulima. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hayo ndiyo ambayo naomba mtakapokuwa mna-wind up mtuelezee mikakati yenu kama Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nadhani nimezungumzia kuhusu makato mbalimbali ambayo mtatueleza kwamba makato haya, mtayapunguza kwa kiasi gani. Nilikuwa naangalia makato ya mkulima, jamani ndugu zangu, kama kuna mtu anayeyonywa hapa duniani, ni mkulima wa tumbaku. Eti kuna Kodi ya Kupakua, Kodi ya Usafirishaji, Kodi ya Damage, yaani kuharibika; eti Kodi ya Insurance! Ninyi mliona wapi mkulima na mambo ya insurance. Halafu sasa akishauza, anakatwa; Halmashauri inachukua, Union inachukua, Vyama vya Msingi vinachukua; yeye mkulima abaki na nini? Kwa hiyo, nafikiria haya ndiyo makato ambayo tunategemea mtatusaidia kuona ni jinsi gani ambavyo mnayapunguza.
Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu kama nilivyosema, tukija kwa upande wa kilimo cha tumbaku, nimeomba kwamba wakati wa ku-wind up Mheshimiwa Waziri azungumzie jinsi gani atakavyoiwezesha Bodi ya Tumbaku.
Bodi ya Tumbaku ndugu zangu ndiyo ambayo inaajiri classifiers, wale wanaopanga madaraja (grade) za tumbaku. Sasa utakuja kukuta kwamba wengi wamestaafu, Serikali haijaajiri mpaka sasa hivi. Kwa Wilaya zetu za Mkoa wa Tabora, Wilaya moja haipaswi kuwa na chini ya classifiers watano. Eti sasa hivi katika Wilaya zetu zote zilizoko Mkoa wa Tabora, zile zinazolima tumbaku wako classifiers watatu. Mmoja aende Kaliua, mwingine aende Ulyankulu na mwingine Sikonge. Wataweza wapi?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unakuta classifier mmoja anapanga mabelo 1,500 kwa siku, saa 3.00 mpaka saa 11.00, si wizi tu huo! Yeye ana akili gani ya kupanga belo 1,500 kwa siku? Kwa hiyo, badala yake bei wanabambikiziwa tu. Halafu walivyofanya ni kwamba, mpaka uipate hiyo hela; tumbaku inatakiwa kama ikiwa nzuri ilipwe Dola tatu angalau kwa kilo, lakini walivyozipanga sasa.
MHE. MARGARET S. SITTA: Sijui hiyo kengele ndiyo ya kwanza au ya mwisho!
NAIBU SPIKA: Ya mwisho Mheshimiwa!
MHE. MARGARET S. SITTA: Ooh! karibuni sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, mjionee wenyewe tunavyonyanyaswa huko.