Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia kwenye Wizara hii muhimu sana. Kwa kuanza nitambue jitihada za Mawaziri na timu zao kwenye Wizara hii kwa kazi wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu kwa leo kwanza niongelee juu ya magonjwa yasiyo ya kuambukizwa ambayo yamekuwa common sana kwenye jamii yetu na kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri sikuona kama kuna eneo yamepewa msisitizo sana. Kuna magonjwa kama kisukari, shinikizo la damu na kadhalika kama hayo, yamekuwa ni ya kawaida sana kwenye jamii yetu na yamekuwa yanapoteza maisha ya watu wengi sana kwenye maeneo hasa ya vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ushauri wangu kwenye eneo hili, niombe Serikali kupitia Wizara kama ambavyo imekuwa inafanya kwenye matatizo ya UKIMWI, zahanati zetu vituo vya afya na hospitali viwe na dawa hizi na ikiwezekana kusiwe na gharama wakati wa kupata dawa hizi ili watu wetu waweze kupata madawa haya na huduma kwa urahisi kwenye maeneo yetu ya vijijini na kwa hivyo kuweza kuokoa maisha ya watu wetu wengi sana wanaopoteza maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nafikiri nilichangie, nimeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kaongelea namna ambavyo kumekuwa na mkakati wa kuimarisha hospitali za rufaa na hospitali za mikoa. Nikizungumzia kwenye Jimbo langu ya Ukerewe, sisi hospitali yetu ya rufaa ni hospitali ya wilaya hasa kutokana na jiografia yetu na kwa maana hiyo msaada mkubwa ambao tungeweza kuupata kwenye Visiwa vya Ukerewe na akatusaidia sana ni kuimarisha hospitali yetu ya Wilaya Hospitali ya Nansio.

Mheshimiwa Naibu Spika, sawa tumekuwa na maboresho ya wakati fulani lakini bado tuna tatizo kubwa sana la wataalam kwenye hospitali yetu ya Wilaya. Kama mnavyojua jiografia ya ukerewe ni ya visiwa, sasa yanapotokea matatizo ya dharura kwa mfano wagonjwa wanaohitaji kupata rufaa na wakati huo usaifiri wetu una limited time, ikifika jioni hakuna usafiri wa kuvusha wagonjwa kwenda maeneo mengine. Tunashukuru kwamba tumepata shilingi milioni 200 kwa ajili ya kununua boti, lakini bado haiondoi umuhimu wa kuongeza wataalam na Madaktari kwenye hospitali yetu ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, tunashukuru kwamba tumepata shilingi milioni 200 kwa ajili ya kuboresha Kituo cha Afya cha Bwisya ambayo itasaidia sana. Kituo kile kinahudumia zaidi ya watu 30,000 kwenye Kisiwa cha Ukala, lakini wakati tunakamilisha ujenzi wa kituo kile cha afya Mheshimiwa Waziri niombe sana sambamba na kukamilisha kituo kile Wizara basi ione uwezekano, kama jambo la muhimu sana kufanya maandalizi ya wataalam kwa ajili ya kuhudumu kwenye vituo hivi ambavyo tumekuwa tunaviboresha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kile ni kituo kikubwa, kinakamilika lakini mpaka sasa kina watumishi sita pekee, jambo ambalo kama litaendelea kuwa namna ile hata kama kitakamilika hakitakuwa na tija. Kwa hiyo, niombe sana kwa Mheshimiwa Waziri, hiki Kituo cha Afya cha Bwisya kinaelekea kukamilika, basi tupatiwe wataalam wa upasuaji lakini na Madaktari kwa ajili ya kutoa huduma, sambamba na upatikanaji wa gari la wagonjwa kwa ajili ya kuhudumia kwenye kituo kile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema mwanzo kutokana na jiografia yetu tuna matatizo makubwa ya afya na ningefurahi sana kama wakati wa kuhitimisha Mheshimiwa Waziri angeongelea maeneo tata hasa kimazingira kama Ukerewe, Serikali ina mkakati gani kuweza kuboresha huduma za afya ili kuweza kuokoa maisha ya akinamama na watoto ambao mara kwa mara wamekuwa wanapoteza maisha kutokana na jiografia au mazingira kama hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Visiwa vyetu vya Ukerewe bahati nzuri Mheshimiwa Waziri, tumekuwa mara kwa mara tunabadilishana mawazo juu ya kutusaidia kwenye visiwa vyetu vya Ukerewe. Kisiwa cha Ilugwa, kutoka Kisiwa cha Ilugwa kuja Wilayani kuna karibu saa tano ambazo mgonjwa anatakiwa asafiri na kule tuna zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ili kuweza kuwasaidia wananchi wale ambapo Ilugwa ile zahanati inahudumia zaidi ya visiwa vitano, inahudumia watu zaidi ya 20,000, tuombe basi zahanati hii iweze kusaidiwa kupandishwa kuwa kituo cha afya ili iweze kutoa huduma zinazostahili.