Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nachukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia uhai ili niweze kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii.

Naomba nianze kuwapongeza Mawaziri wote wawili na watumishi wote wanaohudumu kwenye Wizara hii. Sina budi kushukuru kwa kile kidogo nilichojaliwa kupata kwenye jimbo langu la Liwakle kwa kunipatia watumishi wanne, Mungu awabariki sana.

Sasa naomba kuchangia/kugusia suala la wazee nchini. Imekuwa ni jambo la muda sasa tangu Serikali iahidi kuleta sheria ya wazee humu Bungeni. Kwani pamoja na matamko mengi juu ya wazee kama vile makazi bora kwa wazee, matibabu bure kwa wazee na kadharika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo haya hayawezi kukamilika bila kwanza kuwatambua hao wazee ni akina nani kwa mujibu wa sheria. Hivyo ni bora sasa sheria hiyo ikaletwa ili tuweze kuwatambua hao wazee. Pamoja na juhudi kubwa inayofanywa na Serikali ya kuboresha miundombinu ya afya juhudi hizi zinaweza zisilete matunda tarajiwa kwa kuwepo na tatizo la uhaba wa watumishi kwenye Wizara halitatatuliwa. Kwa kuwa sehemu kubwa ya watumishi hawa wanashughulikia afya ya watu, hivyo weledi mkubwa unahitajika, hivyo watumishi wachache kuhudumia watu wengi kunawaondolea umakini na kukosa ufanisi, kwa mfano katika Hospitali ya Wilaya ya Liwale ina watumishi wachache sana hospitali ina wodi za grade II, kwa saa za usiku wodi hizi zote zina huduma na wauguzi wasaidizi, ni zahanati nne tu ndio zinahudumiwa na clinical officers wasaidizi. Jambo hili ni baya sana kwani ikitokea akiwa likizo zahanati husika hufungwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Liwale iko mbali sana na Hospitali ya Rufaa ya Sokoine, Lindi. Jambo hili limefanya umuhimu wa kuwa na gari kwani umbali uliopo ni zaidi ya kilometa 300. Hospitali pekee ya karibu ni ya Ndanda iliyoko Masasi, Mkoani Mtwara, kwa sababu hizo uhitaji wa vifaa bora na Madaktari Bingwa ni muhimu sana kwa hospitali ambayo haina usafiri na haina Madaktari Bingwa ni hatari ya wagonjwa kufia njiani ni kubwa sana wakati wakielekea Ndanda kwa kutumia magari ya abiria. Naomba jambo hili lingepewa msukumo wa kipekee.

Mheshimiwa Naibu Spika, maduka ya MSD yameongezeka kuwa msaada mkubwa sana katika idara hii ya afya, hivi imefikia wakati sasa maduka hayo sasa yangepatikana katika Mikoa a Wilaya zote nchini hasa kwenye zile Wilaya ambazo ziko mbali na Makao Makuu ya Mikoa ambako kuna maduka hayo, lakini vilevile pale ambapo maduka hayo yapo basi ni bora dawa zote muhimu zikapatikana ikiwa ni pamoja na vitendea kazi vingine yaani vifaatiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bima ya Afya imeonesha kuwa na manufaa makubwa kwa jamii. Changamoto pekee katika utekelezaji wa jambo hili ni elimu duni katika jamii juu ya uchangiaji na uandikishaji wake. Lakini jambo lingine ni tatizo kwenye Halmashauri zetu ni juu ya uchangiaji wa CHF, pamoja na jamii kuendelea kupewa elimu . Lakini mchango wa fedha za kutoka Serikali hazipatikani kwa maana ya tele kwa tele, jambo hili linalea mkanganyio mkubwa kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa zahanati na nyumba za watumishi sasa jambo hili linaachwa kwenye Halmashauri. Lakini mkumbuke kuwa Halmashauri hizo kwa sasa zina mzigo mkubwa sana. Mfano ujenzi wa maabara za shule za sekondari, nyumba za walimu, vyoo vya shule na walimu na majengo mengine. Hivyo ni bora Serikali ikaona upo umuhimu wa kuzisaidia Halmashauri kujenga zahanati kila kijiji na kituo cha afya kila kata kama Sera ya Taifa inayotaka ujenzi wa vituo vya afya na zahanati ukiachwa chini ya Halmashauri, kwenye Halmashauri zenye mapato kidogo jamii itaendelea kuteseka maana Serikali ya Awamu ya Tano mara zote wanasema hakuna miradi mipya itakayoanzisha mpaka Halmashauri husika yaani Serikali kazi yake ni ku-support tu nguvu za wananchi mahali ambapo wananchi hawana uwezo, patabaki kuwa nyuma kimaendeleo ya kiafya. Na sera ya kuwa na kituo cha afya kila kata haitafikiwa kwani Halmashauri zetu nyingi zina uwezo mdogo na zina mzigo mkubwa sana ikiwa ni pamoja na matamko ya mara kwa mara ya kutoka Serikali Kuu.