Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Mashimba Mashauri Ndaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Maswa Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Afya.

Kwanza niwashukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na Naibu wake kwa kutupeleka mbele kwenye suala la afya kwenye nchi yetu. Wakati tunaanza Bunge hili kulikuwa na kelele za upatikanaji wa dawa, dawa zilikuwa hazipatikani kwenye zahanati, vituo vya afya na hata hospitali zetu, lakini leo tuna asilimia kama 80.

Pia kulikuwa na kelele za upatikanaji wa dawa za chanjo wakati tunaanza Bunge hili leo hatusikii kelele hizo zikiwapo, nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu wake. Kiwango cha chanjo kwenye nchi yetu kimepanda mpaka asilimia 90 na kwa Afrika kama taarifa yao ilivyosema tuko watatu baada ya Rwanda na Zambia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwapongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa ujenzi wa miundombinu pamoja na upatikanaji wa vifaa na vifaa tiba. Niwashukuru sana kwa ajili ya kuniletea vifaatiba kwenye kituo changu cha afya cha Malampaka, tumepata vifaatiba vizuri vya kisasa vingi vinatosheleza pia tumepata pesa za kutosha kuweza kujenga wodi pamoja na majengo mengine, tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala la upungufu wa watumishi wa afya sasa hivi kwenye nchi yetu ni mkubwa. Taarifa ya kamati inasema tuna upungufu wa asilimia 48, hiki ni kiwango kikubwa sana na hiki kinaenda mpaka kwenye maeneo yetu. Mkoa wa Simiyu tuna wataalam wenye ujuzi ambao wanaweza wakahudumia wagonjwa wachache sana. Kwa taarifa nilizonazo ni kwamba mwaka 2012 wakati mkoa unaanza tulikuwa na wataalam wenye ujuzi asilimia 2.6, lakini mwaka 2016 wameongezeka kidogo asilimia 4.8. Sasa ukijaribu kuangalia kiwango hiki ni kidogo sana. kwa Wilaya yangu ya Maswa ina upungufu wa watumishi wa afya 525, uhitaji ni 726 na waliopo ni 201 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo upungufu huu ni mkubwa Sana na nilkuwa nasihi kwamba Serikali sasa iangalie tatizo hili kama tatizo kubwa linaloikumba nchi yetu na lishughulikiwe kwa pamoja Wizara ya Utumishi, Wizara ya Afya pamoja na Wizara ya TAMISEMI. Vinginevyo lishughulikiwe kama ambavyo tumeshughulikia tatizo la upatikanaji wa walimu kwa shule zetu. Suala hili lazima lifanyiwe hivyo vinginevyo watu wetu watakuwa wanaangamia kwa sababu ya kukosa huduma kwenye vituo hivi ambavyo tuna bidii kubwa ya kuviboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala lingine ambalo halijazungumzwa kabisa; kuhusu uzazi wa mpango. Uzazi wa mpango sijaona hata kwenye hotuba ya Kamati hata hotuba ya Mheshimiwa Waziri mwenyewe. Hata hivyo najaribu kuangalia kwa mbele kwamba idadi ya watu inaongezeka kwa kasi sana. Nchini mwetu sasa inakadiriwa kuwa na watu kama milioni 58 na tunavyoendelea mpaka mwaka 2022 pengine tutakuwa watu milioni sitini na kitu; na kwa kuangalia vizuri watoto watu walio chini ya umri wa miaka 15 kwenye nchi yetu ni nusu ya Watanzania. Sasa utaona Watanzania hawa watu wazima wanahudumia watu wengi kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja ahsante sana.