Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie katika mjadala uliokuwa mbele yetu kuhusu hoja hii katika Wizara yetu hii ya Afya. Nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa afya na uzima tumeikuta jioni hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na pongezi na shukrani, Wizara ya Afya hii imefanya mambo makubwa sana, hasa katika uimarishaji wa upatikanaji dawa pamoja na uboreshaji wa vituo vya afya nchi nzima. Nitolee mfano kwangu nimepata kituo kimoja pale kwenye Kata yetu ya Mkuyuni, pia tumepata kituo kingine katika halmashauri hiyo hiyo katika eneo la Dutumi, niwapongeze sana kwa hayo yote. Pia tumepata katika mgao unaokuja katika bajeti hii tutengewa 1.5 bilioni kwa sababu ya hospitali ya wilaya, tunaishukuru sana Serikali hasa Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mazuri hayo kuna ombi ambalo nataka niombe. Mheshimiwa Waziri wa Afya, pamoja na mambo mazuri anayotufanyia lakini tuna ahadi za Mheshimiwa Rais tangu 2010 kuhusu upatikanaji wa magari ya wagonjwa kwenye Kituo cha Afya Mkuyuni na Kituo cha Afya Kinole; ahadi hizi ni za muda mrefu, namwomba sana ikiwezekana aziingize ili atupatie turahisishe huduma ya afya katika jimbo letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia watumishi wa afya wako wachache; tuna zahanati ambazo tumeshazimaliza, kwa mfano Zahanati ya Bamba, tangu mwaka jana imekwisha, kuna Zahanati ya Tununguo, kuna Zahanati ya Kidugalo, zote hizi tunashindwa kuzifungua kwa sababu ya ukosefu wa watumishi wa afya. Nimwuombe sana atupatie hao watumishi ili tupeleke huduma karibu kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia kidogo kwa umbali ile ripoti ya CAG; nimegundua, kuwa pamoja na kwamba wanafanya juhudi kubwa katika upatikanaji wa dawa lakini Shirika la Dawa la MSD linadai zaidi ya bilioni sitini na moja. Niwaombe sana hizi pesa kwa sababu zilikuwa zitolewe na global fund na hazijatolewa mpaka leo niwaombe sana Serikali muisaidie MSD ili fedha hizi zipatikane ili tuweze kuongeza upatikanaji wa dawa katika hospitali zetu, zahanati na vituo vya afya ili tuweze kuwahudumia wananchi vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe sana Serikali waisukume hii MSD, imekuwa ni msaada mkubwa sana na inatuletea sifa ndani ya nchi na nje ya nchi hasa baada ya kupata ule mkataba wa usambazaji dawa katika nchi za Afrika ya Mashariki pamoja na Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo katika ripoti ya CAG tumegundua pia kwamba sasa hivi kuna upungufu wa zaidi ya 1.5 trillion kwenye ripoti ile. Kwanza lazima nikiri, maana tusije kupotosha kitu ambacho CAG amekiweka ni kweli kuna mapungufu ya 1.5 trillion haionekani. Hii ni Serikali ya kwetu na tusiposema ukweli tutakuwa hatujaitendea haki, tusipende kona kona wakati jambo ni kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa kuliko chote CAG ndilo jicho la Wabunge na sisi Wabunge ni wawakilishi wa wananchi. Kwa hiyo anaposema CAG anatusemea sisi Wabunge na anawasemea wananchi wote wa Tanzania kwa sababu ndio wenye mali. Sasa leo CAG amezungumza kwamba kuna pesa ambazo hazionekani 1.5 trillion halafu sisi wenye mali tukisema tukishabikia tunakosea sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwa kirefu katika hili kwa sababu ndio umekuwa mjadala kwenye mitandao ya kijamii na kuna upotoshaji mkubwa kwenye hili. Hii ripoti ya CAG imekuja hapa Bungeni baada kwanza kukabidhiwa Mheshimiwa Rais pale Ikulu kwa mujibu wa Katiba na Sheria inavyotaka. Kwa hiyo Mheshimiwa Rais kama angetaka isije au angetaka kufanya uchakachuaji wowote angeichakachua siku ile pale Ikulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulimsikia kwa macho yetu Mheshimiwa Rais akimpongeza CAG mwenyewe Profesa kwamba wewe ni mtu mwema, ni mcha Mungu, naamini hukumwonea mtu katika ripoti hii na tutaifanyia kazi. Sasa akitokea mtu mwingine akianza kusema kwamba Rais anakumbatia haijulikani ni upotoshaji.

T A A R I F A. . .

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu na huyu ni ndugu yangu tunaheshimiana sana kwa sababu mimi naongelea taarifa ya 1.5 trilioni yeye anaongelea ATC ni vitu viwili tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hilo nilikuwa nazungumza kwamba Mheshimiwa Rais mwenyewe alijipambanua katika vita vya ufisadi na rushwa na kwa namna yoyote ile hawezi kufumbia macho hili na ninavyomjua Mheshimiwa Dokta John Pombe Magufuli na ndio maana aliipokea na aliruhusu ile taarifa ije hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili tulimwona Mheshimiwa Waziri Mkuu pia akipokea maelekezo kwa Mheshimiwa Rais baada ya kupokea taarifa hii kwamba wataifanyia kazi hasa pamoja na hayo mapungufu, maana yake ukisema unaifanyia kazi na huu upungufu upo lazima wamekubali kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali na niitake Serikali hili jambo si la kupuuza, ni jambo ambalo limezungumzwa na CAG katika ripoti yake ambayo sisi Wabunge na wananchi wa Tanzania ndio jicho letu. Kwa hiyo tunapoona 1.5 trillion haina maelezo ya kutosha tunapata mashaka. Nimtake Waziri wa Fedha na Serikali kwa ujumla atuletee majibu ya kuridhisha katika hili sio kuanza kupiga kona kona ili kwamba kweli tuone Serikali hii na Mawaziri wanamuunga mkono Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli katika vita hii ya ufisadi na rushwa iliyokuwepo nchini kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna namna yoyote lazima tupate majibu ya uhakika, Bunge hili ni moja, katika maendeleo hakuna vyama iwe CCM, iwe CHADEMA, iwe CUF, iwe ACT hakuna mtu anayetaka ufisadi wowote. Tunamtaka Waziri wa Fedha alete hapa majibu ili tuone namna gani na huu ubabaishaji uishe, tumechoka.