Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. VEDASTUS E. NGOMBALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami nitoe mchango wangu kwa Wizara hii ambayo inahusiana na afya ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kwa kutoa pongezi kwa Serikali kwa kutuwezesha kwa kutupa fedha katika Kituo cha Afya cha Kilwa Masoko shilingi milioni mia tano, Kituo cha Afya Pande, Kituo cha Afya Tindi shilingi milioni mia nne pamoja na ambulance. Tunashukuru sana kwa hilo, lakini pia tunaomba tupate pesa kwa ajili ya Kituo cha Afya Njinjo ili basi huduma ya afya iweze kwenda sawasawa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala zima la sera ya huduma bure kwa akinamama wajawazito pamoja na watoto walio chini ya miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la sera ya huduma bure kwa akinamama wajawazito pamoja na watoto chini ya miaka mitano. Ni sera inatekelezwa, lakini bado ina changamoto kubwa. Kuna changamoto kubwa kwamba bado huduma hii haitolewi ipasavyo, bado akinamama wanahitajika wajiandae kwa vifaa kwa ajili ya kwenda kujifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limezungumzwa suala la delivery kit, naomba suala hili liwe wazi, elimu itolewe, wananchi wafahamu stahili yao kutokana na huduma hii, kama linachangiwa au linatolewa bure ili basi kila mwananchi aweze kupata huduma hii ipasavyo. Kwa hali iliyopo sasa suala hili ni kama limejifichaficha na akinamama wetu kule wanalazimika kuagizwa viwembe, mipira, wanaagizwa kanga; kumekuwa na vurugu na Serikali bado haijaweza kutatua tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nizungumze, kwangu kuna hospitali ya mission. Serikali imeingia mkataba na Hospitali ya St. Mark’s Kipatimu pale na kwa hivyo, akinamama wanatakiwa wapate huduma hii bure, lakini kumekuwa na changamoto katika hospitali hii na hasa pale Serikali inapochelewesha kupeleka pesa katika ule Mfuko wa Basket Fund. Uongozi wa hospitali ukiona Serikali imechelewa kupeleka fedha pale, wanachokifanya ni kuwatoza akinamama wajawazito gharama hizi za kujifungua. Kwa hiyo, hii sera ya utekelezaji huduma bure kwa akinamama wajawazito ni kama haieleweki kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila nilipojaribu kuona sasa baada ya kuwa wamepata hizi pesa wanawezaje kuwarudishia wale akinamama pesa zao, inakuwa ngumu, nimefuatilia mara nyingi, lakini majibu hayajapatikana. Ninao ushahidi wa receipts ambazo wamelipa. Kwa hiyo, ninaomba ulisimamie hili, ili basi wananchi wapate haki zao, kwa sababu ni sera kwamba, huduma ya mama mjamzito na mtoto ni bure, lakini pale pana changamoto kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, katika ule mkataba tunaomba tupate maelekezo ya gharama za huduma zinazotolewa na hospitali hizi. Gharama zimekuwa za juu mno, tupate maelezo tufahamu sasa kwamba, gharama wanazotakiwa kutoa hospitali binafsi ni zipi; gharama zimekuwa juu mno kiasi kwamba wananchi wetu wanashindwa ku-afford. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Wizara ya Afya ilifuatilie hili kwa sababu, wananchi wanapata shida katika suala zima la gharama za matibabu katika eneo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la tatizo la maji katika Hospitali ya Wilaya ya Kinyonga, pale Kivinje. Hospitali yetu ya Wilaya ya Kilwa ina tatizo la maji. Mpaka leo wagonjwa wakienda pale suala zima la maji ni kizungumkuti. Kwa hiyo, tunaomba Wizara iliangalie tatizo hili na ilitatue haraka iwezekanavyo kwa sababu, pamekuwa na mashaka ya upatikanaji wa maji katika Hospitali ya Kilwa Kivinje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la ujenzi wa vituo vya afya pamoja na ujenzi wa zahanati. Wananchi katika jimbo langu wamejitahidi kujitolea kujenga zahanati, lakini mpaka sasa zile zahanati zimeisha, lakini bado hazijafunguliwa. Kuna Zahanati za Pungutini, Miyumbu, Marendego, Kipindimbi, Nambondo pamoja na Ongwe. Hizi zahanati zimekamilika kwa nguvu za wananchi lakini mpaka sasa hazijafunguliwa. Tuiombe Serikali ijitahidi kuhakikisha kwamba zahanati hizi zifunguliwe ili wananchi wetu waweze kupata huduma ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la huduma bure kwa wazee. Ni sera ya Serikali kwamba wazee sasa wapate huduma bure, lakini suala hili ni kama halijasimamiwa ipasavyo. Kule kwangu mpaka sasa haieleweki kuna taratibu gani kwa hawa wazee kupata ile huduma. Ilitokea mara moja tu Mkurugenzi alitoa tangazo kwamba wazee wajiandikishe ili waweze kupata utaratibu wa kuweza kupata hizo huduma bure. Hata hivyo, mpaka sasa ni wazee wachache sana wamesajiliwa katika utaratibu ule. Tuombe Serikali itoe elimu zaidi ya namna gani wazee wetu watatibiwa bure, suala hili ni muhimu na ni suala la kisera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la walemavu. Ndugu yangu Mheshimiwa Mussa hapa amezungumza, nami nimekuwa nikilizungumza mara nyingi. Serikali bado haijaliona kwa kina suala la mahitaji maalum kwa walemavu. Kwa mfano katika Wilaya yangu ya Kilwa, katika Jimbo langu la Kilwa Kaskazini, takribani walemavu wa ngozi 15 tulilazimika kuwapeleka Ocean Road kwa ajili ya kupata matibabu ya mionzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya kupata hayo matatizo ya ngozi ni kutokana na kukosa hitaji lao maalum la kupata mafuta ya kuwakinga dhidi ya athari ya miale ya mwanga. Tumekuwa tukisema mara nyingi, kama Serikali imeweza kuhudumia mama mjamzito na mtoto wa miaka mitano kwa nini isiweze kutoa mafuta bure kwa walemavu wa ngozi? Hawa walemavu wa ngozi wanaishi katika maisha ya kawaida kabisa na wakati mwingine hawajui hii bidhaa inapatikana wapi? Hili ni lazima lionwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sio hilo tu, sisi sote ni walemavu watarajiwa, lakini mpaka leo Serikali bado hospitali zinazohusika na kutoa viungo bandia zinatoa kwa gharama ya juu mno. Leo ukitaka mguu bandia lazima uwe na milioni tatu, ni hela nyingi kwa mlemavu na hatuwezi kujua mlemavu ni nani? Sijui Serikali inalionaje suala hili? Suala la walemavu, ni asilimia ngapi walemavu katika nchi hii? Kwa nini mahitaji yao maalum yasitolewe bure? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwa mlemavu si suala la kuchagua, kama tunatoa huduma kwa mama wajawazito, tutoe huduma kwa walemavu. Kuwa kipofu, kuwa kiziwi au kuwa mlemavu wa ngozi si suala la kuchagua. Mahitaji maalum kutokana na ulemavu wao ni suala ambalo Serikali inatakiwa iliangalie, sasa nashangaa kwamba leo tuna walemavu wa ngozi tunawapeleka Ocean Road tena kwa kuchangishana ilhali Serikali ipo. Serikali ifanye sensa ya walemavu wa ngozi, vile vile Serikali itoe huduma ya mafuta haya bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)